WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Sunday, October 14, 2012

WINGU ZITO:Utata wagubika kifo cha RPC Barlow



Utata umegubika mauaji ya Kamanda wa 

Polisi mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow, baada ya kupigwa risasi na watu wanaosadikiwa kuwa majambazi usiku wa kuamkia jana.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Evarist Ndikilo, aliwaambia waandishi wa habari ofisini kwake jana kuwa Barlow, aliuawa maeneo ya Kitangiri katika barabara inayoelekea Bwiru, jirani na hoteli ya Tai Five jijini hapa. Alisema mauaji hayo yalifanyika kati ya saa 7 na saa 8 usiku, wakati Barlow akimsindikiza mwanamke aliyejulikana kama Doroth Moses. Inasemekana kuwa wote wawili, walikuwa wametoka kuhudhuria kikao cha maandalizi ya harusi ya mtoto wa dada wa Barlow, kilichofanyika hoteli ya Florida.

Hata hivyo, taarifa zisizo rasmi kutoka mitandao ya kijamii kuhusu utata wa mauaji hayo, zinaeleza kuwa Barlow na mwanamke huyo walikuwa wanatoka katika hoteli inayotajwa kwa jina la La-Kairo. Akifafanua, Ndikilo alisema Barlow alikuwa akiendesha gari yake binafsi aina ya Toyota Hilux- double cabin na kwamba alikuwa akimsindikiza mwanamke huyo kwenda nyumbani kwake.
Mwanamke huyo ambaye anashikiliwa na polisi kwa mahojiano zaidi, ni mwalimu katika Shule ya Msingi Nyamagana. Alisema wakati wakikaribia eneo la Kitangiri anakoishi mwanamke huyo, waliwaona watu wawili wakiwa wamevaa mavazi maalum (jackets) yanayovaliwa na wananchi wanaoshiriki ulinzi shirikishi unaofahamika pia kama polisi jamii. Kwa mujibu wa Ndikilo, baada ya kuwaona watu hao ambao waliwamulika kwa tochi, Doroth alimuuliza Barlow iwapo anawafahamu, naye alimjibu kuwa watakuwa ni polisi jamii.
Hata hivyo, Ndikilo alisema baada ya Barlow kusimamisha gari pembeni, mkabala na nyumba anayoishi mwanamke huyo, watu hao wawili waliwasogelea huku wakionyesha kukerwa na mwanga wa taa za gari. Alisema watu hao walimhoji Barlow kwa nini anawamulika kwa taa za gari, lakini wakati akijaribu kutoa ufafanuzi kwamba yeye ni RPC, ghafla walitokea watu wengine wapatao watatu, walisimama kuzunguka gari la Kamanda huyo.
Baada ya kuona hali hiyo, huku akijaribu kuwauliza iwapo hawamfahamu kuwa yeye ndiye RPC na kutoa radio call (simu ya upepo) ili kufanya mawasiliano na polisi wa doria. “Ghafla mmoja wa watu hao alitoa bastola na kumfyatulia risasi ambayo iliingilia shingoni na kutokea upande wa pili wa bega,” alisema Ndikilo.
Alisema baada ya tukio hilo, watu hao walichukua vitu kadhaa ikiwemo bastola, simu na radio call alivyokuwa navyo Barlow na kutoweka kusikojulikana. “Kimsingi mazingira ya mauaji yenyewe bado yana utata, lakini Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi tunafanya kazi ya kuchunguza ili kuujua ukweli,”alisema.
Kwa mujibu wa Ndikilo, baada ya kufyatuliwa risasi inaaminika Barlow alikufa papo hapo kutokana na kuvuja damu nyingi na mwili wake umehifadhiwa katika hospitali ya rufaa ya Bugando ukisubiri taratibu za mazishi. Alisema kutokana na mazingira hayo ya utata ya mauaji, Jeshi la Polisi linamshikilia mwanamke aliyekuwa naye kwa mahoajiano zaidi. Taarifa za awali zilidai kwamba mwanamke huyo anayesadikiwa kuwa ni mjane, ni dada yake Barlow.
Lakini baadaye jana, Mkuu wa mkoa wa Mwanza alikanusha taarifa hizo na kusisitiza kuwa ni mtu ambaye alikuwa amempa lifti wakati wakitoka katika kikao cha harusi. Kufuatia mauaji hayo Ndikilo alisema kuwa Polisi Makao Makuu, limemtuma Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) Robert Manumba kuongeza nguvu ya uchunguzi wa tukio hilo.
Nyumbani kwa Doroth, kijana Kenrogers Edwin aliyejitambulisha kama mtoto wa kaka yake wa mwanamke huyo, alisema kabla ya tukio hilo, shangazi yake (Doroth) alipiga simu ili wamfungulie geti. Alisema kwamba wakati akifungua geti, aliona gari likiwa limeegesha huku watu wawili wakiwa upande wa abiria na wengine watatu wakiwa upande wa dereva na kisha alisikia mlio wa risasi na baadaye watu hao walitimua mbio baada ya kuona pikipiki inakuja nyuma yao.
Baadhi ya wananchi waliozungumzia mauaji hayo walielezea kushangazwa kwao na hatua ya Barlow kutembea usiku bila mlinzi wake (bodyguard) ambaye kwa kiwango kikubwa angeweza kusaidia kumuepusha na kifo.
IGP MWEMA AMTUMA DCI KWA UPEPELEZI
Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) Said Mwema, katika taarifa aliyoitoa jana jijini Dar es Salaam, alisema ameshamtuma Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai DCI Robert Manumba, mkoani humo kuimarisha ulinzi na upepelezi wa tukio hilo.
Aidha, Mwema amewaomba wananchi kuwa watulivu na kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo, utakaowezesha kuwabaini wahalifu hao. Akielezea kuhusu mauaji hayo, Mwema alisema, wakati huo Barlow alikuwa akitokea kwenye kikao cha harusi ya ndugu yake eneo la Florida hoteli Mwanza mjini. Alisema alikuwa ameongozana na ndugu yake wakitoka kwenye kikao hicho. Alisema tukio hilo limewashtua na kuwahuzunisha na kwamba wakati uchunguzi ukiendelea, wataendelea kutoa taarifa kadri wanakavyozipata. ….
MAKAMANDA WA MIKOA WATOA KILIO
Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya makamanda wa polisi wa mikoa mbalimbali nchini, wamesema kuwa wamempoteza kiongozi mwenye uzoefu wa muda mrefu kazini na aliyekuwa mchapakazi katika jeshi hilo. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela, alisema ukomavu wa kazi ndio uliosababisha kamanda huyo kupelekwa katika mkoa ambao ni miongoni mwa mikoa migumu nchini.
Alisema enzi za uhai wake, alikuwa akiwaelimisha wenzake ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi na kwamba alikuwa mwepesi kuwarekebisha wale wanaoenda kinyume na kazi. Kenyela alisema kwa upande wake atamkumbuka kwa sababu ndiye aliyempokea wakati akianza kazi hiyo na alikuwa akiishi naye kwenye kambi za maofisa huko Tabata.
“Wito wangu kwa wananchi walaani vitendo vya mauaji ya viongozi kwa sababu kumpoteza kiongozi ni gharama kubwa katika nchi hasa ukiangalia muda uliotumika kumuandaa hadi amefikia hatua hii,” alisema. MOROGORO Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, alisema kuwa, ameguswa na msiba huo wa ghafla na kueleza kuwa, atamkumbuka daima kwa kuwa alikuwa akifanya kazi yake kwa kujiamini.
“Tumempoteza jembe kwa sababu alikuwa mzoefu kwenye kazi na asiye mchoyo pindi umwombapo ushauri, kwa wale wachanga kwenye kazi walikuwa wakimtumia sana ili waweze kuifanya kazi yao kwa ufanisi,” alisema. MTWARA Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara, Maria Nzuki amewataka wenzake, kuyaenzi na kuyaendeleza yale mazuri aliyokuwa akiyafanya Barlow enzi za uhai wake.
TANGA
Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Constantine Massawe, ameeleza kusitikitishwa na mauaji ya Barlow na kuwataka watumishi wa jeshi hilo kuwa wavumilivu wakati wakisubiri uchunguzi wa tukio hilo ukiendelea ili hatua madhubuti ziweze kuchukuliwa.
“Kwa sababu kuna kikosi maalum ambacho kimeenda kufanya uchunguzi wa mauaji hayo basi nawasihi wenzangu tuendelee kuwa wavumilivu mpaka hapo upelelezi utakapokamilika na kujua hatma yake au hatua gani za kuchukua, “alisema. Alimwelezea marehemu alikuwa mtu mchapa kazi, mvumilivu na aliyeipenda kazi yake na kwamba ameacha pengo kubwa katika nafasi hiyo.
KILIMANJARO Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro Robert Boaz, amesema kifo cha Barlow ni cha kawaida ambacho kinaweza kumkuta mtu yeyote na haipaswi kujiuliza maswali mengi. Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu, Boaz alisema kifo hicho kinaweza kikamkuta hata rais wa nchi yoyote ambaye analindwa na walinzi chungu nzima.
“Kifo chake kinatupa majonzi sisi makamanda wenzake,lakini kikubwa kilichobaki ni kumuombea kwa Mungu na kuacha uchunguzi kufanyika,” alisema. Aliongeza, “kwa sasa ni mapema mno kuzungumza chochote,lakini ninachoweza kusema ni kuwa kifo chake kimenistua na ni kifo ambacho kinaweza kikamtokea mtu yeyote.”
Aidha kwa upande wao baadhi ya wananchi mkoani Kilimanjaro wameeleza kushangazwa na kiongozi mkubwa wa Polisi kuuawa na majambazi. Bariki Sanga mkazi wa Kilimanjaro aliliambia NIPASHE Jumapili kuwa,ni jambo la kujifunza kwa kila kiongozi na kila raia kuwa mlinzi wa mali zake mwenyewe.
MBEYA 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Diwani Athuman, amesema amepokea kwa mshtuko na masikitiko kifo hicho. Alisema ingawa hapaswi kulitolea tamko kwa kuwa linashugulikiwa na Polisi Makao Makuu, kifo hicho ni changamoto kubwa kwa jeshi hilo ambalo sasa linatakiwa kujipanga na kufanya kazi kwa bidii. Alisema kuwa yeye binafsi anamfahamu vizuri Barlow kwa kuwa alimpokea vizuri wakati yeye (Diwani) alipoteuliwa kwa mara ya kwanza kuwa Kamanda wa Polisi wa mkoani Shinyanga.
Alisema Barlow pia alikuwa ni mwenyekiti wa Makamanda wa Polisi wa Kanda ya Ziwa ambaye alikuwa akiwaunganisha vizuri na kupunguza kabisa matukio ya uhalifu kwenye kanda hiyo. Aliongeza kuwa kwa vyovyote ambavyo uchunguzi utakavyobaini, kifo cha Barlow ni pigo kwa Polisi, kwa kuwa mchano wake ulikuwa bado unahitajika sana ndani ya jeshi hilo.
DODOMA 
Kamanda wa Polisi Mkoani Dodoma, Stephen Zelothe, ambaye Barlow alikuwa mwanafunzi wake kikazi, alisema ni masikitiko makubwa kutokea kwa tukio hilo. “Ni masikitiko makubwa kutokea kwa jambo hili…siwezi kusema lolote tuache kwanza mambo ya kidunia (mazishi) yapite,”alisema Zelothe kwa masikitiko makubwa alipoulizwa nini kifanyike 

*Taarifa hii imeandaliwa na George Ramadhani, Mwanza, Romana Mallya, Dar es Salaam, Sharon Sauwa, Dodoma, Lulu George, Tanga, Charles Lyimo, Moshi na Emmanuel Lengwa,
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

3 comments:

  1. Jamani Watanzania kwa nini kwetu uwazi hakuna? Kikao cha arusi mpaka saa 7 usiku? Hicho kikao sina imani kama kilikuwa cha arusi ya ndugu wa marehemu Kamanda kweli! Maana wangemsindikiza huyo "binti" na mkewe! Au mkewe hakuhudhuria kikao? Mimi inanisikitisha kwa kuwa hata kitu kilichowazi watanzania tunaunda tume ya uchunguzi. hakuna bindadamu asiyekuwa na mapungufu! Twambieni tu, jambazi hawezi kwenda kumuibia polisi kwa maana polisi hawana hela nyingi hivyo!

    ReplyDelete
  2. ... “Wito wangu kwa wananchi walaani vitendo vya mauaji ya viongozi kwa sababu kumpoteza kiongozi ni gharama kubwa katika nchi hasa ukiangalia muda uliotumika kumuandaa hadi amefikia hatua hii,” ...
    Wito kama huu wa Kamanda Kenyela wa Kinondoni hauna maana sana. Kwangu binafsi unaeleweka kama vile kuna baadhi ya binadamu wana "haki" ya kuuawa kwa kigezo cha gharama ya kuwaandaa. Ninachokijua mimi ni kwamba hakuna mwanadamu mwenye haki ya kuuondoa uhai wa binadamu mwenzake. Sasa kauli kama hii, kutoka ka kiongozi inanipa picha mbaya sana ya jamii... hadi kufikiria kwamba polisi wanapoua raia wanakuwa na vigezo vya "gharama" ...

    ReplyDelete
  3. Nakubalia na maoni yako kwa kweli kama taifa bado tunakosa elimu ya uraia na elimu ya uongozi bora kwa viongozi wetu; Hakuna mwanadamu mwenye haki ya kuua binadamu mwenzake; Katika siku za karibuni Taifa letu limegumwikwa na tatizo la mauaji ya mara kwa mara ambayo yameigharibu taifa haki ya msingi ya binadamu mwenzake kuishi. tunaiomba serikali yetu kukemea na kuwa mstari wa mbele katika kupinga na kusimamia sheri za kuzuia mauaji dhidi ya binadamu mwingine.

    ReplyDelete