WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, May 3, 2013

Serikali yachukua uamuzi mgumu, yafuta matokeo



Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, akiwasilisha kauli ya serikali Bungeni Dodoma jana kuhusu taarifa ya awali ya Tume ya Taifa ya kuchunguza matokeo ya mtihani wa taifa wa Kidato cha nne wa mwaka 2012. Picha na Edwin Mjwahuzi 
Dodoma/Dar. Serikali imechukua uamuzi mgumu na kuamua kuwafariji wanafunzi waliofeli mitihani ya kuhitimu kidato cha nne mwaka 2012 baada ya kufuta matokeo hayo na kuamua yaandaliwe upya kwa kutumia utaratibu uliotumika mwaka 2011.
Uamuzi huo wa Serikali umetokana na matokeo mabaya ya mitihani huo yaliyosababisha zaidi ya asilimia 60 ya wanafunzi kupata sifuri.
Kutokana na matokeo hayo, Serikali iliunda Tume inayoongozwa na Profesa Sifuni Mchome kuchunguza matokeo hayo ili kupata ufumbuzi wa kudumu.
Muda mfupi baada ya tamko la Serikali, baadhi ya wadau wa elimu wameeleza kufurahishwa na uamuzi huo, huku Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kikiikosoa hatua hiyo, kuwa imekiuka sheria na kupora madaraka ya Baraza la Mitihani Tanzania (Necta).
Akitoa kauli ya Serikali bungeni kuhusu taarifa ya awali ya Tume ya Taifa ya Kuchunguza Matokeo ya Mtihani wa Taifa Kidato cha nne mwaka 2012 jana, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisema wameagiza Necta kuweka viwango ili matokeo ya wanafunzi yalingane na juhudi zao.
“Standardization ifanyike ili matokeo ya wanafunzi yalingane na juhudi wazizoziweka katika kusoma kwa mazingira, hali halisi ya Tanzania na uamuzi wa taifa kuongeza idadi ya shule na wanafunzi wakati uwekezaji katika ubora unaendelea,” alisema Lukuvi.
Lukuvi alisema Necta imeelekezwa kuwa licha ya sheria ya kuanzishwa kwake kuruhusu kufanya marekebisho ya mchakato wa mtihani, marekebisho yoyote ya kubadilisha utaratibu wa kupanga viwango vya ufaulu na madaraja ya mitihani yanatakiwa yahusishe wadau wote wanaohusika na mitalaa, ufundishaji na mtihani.
“Wakati Tume inaendelea kukamilisha kazi yake, uamuzi wa Necta kutumia utaratibu mpya wa kupanga viwango vya ufaulu na madaraja ya matokeo ya mitihani uliotumika 2012 usitishwe,” alisema Lukuvi na kuongeza:
“Badala yake Necta itumie utaratibu uliotumika mwaka 2011 kwa kidato cha nne na sita kwa mitihani yote, ikiwamo utaratibu wa Standardization na kutoa matokeo mapya kwa kuzingatia maelekezo haya.”
Pia, Serikalli imeagiza mchakato wa tuzo wa taifa (National Qualifications Framework) na Mfumo wa Kutahiniwa/ kuthamini maendeleo ya mwanafunzi masomo yake (National Assessment Framework) ukamilishwe haraka iwezekanavyo.
Katika mtihani wa mwaka 2012, wanafunzi 367,756 walifanya mtihani huo na waliofaulu ni 126,847. Waliofaulu kwa kwa madaraja ya kwanza hadi la tatu ni 23,520 sawa na asilimia 6.4 na daraja la nne ni 103,327 sawa na asilimia 28.1, huku 240,909 ambao ni asilimia 65.5 wakipata daraja sifuri.
Kauli ya CWT
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Ezekiel Oluoch alisema Baraza la Mawaziri limepora kazi za Bodi ya Baraza la Mitihani kwani ndio yenye jukumu la kufuta matokeo kisheria.
Mbali na hilo Oluoch alisema bado wanafanya utafiti ili kuona kama Baraza la Mawaziri lina uwezo wa kufuta matokeo na kuamuru mitihani isahihishwe upya, badala ya Bodi ya Baraza la Mitihani.
Oluoch aliyesema tamko rasmi la CWT kuhusu uamuzi huo wa Serikali litatolewa wiki ijayo, alieleza kuwa kwa sasa wanachunguza kuona kama jambo hilo lina usahihi kwa kiasi gani.
“Mitihani iliyofutwa ilitolewa na Bodi ya Necta ambayo ndio itakuwa na jukumu la kusimamia usahihishaji mpya na kutangaza tena matokeo.
Kama hali yenyewe ndio hiyo ni wazi kuwa haina tena uwezo wa kusimamia jambo hilo, inatakiwa kung’oka na kuundwa bodi mpya,” alisema Oluoch na kuongeza;
“Nasema hivyo kwa sababu hawawezi kula matapishi yao kwa kuwa wao ndio wenye mamlaka ya kutoa tena matokeo hayo na walishasema kuwa yalikuwa mabaya, sasa uzuri wake utatoka wapi tena.”
Alisema kuwa kufutwa kwa matokeo hayo kunaonesha wazi kuwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imeshindwa kazi ya kusimamia elimu nchini.
“Pia katika utangazaji wa matokeo anatakiwa waziri mpya wa kufanya hivyo kwa kuwa huyu wa sasa alieleza sababu za wanafunzi kufeli, sasa akiwa anatangaza matokeo mapya atatueleza nini,” alihoji.
Sababu za matokeo mabaya
Waziri Lukuvi alisema takwimu zinaonyesha kushuka kwa ufaulu huo unahusu shule zote na asilimia kwenye mabano, shule za wananchi (1.82); Shule za umma yaani kongwe (6.43); Binafsi (6.39) na Seminari (7.29).
Kuhusu matokeo ya kidato cha nne 2012, Lukuvi alisema tume imebaini licha ya wanafunzi kuwa kwenye mazingira yanayofanana na wenzao waliopita, ufanisi umekuwa ukishuka kwa sababu mbalimbali.
“Ufaulu wao umeshuka zaidi kwa sababu ya mabadiliko ya mchakato wa kuandaa na kutoa matokeo ya mtihani mwaka 2012, mfumo uliotumika kupanga matokeo na madaraja ni tofauti na ule uliotumika miaka iliyotangulia,” alisema Lukuvi na kuongeza:
“Uchunguzi unaonyesha kuwa mwaka 2011, Necta lilikuwa linachakata alama za mwisho kwa kutumia mfumo ambao ulikuwa unabadilika kutegemea hali ya ufaulu kwa mwanafunzi ambao ni National Mean Difference (NMD).
Alisema uataribu huo ulitokana na tofauti ya wastani wa kitaifa wa alama za maendeleo, kutoka alama ya maendeleo endelevu (Continued Assessment-CA) za watahiniwa wote na wastani wa kitaifa wa ufaulu wa mtihani wa mwisho kwa somo husika.
Aliendelea kuwa kila mtahiniwa aliongezewa NMD iliyokokotolewa kwenye alama za mtihani wa mwisho, ili kupata alama itakayotumika kupada daraja la ufaulu.
“Lakini mwaka 2012 lilitumia mfumo mpya wa kuwa na viwango maalumu vya kutunuku (Fixed Grade Range). Tume imebaini kwamba licha ya mfumo huo ulioandaliwa kwa nia nzuri, utaratibu huo mpya hakufanyiwa utafiti wa maandalizi ya kutosha kabla ya kutumika,” alisema.
Lukuvi alisema taarifa ya awali ya tume, inaonyesha kutokana na uchunguzi uliofanyika kwa muhtasari imebaini mambo mbalimbali.
Alisema matokeo ya  kidato cha nne kuanzia mwaka 2008 yamekuwa na mserereko wa kushuka tofauti na miaka iliyotangulia, kwa sababu ya changamoto zinazotokana na mafanikio yaliyopo sasa ya kuongezeka kwa idadi ya shule za msingi na sekondari, hususan mwaka 2011 na 2013 hivyo kuwa na idadi kubwa ya wanafunzi.
“Mwaka 1961 hadi 2011 idadi ya wanafunzi kwa shule za msingi imeongezeka kutoka 486,470 hadi 4,875,764, sawa na ongezeko la wanafunzi 4,389,294 kwa takriban miaka 40,” alisema.
Alisema wanafunzi wameongezeka kutoka 4,875,764 mwaka 2001 hadi 8,247,472 mwaka 2012, sawa na ongezeko la wanafunzi 3,371,708 kwa kipindi cha miaka 11.
Sekondari wanafunzi wameongezeka kutoka 11,832 mwaka 1961 hadi 289,699 mwaka 2001 sawa na ongezeko la wanafunzi 274,867 kwa miaka 40.
Lukuvi alisema kati ya mwaka 2001 hadi 2012 wanafunzi wameongezeka kutoka 289,699 hadi 1,884,270 sawa na ongezeko la watu 1,594,571.
Tume hiyo imebaini changamoto nyingine ni mazingira yasiyo ya kuridhisha ya kufundishia na kujifunzia, ikiwamo upungufu wa miundombinu muhimu ya shule; madarasa, madawati, maktaba, nyumba za walimu, bweni na majengo mengine muhimu.
“Kuna tatizo la uhaba wa walimu, vitabu, zana za kufundishia na matatizo ya ukaguzi wa shule. Vilevile tumebaini Mfumo wa Elimu ya Msingi na Sekondari unakabiliwa na changamoto nyingine mbalimbali ambazo taifa linapitia kwa sasa,” alisema Lukuvi na kuongeza:
“Yapo masuala ya sera, sheria, mfumo, muundo na changamoto za uhaba wa rasilimali fedha na watu. Tume inaendelea kufanyia kazi maeneo haya kwa kushirikiana na wataalamu na wadau wengine.”

source: Mwananchi

No comments:

Post a Comment