WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Wednesday, May 22, 2013

UONGOZI BORA MAANA YAKE NINI?




Picture
  •  MPE KAISARI YALIO YA KAISARI NA MPE MUNGU YALIYO YA MUNGU;


  • CHUKUA CHAKO MAPEMA KABLA HUJEFUKUZWA


  • TIMIZA WAJIBU WAKO

Dhana ya uongozi wa namna yeyote ile; unafaa uanzie nyumbani kwa kila mtu  uongozi ni uwezo wa kuweza kuyakabili kwanza maisha yako binafsi; uwezo wa kuyatawala maisha yako kulingana utaratibu ambao wewe mwenyewe umejiwekea kuanzia ndani ya familia yako;  ukifanikiwa hili unakuwa umefaulu katika mtihani huu wa kwanza wa uongozi ndipo jamii inapoanza kukuona kuwa hata ukawaongoza wao pia.
 
Kwa maneno mengine ni uwezo au njia ya kuweza kuwashawishi watu ili waweze kufanya kitu au kufikia lengo fulani la kikundi kwa ridhaa yao wenyewe. ili uongozi uwe bora ni lazima kuwe na kiongozi anayeongoza kundi fulani la watu au jamii husika.

Katika kila jamii kuna umuhimu wa kuwa na kiongozi kunatokana na ukweli kwamba watu wanapaswa kuwa na namna ya kuunganisha nguvu zao ili kufikia malengo yao. Katika  kila jamii, ni lazima kuwepo na mikakati ya kuunganisha nguvu, vipaji, uwezo na stadi mbalimbali za wana jamii. Wajibu wa msingi wa kiongozi yoyote ni kusaidia kuunganisha uwezo wa watu, kuratibu, kusimamia shughuli za watu, na kila inapobidi aonyeshe njia itakayosaidia kufikia lengo.

 

Kwa dhana ya Plato uongozi ni dhana  au taaluma inayompa muhusika madaraka na uwezo wa kuwawezesha wale wanaoongozwa kuunganisha nguvu, stadi na vipaji vyao na kuvitumia ili kufikia malengo yao. Kuongoza ni kujua lengo la wale wanaoongozwa na njia ya kufikia lengo lao.


Uongozi bora una mchango mkubwa sana katika uimara wa jamii. Lakini tufahamu kuwa Ubora wa kiongozi unachangiwa na vitu vingi lakini tusidahau kuwa vile vile uongoziau kiongozi bora hutoka kwa Mungu.

 

(i)     Ufahamu

Kiongozi ni lazima awe na ufahamu mkubwa juu ya taasisi anayoiongoza, malengo yake, mazingira, na matatizo. Vilevile anapaswa kuwafahamu wale anaowaongoza (vipaji vyao, changamoto,n.k).

 

Ubunifu

Kila taasisi inalenga kufikia lengo fulani. Ni wajibu wa kiongozi kuwaongoza wana taasisi ili wafikie malengo yao. Kwa hiyo, kiongozi ni lazima aweze kubuni mikakati na mbinu zitakazoiwezesha taasisi anayoingoza kufikia malengo yake.

 

Maadili

Kiongozi ni lazima akubalike katika jamii na taasisi anayoiongoza. Ili akubalike hana budi kuzingatia maadili ya msingi ya jamii na taasisi yake. Kiongozi mwongo, mlevi, mvivu, asiye mwaminifu n.k hawezi kuitwa kiongozi bora.

 

Mfano bora kwa wengine

Kiongozi bora ni yule anayewajibika na kuwa mfano bora kwa wengine. Kiongozi anapaswa kuwa mstari wa mbele ktk kutimiza wajibu badala ya kujali maslahi yake binafsi uongoza kwa mofano.

 MBINU ZA KUONGOZA

Ili kiongozi aweze kuunganisha wale anaowaongoza ni lazima azingatie misingi ifuatayo:-

(i)     Ajifahamu mwenyewe.

(ii)   Afahamu itikadi, uwezo, mwelekeo na malengo ya wale anawaongoza.

(iii) Ayajue mazingira ya uongozi wake.


Akizungumzia dhana ya uongozi, Mwalimu Nyerere alisema, “uongozi ni kuonyesha njia.” Kwa maana hiyo, viongozi shurti wafahamu vema matokeo ya uongozi wao. Wasome imani za wanaowaongoza na nyakati zilizopo ili kutambua matumaini ya umma kimaisha.

TATIZO LETU LA UONGOZI TUNALIONAJE LEO HII?

Je ni kweli kuwa nchi yetu Tanzania  imekosa viongozi makini, wabunifu, waaminifu, waadilifu na wazalendo wa kweli. Au hizi ni propaganda za siasa tu za kuchafuana? Au taifa letu leo limekosa viongozi wanaojali kuwa watu wana haki ya kupata chakula bora, mavazi bora, malazi bora – maisha bora kwa jumla? La msingi hapa ni kuwa kiongozi yeyote anayekuwa tayari kuongoza na anapochaguliwa  kuongoza popote, ajuwe anabeba jukumu la kubadilisha hali za watu kuwa nzuri. Atumie stadi za uongozi mwema kuonyesha njia.
 
Tabia ya viongozi kuongoza kwa kufikiria zaidi maslahi binafsi mwiko. Walitumia stadi za uongozi kusimamia haki za waliowaongoza; wanyonge na hata waliokuwa na uwezo. Wajikumbushe kuwa kupewa uongozi ni kuchukua ahadi ya kutenda kwa haki.

Lakini wanaoifanya kazi ya siasa kwa kuigeuza ni pango la wizi, rushwa, uonevu, unyonyaji na hata kuua raia, wajiandae kupokea adhabu ya muumba. Yeye anaona kila tendo linalotendwa na viumbe wake wakati wote. Wanasisitiza viongozi lazima wawe waadilifu na umma uwe na uwezo wa kuwajibisha viongozi wao wanapotenda kinyume na taratibu na sheria zilizowekwa.

Mwalimu Nyerere aliandika miongozo mizuri katika Azimio la Arusha akisema kwamba ili tuendelee tunahitaji mambo matatu: Watu, Ardhi, Siasa Safi na Uongozi Bora. Alitambua mchango wa mambo hayo katika maendeleo ya mwanadamu.

Kupitia siasa safi kila kitu cha kunufaisha wananchi hupatikana. Bali ni muhimu viongozi wanaotarajiwa kufanikisha ustawi wa wanadamu, wapatikane kwa njia ya haki. Watokane na ridhaa ya watu wenyewe wanaotaka kuongozwa.

Hata kwenye vyama vya siasa au vikundi vingine vya kiraia, viongozi lazima wapatikane kwa njia ya haki siyo vurugu na upindishaji wa sheria na taratibu.

Mungu huwaweka viongozi

viongozi wanajua kuwa hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu. Zaidi ya yote Mungu anaangalia sana nani ataongoza watu wake wateule. Viongozi wa taifa walipoongoza kufuatana na mapenzi ya Mungu nchi yote ilisitawi na kubarikiwa kwa njia nyingi. Walipomsahau Mungu shida na dhiki zilianza.
 Kama Mungu ndiye anayewapa viongozi mamlaka ina maana ya kwamba kila kiongozi atajibu mbele za Mungu jinsi alivyoongoza. Kiongozi anayefahamu kwamba atatoa hesabu kwa Mungu anahakikisha kwamba mwenendo wake unapatana na Neno la Mungu. Mamlaka yote yametoka kwa Mungu. 

Tukumbuke, utumiaji wa nguvu, utumiajia wa matusi katika uongozi sio dhana ya uongozi bora inapingana na maadili ya kibinadamu na ya maadili ya kimungu pia.  

1 comment:

  1. nimeipenda habari hii je tunavyoelekea katika upatikanaji wa katiba mpya na uchaguzi wa mwaka 2015 je tuna imani kuwa tutaweza kupata viongozi bora? au tutapata tu bora viongozi ambao pengine sasa hivi wanahangaika kuyapenyeza mawazo yao katika mchakato wa katiba mpya ili waweze kupata unafuu wa kuchaguliwa kuwa viongozi. Mwenyezi Mungu tujalie hekima ili tuweze kuwapata viongozi ambao ni zao la hekima yako ili waweze kuwaongoza watu wako kwa uwajibikaji mkubwa.

    ReplyDelete