WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Monday, October 22, 2012

Masheikh, wamruka Ponda




  *SMZ yatishia kufuta Jumuiya ya Uamsho

Taasisi  ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiisilamu Tanzania imesema mhemko na ghadhabu zilizoonyeshwa na kikundi cha Waislamu na kutoa mwanya wa kutendeka uhalifu wa kuchomwa makanisa eneo la Mbagala, jijini Dar es Salaam siyo mafundisho ya Mwenyezi Mungu.

Kadhalika, Taasisi hiyo imesema kwa sasa ikipata fursa ya kukutana na Katibu Mkuu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam Tanzania,  Sheikh Ponda Issa Ponda, itamshauri azingatie mafundisho ya Uislam katika kufanya mambo yake.

Tamko hilo lilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Taasisi hiyo, Sheikh  Khamisi Mataka, alipozungumza na waandishi wa habari.



Sheikh Mataka alisema kitendo cha kikundi cha watu kukataa kutii mamlaka za serikali zilizopo ni sawa na kupinga amri za Mwenyezi Mungu kwa mujibu wa Kitabu kitakatifu Qur’aan.

Tukio la kuchomwa makanisa lilitokea Oktoba 12, mwaka huu katika eneo la Mbagala baada ya kijana mmoja kukojolea Qu’raan tukufu hatua ambayo ilidaiwa kuamsha hasira.

Aidha, Taasisi hiyo imelipongeza Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya usalama kwa kufanikiwa kutuliza ghasia zote kuanzia zile za kuchoma makanisa, zilizotokea Ijumaa iliyopita katika eneo la Kariakoo na Zanzibar bila ya kugharimu roho yoyote ya Mtanzania.

Sheikh Mataka aliwataka Waislamu kurejea mafunzo ya Mwenyezi Mungu yanayohimiza kumfanyia uadilifu hata adui yake (Qu’raan Surat Al-Maida (5) Aya ya 8  na kwamba kuvunja sheria za nchi kusiwe mtaji wa kudai haki.

Alisema vikundi vinavyoleta vurugu Tanzania Bara na Zanzibar havijui mafundisho ya Mwenyezi Mungu kwa kuwa vinataka haki ya kuhukumu.

Taasisi hiyo inatarajia kuitisha kikao cha Masheikh na viongozi wa taasisi mbalimbali za Kiislam ili kutafuta dawa ya kumaliza vurugu za kidini zinazoibuka mara kwa mara.

Sheikh Mataka alisema baada ya kufanyika kikao hicho, taasisi yake itawakutanisha viongozi mbalimbali wa dini ya Kiislam na Kikristo ili kujadili njia bora ya kudumisha amani, utulivu na uhusiano mwema kwa wananchi wote nchini.

Aliwaonya wanasiasa kutoingilia na kuanza kushawishi vikundi vya kidini kufanya vurugu na kukataa kutii mamlaka halali zilizopo kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

SMZ YATISHIA KUIFUTA UAMSHO


Serikali ya Zanzibar kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud, imse haitasita kuifutia usajili Uamsho ikiwa itashindwa kufuata utaratibu na matakwa ya kikatiba ya kuanzishwa kwake.

Aidha, Waziri Aboud alisema ikiwa wafuasi wa jumuiya hiyo wakianzisha tena vurugu, Serikali itachukua hatua ya kuifuta Uamsho, kwa vile tayari ilishaandikiwa barua ya kuonywa, kutokana na vitendo vya vurugu.

“Vitendo vya vurugu vinavyofanywa na Uamsho vinazidisha umaskini wa wananchi, kutokana na kuvuruga njia za kiuchumi, na kuwaathiri wajasiriamali, wafanyabiashara na hata mama lishe,” alisema Waziri Aboud na kuongeza:

“Hizi vurugu hazikuwepo kabla ya Uamsho, tulikuwa tukiishi vizuri, tangu kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa miaka miwili iliyopita, hata dunia ilikuwa ikitupongeza kutokana na maelewano yetu,” alisema Waziri Aboud.

Hata hivyo, alisema serikali ina mpango wa kufanya tathmini ya hasara iliyopatikana ili wananchi wapate kufahamu madhara ya vurugu, kiuchumi na uharibifu wa mali.

'KIONGOZI WA UAMSHO HAKUTEKWA' 

Jeshi la Polisi Zanzibar limesema baada ya kuwahoji viongozi wa Jumuiya ya Uamsho, kwa zaidi ya saa kumi, limebaini kuwa Sheikh Farid Hadi Ahmed hakutekwa na vyombo vya ulinzi na usalama, bali ni mchezo wa kuigiza.

Kamishna wa Polisi Zanzibar, Mussa Ali Mussa, amesema viongozi hao akiwemo Farid walianza kuhojiwa juzi kuhusiana na madai yao na kugundua kwamba kiongozi huyo alikuwa katika maficho ya kawaida na kusababisha vurugu visiwani.

“Maelezo ya Farid na dereva wake, Said yanatofautiana, kwanza alisema alitekwa na kupakiwa katika gari aina ya Noah, alipohojiwa na Polisi alisema alipakiwa katika gari aina ya Escudo, suala hili ni uongo ulio wazi,” aliongeza.

“Kajiteka mwenyewe, wala hakutekwa, sisi tulishawahi kumkamata Farid na kumfikisha mahakamani, tukimhitaji tunamkamata, na hatumfichi mtu, iweje adai kakamatwa na Polisi na Usalama, kwa nini tufiche kama tulimkamata?” alihoji Sheikh Farid.

Alisema Jeshi la polisi limeamua kuwakamata viongozi wa Uamsho kutokana na makosa waliyofanya ya kusababisha fujo, uharibifu wa mali, na kifo cha askari Said Abdulrahman aliyeuawa kwa kupigwa mapanga huko Bububu.

“Wako wengi tunawatafuta, hata wanaochangia kwa njia yeyote ile iwe kwa fedha, na wewe pia unachangia maovu na kuhusika na uhalifu, na hii kamatakamata, inaendelea, wote waliohusika na vitendo hivyo tutawakamata kwa vile tuna ushahidi wa picha za wote waliokuwa katika vurugu,” alisema Kamishna Mussa.

Aidha, alisema viongozi hao watafikishwa mahakamani leo, kujibu mashtaka mbalimbali.

“Tutapambana na Uamsho, iwe mwezi mmoja au mwaka mzima, lengo letu ni kuhakikisha amani na utulivu inatawala, na ikibidi tutatumia risasi za moto wakati ukifika,” alisema Kamishna Mussa.

Aliwataja viongozi wa Uamsho waliokamatwa ni pamoja na Amir Farid Hadi Ahmed, Amir Azzan Khalid Hamdan, Amir Mselem Ali Mselem, Mussa Juma Issa, Suleiman Majisu, Haji Sadifa ambaye ni Mkuu wa Usalama wa Uamsho na mwingine aliyemtaja kwa jina moja la Hassan na wengine wawili.

Alisema viongozi hao wanatuhumiwa kutoa taarifa za uongo kwamba kuna kaburi lilionekana eneo la Bumbwini, ambalo linahofiwa kufukiwa kwa mwili wa Farid, jambo ambalo lilidhihirika kuwa si kweli baada ya Polisi na viongozi hao kwenda kulifukua na kutokuta mwili wa mtu yeyote.

WANAODAIWA KUUA  ASKARI WAPELEKWA Z’BAR


Aidha, alisema watu watatu wanaotuhumiwa kumuua kwa mapanga askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) mkoa wa Mjini Magharibi Zanzibar wamepelekwa Zanzibar kutokaTanga walikokuwa wametorokea baada ya tukio hilo.

Alisema watu hao wataunganishwa na wenzao watatu waliokamatwa Jeshi hilo katika maeneo tofauti ya Mji wa Zanzibar baada ya kumuua askari huyo katika mtaa wa Bububu wakati akitoka kazini usiku wa kuamkia Oktoba 17, mwaka huu.

Alisema tangu kutokea vurugu hizo, watu 65 wamekamatwa wakiwamo watuhumiwa hao na kuwa Jeshi la Polisi linaendelea kuwasaka watu wanaofanya vitendo vya kuchochea vurugu.

MCHUNGAJI: WANAOCHOMA MAKANISA WAOMBEWE

Mchungaji wa Makanisa ya Youth International Association, Orkey.

Mgonja, amesema ikiwa uchomaji wa makanisa utaendelea kufanywa na watu wanaojificha katika mgongo wa dini za watu, watalazimika kutoa tamko kali, pamoja na kumwomba Mungu awashughulikie wahusika.

Aliyasema jana wakati alipokuwa akiwatunuku vyeti wanachuo cha Sinoni 112, waliohitimu kozi ya ualimu, hoteli, kuongoza watalii, biashara na ushauri nasaha wa ugonjwa wa Ukimwi.

Alisema matukio ya uchomaji makanisa ni uvunjifu wa amani ambao haujazoeleka kuonekana nchini.

“Muasisi wa Taifa hili, Julius Nyerere, alipokuwa akitafuta Uhuru wa Taifa hili, alienda Umoja wa Mataifa na alisema endapo atashindwa, basi atapiga goti kumwomba Mungu atupatie Uhuru kwa njia ya amani na tulipata Uhuru bila umwagaji damu, hivyo yatupasa kila mmoja kulinda amani tuliyonayo,” alisema Mchungaji huyo.

Alisema inasikitisha kuona baadhi ya watu wanaojificha kwenye dini za watu wengine, wanashindwa kumwogopa hata Rais wa nchi na viongozi wengine na kuwataka watu hao kufikiria na kufahamu kuwa kuna Mungu ambaye ni zaidi ya vitu vyote.

Aidha, alisema haya yanatokea kutokana na vijana wengi kukosa kazi za kufanya.

‘JIEPUSHENI NA MIGOGORO’

Waumini wa madhehebu mbalimbali ya kidini nchini wametahadharishwa  kuepukana na migogoro inayoashiria uvunjifu wa amani na kutaka kila mmoja kwa imani yake kuendesha maombi maalumu ya  kuliombea Taifa utulivu.

Aidha, viongozi wa dini wametakiwa kuwa makini na matumizi ya nafasi zao.

Wito huo umetolewa na Mchungaji Nestory Ngwega, wakati akizungumza na washiriki wa mafunzo ya siku tatu ya unyanyasaji yaliyowashirikisha watu wa kada mbalimbali mjini Muheza, mkoani Tanga.

Alisema kazi ya kiongozi wa dini ni kuwa chachu ya watu kumtafuta Mungu, kudumisha amani na kuwataka wafuasi wa madhehebu ya dini waachane na udini.

“Dhambi kubwa katika kipindi hiki ni ile ya udini na udhehebu, jambo hili si agizo la Mungu, tuachane nao kabisa ili kuokoa dunia na watu wa dunia hii,” alisema Mchungaji Ngwega.

KANISA LALAANI MACHAFUKO


Kanisa la Wasabato Conference la mkoani  Mara, limelaani  vikali machafuko yanayoendela kutokea nchini na kuwataka wananchi kuheshimu sheria bila shuruti na  viongozi walioko madarakani kwani wapo kwa mamlaka ya Mwenyezi Mungu.

Askofu wa kanisa hilo, David Makoye alitoa kauli hiyo mjini Bunda  wakati akifunga kambi ya siku 21 kuhusu afya ya jamii kwa kaya na familia, kuishi kwa amani, injili ya neno la Mungu na wananchi kufundishwa ujasiriamali.

 Akofu Makoye alisema kuwa haipendezi watu kufanya machafuko ya aina yoyote kwa kisingizi cha udini, yakiwemo ya kuchoma nyumba za ibada na kwamba ni vema wanaofanya vitendo hivyo wakabadilika na kufuata maagizo ya Mwenyezi Mungu.

Askofu aliwaomba watu wote wayaheshimu madhehebu yao ambayo kimsingi yanasistiza kwamba watawala wote wanatokana na mamlaka ya mwenyezi Mungu, hivyo wanapaswa kuheshimiwa.

“Heshimu madhebu yenu pia heshimu viongozi walioko madarakani hata biblia imeandika watawala wanatokana na mapenzi ya Mungu,” alisema.

Askofu Makoye aliwaomba wananchi pia waache tabia ya kubeba silaha yakiwemo mabomu, mawe na silaha za jadi kwa ajili ya kufanya vurugu na uhalifu wa aina yoyote na kuonya kuwa iwapo amani ikivunjika nchini watakaoathirika ni watu wote bila kujali wametokea katika dhehebu au kabila gani.

APPT YABAINISHA SABABU ZA VURUGU

Chama cha APPT Maendeleo kimesema matukio ya vurugu na maandamano yanayoendelea nchini na kusababisha uvunjifu wa amani ni matokeo ya mfumo wa kibepari ambao umewagawa Watanzania kati ya walionacho na wasionacho ambao umeruhusu siasa kuingia katika dini.

Kimesema pia sualala upatikanaji wa haki limechangia watu kuwa na mfadhaiko ambapo watu wanawekwa rumande kwa makosa ambayo hawajayatenda na pia yapo matatizo mengi ya ardhi lakini haki haitendeki kwa wanyonge.

Mwenyekiti wa Chama hicho, Peter Mziray, alisema mfumo wa kibepari  umewafanya wananchi wasiokuwa nacho kujenga hasira dhidi ya walionacho na hivyo kunapotokea vurugu kundi hilo linatumia fursa hiyo kujinufaisha.

 Mziray alisema katika historia ya nchi watu hawajawahi kuandamana kwenda Ikulu, lakini kutokana na hali ngumu ya maisha wananchi wamejenga imani kuwa walionacho wote wanatoka chama tawala ndiyo maana wanatafuta sehemu ya kupumulia.

 “Hivi sasa hakuna ajira maisha magumu, na ndiyo maana watu wanalazimika kujazana kwenye misikiti makanisani watafute pa kupumulia,” alisema Mziray.

Alisema mfano suala la kukojolea Qur’aan halikuwa jambo la kukuzwa  kiasi hicho kwa sababu lilikuwa tayari linashughulikiwa kisheria, lakini wananchi waliamua kulipuka sababu  ya kuchoka na hali ya kibepari inayoendelea nchini.

Mziray alisema ili kukabiliana na tatizo hilo, kunahitajika mwafaka wa kitaifa utakaoshirikisha wadau muhimu vikiwamo vyama vya siasa na madhehebu ya dini  ili kuweka mkakati wa pamoja ambao utaingizwa kwenye katiba mpya.

“Lazima kuwe na mwafaka ambao chama chochote cha siasa kitakachoshika hatamu za uongozi, raslimali zote za nchi zitumike kwa manufaa ya wananchi wote tofauti na sasa. Ukitaka kunufaika lazima uwe CCM,” alisema Mziray.

Imeandikwa na Richard Makore, Thobias Mwanakatwe, Dar; Mwinyi Sadallah, Zanzibar, Dege Masoli, Muheza, Cynthia Mwilolezi, Arusha na Ahmed Makongo, Bunda.

CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment