WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, October 26, 2012

Machafuko Tanzania: NAMJOF yalaani; Hay-atul Ulamaa yatoa tamko



Tamko hilo la kurasa saba likisomwa mbele ya waandishi wa habari Oktoba 25, 2012. (picha na via K-VIS blog)

Pamoja na mambo mengine, katika tamko hilo lenye kurasa 7, wameutaka umma wa Kiislamu, kusherehekea kwa amani Sikukuu ya Idul al Adh-haa, inayoanza Ijumaa Oktoba 26, 2012, wakiwatahadharisha waumini wa Kiislamu, wasipandwe na munkar wakati wa mawaidha yatakayotolewaq na viongozi mbalimbali wakati wa maadhimisho hayo.

Pia wametoa angalizo kwa Waumini wa dini nyingine kujenga tabia ya kuheshimiana na kuheshimu imani za dini nyingine, kwa mustakbala wa kujenga jamii yenye umoja. 


Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanazuoni (Wasomi) wa Kiislamu Tanzania, (HAY-ATUL-ULAMAA), Sheikh Mohammed Issa Hemed, (Kulia), akifafanua jambo wakati umoja huo ulipotoa tamko kuhusu kadhia ya kuvunjiwa heshima Qur'an na vurugu zilizofuatia kwenye hoteli ya Tansoma, Dar es Salaam Alhamisi Oktoba 25, 2012. Katikati ni Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Sheikh Suleiman Kilemile, na kushoto ni Makamu wake, Sheikh Abdallah Bawazir. Wengine ni wajumbe wa umoja huo. (picha via K-VIS blog)


NAMJOF YALAANI VURUGU ZENYE SURA YA KIDINI
JUKWAA la Kitaifa la Waandishi wa Habari wa Kiislamu (NAMJOF) limelaani vikali tabia za vurugu za kidini zinazoendeshwa na baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu hapa nchini.

Aidha, NAMJOF imeitaka jamii ya Kiislamu kuishi kwa kutumia falsafa ya dini hiyo kama ilivyoshushwa na Mwenyezi Mungu kupitia kwa mtume wake Muhammad (SAW) ya kuvumiliana, kuwa na subira na upendo baina yao na wasiokuwa Waislamu.

Akitoa tamko hilo la kulaani vurugu hizo, Mratibu wa NAMJOF hapa nchini, Hemed Kimwanga amesema mjini Dar es Salaam leo kuwa waumini wa dini ya Kiislamu wanatakiwa kujua ni wapi walipojikwaa badala ya kuangalia pale walipoangukia.

Amesema mahitaji ya Waislamu siyo vurugu bali  ni elimu, afya, shufaa, zakkah na upendo ili kupiga mbele hatua yao wenyewe, ya dini yao na nchi yao kwa jumla.

“Kufanya vurugu eti kwa kusema ni jihad si sahihi bali ni ujahili sawa na ule uliokuwa ukifanywa na wapinzani wa mwanzo wa Uislamu enzi za Mtume”, amesema Kimwanga katika taarifa ya NAMJOF iliyopatikana jijini Dar es Salaam.

“Wanaofanya hivyo wanakiuka maagizo na mafundisho ya Mtume wetu Muhammad (SAW) ya kutaka kuieneza na kuilingania dini ya Allah (SW) kwa hekima na busara”, amesisistiza.

Amesema iwapo Mtume angehubiri dini ya Mwenyezi Mungu kwa staili hii ya sasa ya mapambanao dhidi ya watawala na wasiokuwa Waislamu, kamwe asingefanikiwa, “Kwa sababu ulinganiaji huo wa hao wanaojidai wanalingania Uislamu hauzingatii busara wala hekima”, imesema taarifa hiyo.

Kimwanga amefafanua kuwa hekima haipatikani sharti kwa kusoma au kuwa na elimu ya kutosha na pia busara haipatikani sharti kwa mtu kuwa na umri mkubwa au kuitembea dunia kwa dhana na dhima kubwa isiyokoma.

Amesisitiza kuwa huu ni wakati wa Waislamu wenye uwezo kutoa zakkah ili kuwapatia vijana wao wasiojiweza elimu na/au mitaji kwa ajili ya kujiendeleza ili waondokane na magenge ya kihuni na yale yaliyokata tamaa ya maisha.

“Uislamu ukiwa ndiyo dira elekezi kwa maisha ya mwanadamu, hauna budi kufuatwa kwa vitendo na siyo kwa blablaa au vurugu”, anasisistiza Kimwanga kwenye taarifa hiyo ya NAMJOF na kuongeza:  “Kwa kuanza na tuanze na matajiri kutoa zakkah kama ilivyokadiriwa na Allah (SW) ili itumike kusaidia vijana wetu na watu wengine wasiojiweza kujikwamua kimaisha”.

Ameeleza kuwa falsafa ya maswahaba watano wa mwanzo nyakati za Mtume Muhammad (SAW) ni jawabu pekee la kuusukuma mbele Uislamu na Waislamu si Tanzania tu bali dunia nzima.

Kimwanga amesema endapo waumini wa dini ya Kiislamu  wangeielewa falsafa hiyo ya Mwenyezi Mungu katika kuwaleta maswahaba hao watano, hapana shaka vurugu zinazoendeshwa  dunia nzima na makundi ya Waislamu zisingekuwepo na badala yake amani, upendo, maendeleo na mshikamano vingetawala kwa ustawi wa dunia na walimwengu wote.

Amesema maswahaba hao wanawakilisha wizara tano maalum za kustawisha Uislamu na waumini wake na endapo waumini hao wangeelewa hivyo, dunia hii ingekuwa pepo kwa wakaaji wake. Amesema Swahaba Abubakar Sidiq anawakilisha Wizara ya Fedha kwa kuwa alikuwa tajiri wa kupindukia wa Makkah enzi za Mtume.

“Naye Omar Ibni Khattab anawakilisha Wizara ya Ulinzi kwa vile alikuwa mtu shababi mwenye nguvu nyingi”, anayakinisha Kimwanga na kusisitiza kuwa Swahaba Omar Ibni Khalfan anawakilisha Wizara ya Elimu kwa vile alikuwa msomi wa kutosha.

Amesema kuwa Swahaba Ally Ibni Abuu Taalib anawakilisha Wizara ya Vijana kwa vile alikuwa kijana.

“Vijana ndiyo wanaotegemewa kulelewa vyema ili waje washike nafasi za wazee wao watakapokuwa hawapo au wamestaafu uongozi”, amesisitiza Mratibu huyo wa NAMJOF.

Amesema swahaba Bilal ambaye alikuwa mtumwa kutoka Ethiopia wakati ikiitwa Abysinia ndani ya Bara la Afrika anawakilisha Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ambayo itaendeshwa kwa umahiri zaidi pale matajiri wa Kiislamu watakapotimiza maagizo ya Allah (SW) ya kuhusu Zakkah. Pamoja na yote hayo, NAMJOF imeitaka serikali kuwa macho na wachochezi wa vurugu hizo kwa kuzingatia kuwa wanafahamika hasa baada ya mbinu zao kugonga mwamba za kumng’oa Mufti wa Tanzania, Sheikh Issa bin Shaaban Simba kinyume cha sheria.

“Hawa watu lazima wana wafadhili wa ndani na nje ya nchi”, taarifa hiyo imesema na kuongeza kuwa kinyume chake suala la muungano ni kama sababu tu au ‘danganya toto’. “Muungano na dini ni wapi na wapi?”, ameuliza Kimwanga kwenye taarifa hiyo na kuongeza: “Hizo ni chokochoko zenye lengo la kuitenga Zanzibar na wazalendo ndugu zao wa damu wa Tanzania Bara” “Imefika mahala watawala na Watanzania kwa jumla wajue kuwa wafuasi wa Sultan Jamsheed kwa kusaidiwa na dola moja kubwa la Ulaya (jina tunalo) wanataka kuirejesha Zanzibar kwenye tabaka za rangi na utumwa kama ilivyokuwa kabla ya Aprili 12 mwaka 1964 wakati mapinduzi ya kumkomboa Mzanzibari yalipofanyika na Jasheed kuimbia Zanzibar”, inasema taarifa hiyo.

Historia inaonesha kuwa Uingereza ilitoa uhuru wa bandia kwa Sultan Jamsheed wa Zanzibar Desemba 10 mwaka 1963 kama ilivyofanya Afrika Kusini kwa makaburu Januari mwaka 1960 na kupanga na makaburu hao kuinyakua Namibia mwaka 1962.

Baadaye Uingereza ilikula njama na Ian Smith wa Rhodesia aliyejitangazia uhaini dhidi ya dola hiyo na hivyo kuitawala chi hiyo kwa mabavu na ubaguzi wa rangi hadi Oktoba 25 mwaka 1965 aliposalimu amri kufuatia kushindwa kuhimili mapambano makali yaliyoanzishwa na wazalendo.

Haini Smith aliachia madaraka Machi 25, mwaka 1985 na kumkabidhi Rais Robert Gabriel Mugabe akiwa wakati huo Waziri Mkuu wa kwanza wa Kiafrika wa Taifa hilo lililobadilishwa jina na kuwa Zimbabwe.


Source: http://www.wavuti.com

No comments:

Post a Comment