WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Wednesday, May 22, 2013

Kikwete atoa msimamo mkali


Rais Kikwete 

Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete amekemea vikali vurugu zilizotokea jana mkoani Mtwara baada ya kusomwa bungeni kwa Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini.

Akizungumza katika eneo la Kizota, Dodoma wakati wa kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Barabara ya Dodoma kwenda Iringa, Rais Kikwete alisema wote waliohusika na vurugu hizo watasakwa na kuchukuliwa hatua kali.

Rais Kikwete alisema rasilimali inayopatikana mahali popote pale nchini inatakiwa kutumiwa na Watanzania wote... “Hivi watu wa Nyarugusu wadai dhahabu ya pale au kinachopatikana Chalinze basi kisitumiwe na watu wa Morogoro! Hivi tutakuwa na taifa kweli?,” alihoji kwa ukali Rais Kikwete.

Rais Kikwete alisisitiza kuwa Serikali itawasaka wale wote wanaoongoza vurugu hizo na watawajibishwa kwa makosa hayo... “Tutawasaka hawa watu na viongozi wao hata kama wana mapembe kiasi gani, tutayakata.”

Alichosema Waziri Muhongo

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amesema mradi wa kusafirisha gesi kutoka mkoani Mtwara kwenda Dar es Salaam, umeanza kwa kasi na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda atakwenda huko wiki ijayo kuweka jiwe la msingi.

Akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini jana, Waziri Muhongo alisema:

“Mradi wa kujenga bomba la gesi uko palepale na unaendelea kwa kasi na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ataenda kuweka jiwe la msingi wiki lijalo.”

“Tumezungumza mengi kuhusu suala hilo na hata viongozi wa watu wa Mtwara walipelekwa nje kujifunza faida zake, lakini hata kama hawajaelewa, nimetoa kijitabu kinachozungumzia faida mbalimbali watakazopata wana Mtwara katika mradi huo.”

Profesa aliyeanza hotuba yake kwa kueleza machapisho mbalimbali yaliyotolewa na wizara yake kufafanua faida za gesi ya Mtwara kwa taifa, alisema mradi huo uliozinduliwa Novemba mwaka jana na Rais Kikwete, unahusisha ujenzi wa bomba lenye urefu wa kilometa 532 na kipenyo cha nchi 36.

“Bomba hilo lina uwezo wa kusafirisha futi za ujazo za gesi milioni 784 kwa siku. Mradi utahusisha mitambo miwili ya kusafirisha gesi asilia katika maeneo ya Mnazi Bay- Madimba (Mtwara) na Kisiwa cha Songosongo (Lindi). Utagharimu Dola za Marekani 1,225.3 milioni,” alisema.

Alisema kazi za usanifu wa mradi na ulipaji fidia kwa wananchi wapatao 3,092 waliopisha maeneo ya mradi, zimekamilika na hatua za awali za ujenzi wa mitambo ya kusafirisha gesi asilia zimeanza.

Alisema hadi sasa visima viwili vya maji vyenye uwezo wa kuzalisha mita za ujazo 50 kwa saa kwa kila kimoja, vimekamilika.

“Visima hivyo ni kwa ajili ya mitambo ya kusafirisha gesi asilia katika eneo la Madimba na kwa matumizi ya wananchi,” alisema na kubainisha kuwa vifaa mbalimbali vya ujenzi wa nyumba za wafanyakazi wa mradi vimewasili nchini mwishoni mwa Aprili mwaka huu.
Upinzani

Msemaji wa Kambi ya Upinzani katika Wizara ya Nishati na Madini, John Mnyika amepinga mradi huo wa kusafirisha gesi akitaka kwanza mikataba yote iwekwe wazi na wananchi washirikishwe ili wajue faida yake.

“Kambi rasmi ya upinzani inayoongozwa na Chadema inaitaka Serikali isiendelee na ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara mpaka Dar es Salaam hadi; Mosi, itakapoweka wazi kwa Bunge mikataba yote inayohusu uendelezaji wa gesi asilia ikiwamo ya ujenzi wa bomba hilo, pili ikutane na wananchi kuwashirikisha na kuhakikisha manufaa kwa taifa na kwao,” alisema Mnyika.

Hata hivyo, mjadala wa bajeti hiyo ulisitishwa jana na Spika wa Bunge, Anne Makinda alipoahirisha Bunge saa 11.00 jioni ili kutoa nafasi kwa Kamati ya Uongozi ya Bunge kujadili suala hilo baada ya kuonekana kuwa limekoleza zaidi mgogoro huo.

“Wiki mbili zilizopita tulipopanga tutajadili bajeti hii tulisikia (wananchi) walipanga kufanya matatizo na kweli leo wakati tunajadili tayari wamefanya matatizo. Nafikiri wengi hapa mnataka tujadili suala hili kwa dharura, nakiri suala hilo lipo. Naiagiza Serikali kesho watoe hali halisi ilivyo kule Mtwara.
Faida za gesi kwa Wanamtwara
Waziri Muhongo ametaja moja ya faida za ujenzi wa bomba hilo kwa wananchi wa mikoa ya kusini kuwa ni tozo ya asilimia 0.3 ya mauzo ya gesi asilia pamoja na huduma za zahanati, shule, umeme, maji na ufadhili wa mafunzo katika Vyuo vya Veta na sekondari.

“Faida nyingine zitakazopatikana ni ujenzi wa viwanda mbalimbali ikiwamo cha Saruji cha Dangote ambacho ujenzi wake umeanza, kiwanda cha mbolea, mtambo wa kufua umeme wa MW 400 kupitia Kampuni ya Symbion na njia za kusafirisha umeme ya msongo wa KV 220 kutoka Mtwara hadi Songea.”

“Aidha, Kampuni ya Schlumberger ya Houston, Marekani imejenga karakana kubwa Mtwara ambayo itakuwa inatengeneza vifaa vya uchimbaji, utafutaji na uendelezaji wa rasilimali za mafuta na gesi.”

Baadhi ya wabunge wa mikoa ya Kusini wamesema hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini haina mkakati wowote wenye lengo la kutatua mgogoro wa gesi asilia unaendelea mkoani Mtwara.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, walisema mgogoro huo umefikia pabaya na njia pekee ya kuutatua ni Serikali kufanya mazungumzo na wananchi.

“Ni vigumu kusema hotuba ya Serikali inaweza kutatua tatizo hilo,” alisema Mbunge wa Viti Maalumu (CUF), Clara Mwatuka na kuongeza kuwa kinachoonekana ni kama Serikali inatumia mabavu kushughulikia suala hilo.

Mbunge wa Lindi Mjini (CUF), Salum Barwany alisema kinachotakiwa ni Serikali kuandaa mjadala wa kina na wakazi wa Mtwara.

source: mwananchi

No comments:

Post a Comment