WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Wednesday, May 1, 2013

Dkt Kigwangallah (Mb) atuhumiwa kufuja misamaha ya kodi

 
Picture
Screen-shot kutoka kwenye ukurasa wa Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Kaskazini
Habari iliyonukuliwa hapo chini kutoka kwenye gazeti la Tanzania Daima imeandikwa na Josephat Isango. Dkt Hamisi Kigwangallah anapatikana Twitter kwa @hkigwangalla

MBUNGE wa Nzega, Dk. Hamisi Kigwangalla (CCM), anadaiwa kuliibia taifa kwa kutumia vibaya misamaha ya kodi ya mamilioni ya shilingi kwa ajili ya ujenzi wa chuo cha afya eneo la Uchama, wilaya ya Nzega.

Kwa mujibu wa nyaraka ambazo Tanzania Daima Jumatano imezipata, Dk. Kigwangallah amejipatia misamaha ya kodi ya ongezeko la thamani na ushuru wake kupitia kampuni ya Emergent Africa Limited, anayoimiliki kwa asilimia 78 na Bayoun Kigwangallah ana asilimia 22.

Kupitia kampuni hiyo, mbunge huyo ameingiza nchini bidhaa mbalimbali ambazo badala ya kuzielekeza katika ujenzi, amefungua duka la kuuza vifaa vya ujenzi eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam na nyingine anaziuza kwa wafanyabiashara wengine.

Nyaraka hizo zinaonyesha kuwa kampuni ya Emergent Africa Ltd, ilisajiliwa katika Kituo cha Taifa cha Uwekezaji (TIC) Septemba 27, 2011 na iliruhusiwa kupata misamaha hiyo kuanzia Septemba 2011 hadi Agosti 2014.

Kwa mujibu wa makubaliano kati ya kampuni ya Emergent Afica Ltd na TIC, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) iliombwa kuisamehe kodi kampuni hiyo ya Dk. Kigwangallah vitu mbalimbali vyenye orodha toka namba 1 hadi 390.

Bidhaa hizo kwa uchache ni kompyuta 1042, mashine za kutolea kopi 12, printa 12, ‘binding machines’ 12, vikokotozi (calculator) 640, projekta 12, video kamera 12, feni 30, vifaa vya simu masanduku 28, jenereta moja, magari aina ya Toyota 13, lori 3, Nissan Navarra Pik up 4, Mitsubishi Canter 2 na mabasi madogo manane.

Pamoja na msahama huo, Dk. Kigwangallah kupitia kampuni hiyo, aliingiza nchini vitu bidhaa mbalimbali vikiwemo vigae vya sakafuni 2500 vyenye ukubwa wa 600X600 na 1000 vyenye ukubwa wa 400 X 400 pamoja na vigae vya ukutani.

Katika orodha hiyo viko viti na meza za kulia, hema la bustanini, sofa, kabati za kuwekea nguo, mazulia, vitanda na magodoro, televisheni na vingine.

Aidha nyaraka hizo zinaonyesha baada ya kupokea bidhaa hizo kutoka nchini China, ziliuzwa katika maduka mbalimbali ya Kariakoo na vigae vingine kuuzwa kwa mkuu wa wilaya moja mkoani Tanga (hatukumtaja) kwa kuwa hakupatikana kujitetea.

Hata hivyo, kumeonekana utata katika nyakara hizo kwani kampuni ya Delmas iliyosafirisha kontena la bidhaa hizo kuja kwa Dk. Kigwangallah, ziko tofauti na ankara za malipo.

Ankara hizo zinaonyesha kuwa zilitolewa na makampuni ya Louis Valentino Investment and Development Co. Ltd iliyopo Na. 19 Ji Hua 3 Road Foshan na Sharpeye Furniture.

Wakati manunuzi yakionekana kufanyika China Oktoba mosi, 2012, nyaraka nyingine zinaonyesha kuwa mali zilishaingizwa nchini tangu Aprili 14 mwaka huo, kupitia kampuni ya Innovative Freight yenye TIN 100-145-596, risiti namba 2012/0000002986.

Na nyaraka za mamlaka ya mapato zinaonyesha bidhaa hizo ziliingia nchini Aprili 3 mwaka jana, hali inayoonyesha kupishana katika tarehe za kununua na kuingiza bidhaa hizo.

Pia utata huohuo unaonekana katika taarifa za Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ambazo zinaonyesha bidhaa hizo zilikaguliwa Machi 28, 2012.

Huku kukiwa na orodha zinazotofautiana za makampuni mawili ya kibiashara wakati ankara ya malipo ilikuwa moja.

Taarifa zaidi zinaonyesha kuwa kontena hilo lilipofika nchini lilionekana kuwa na vitu tofauti na vile vilivyoorodheshwa, hivyo kusababisha kontena hilo kufanyiwa uchunguzi usio wa kawaida kwa kupekua mzigo mmoja mmoja.

Dk. Kigwangallah alipotafutwa kwa simu kufafanua tuhuma hizo, alisema amebanwa na kazi. Na alipoambiwa ametumiwa maswali kwenye barua pepe yake, aliahadi kujibu lakini hakufanya hivyo.

Alipopigiwa tena jioni, alisema, “Sema haraka unataka nini?” Alipoulizwa juu ya tuhuma hizo alikata simu.

Lakini baadaye aliandika ujumbe kwa simu: “Nitakupigia jioni nikitoka bungeni.”

Alipoambiwa inaandikwa habari gazetini, alijibu kwa ujumbe mfupi kuwa tuhuma zilikuwa za uongo bila kufafanua.

No comments:

Post a Comment