WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, May 23, 2013

Hali mbaya

  Mmoja afa, wengine wajeruhiwa
  Nyumba ya waziri, mbunge zachomwa
 
 
Mkuu wa jeshi la polisi nchini, IGP Said Mwema.
Machafuko yamelipuka katika Manispaa ya Mtwara Mikindani baada ya wananchi wa mji huo kuchoma moto ofisi za serikali na nyumba za viongozi wa serikali takribani sita, ikiwamo ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikao na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia na inaripotiwa kuwa mtu mmoja amekufa katika vurugu hizo na wengine kadhaa kujeruhiwa.
Wananchi hao wamefanya uasi huo na uharibifu mkubwa wa mali kupinga uamuzi wa serikali kusafirisha gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam kabla ya kujua mikoa ya kusini itanufaika vipi.

Uchomaji huo ambao pia ulihusisha ofisi za Chama Cha Mapinduzi (CCM) ulianza kutekelezwa jana kuanzia saa 5:00 asubuhi baada ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, kuwasilisha hotuba ya bajeti ya mwaka 2013/2014 katika kikao cha Bunge mjini Dodoma.

Taarifa ambazo NIPASHE imezipata na kuthibitishwa na viongozi wa serikali wa wilaya ya Mtwara, zilieleza kuwa ofisi za serikali za kata za Majengeni, Mtonya na Changani zilichomwa moto.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara, Linus Sinzumwa, alisema kuwa watu 91 walikamatwa kuhusiana na vurugu hizo ambazo zilijitokeza zaidi katika maeneo ya Magomeni na Soko Kuu la Mtwara.

Alisema kuwa nyumba kadhaa za askari polisi mjini Mtwara zilivunjwa na kwamba kutokana na vurugu hizo, abiria waliokuwa wanasafiri kwenda Mtwara kutokea Dar es Salaam waliishia Lindi kuhofia usalama wao.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Wilman Ndile, alisema ofisi ya CCM Wilaya ya Mtwara, ofisi ya Mbunge wa Mtwara Mjini (CCM), Hasnain Murji, na nyumba ya Waziri Ghasia zilichomwa moto.

Alisema wananchi hao pia walichoma jengo la Mahakama ya Mwanzo Mikindani na kwamba hadi saa 11:40 jioni hali ilikuwa tete katika mji wa Mtwara kutokana na wananchi kuendelea kufanya vurugu ambazo zilifuatana na uharibifu wa mali.

Nyumba ya mtangazaji wa Shirika la Utangaza Tanzania (TBC), Kassim Mikongoro, ilichomwa moto.

Alisema dalili za kutokea machafuko hayo zilianza mapema jana asubuhi kutokana na huduma mbalimbali ukiwamo usafiri wa magari, pikipiki na maeneo ya kutolea huduma za afya kusitishwa, hali iliyozua wasiwasi mkubwa kwa wananchi.

“Tangu asubuhi huduma za mama lishe, usafiri wa bodaboda, bajaji, mabasi, hospitali na vituo vya mafuta vilivyopo mjini Mtwara hawakufanya kazi kama serikali tukaanza kujipanga kwamba hapa kutakuwa na vurugu,” alisema Ndile.

Alisema baadaye vurugu zilianza kulipuka na wananchi kuanza kuzichoma moto ofisi nne za serikali za kata za Mtwara Mjini na ofisi ya CCM wilaya na kufanya uharibifu wa mali za watu kadhaa.

Kabla ya RPC Sinzumwa kuelezea hali hiyo, DC  Ndile alisema kutokana na vurugu hizo hadi kufika sa 9:30 alasiri, watu zaidi 50 walikuwa wamekamatwa na Jeshi la Polisi kuhusiana na ghasia hizo na kwamba hadi saa 4:30 jioni mji wa Mtwara ulikuwa haujatulia kutokana na wananchi kuendelea kufunga barabara kuu.

Mkuu huyo wa wilaya alisema madai ya wananchi hao ni kupinga gesi ya Mtwara kusafirishwa kwenda Dar es Salaam kabla ya kujulishwa kama watanufaika vipi na nishati hiyo.

Meya wa Manispaa ya Mtwara, Msharika, alisema hali ilikuwa tete na kwamba kila mkazi wa mji huo alijifungia nyumbani kwake.

“Unavyoongea na mimi hapa nimejifungia ndani na familia yangu hasa ukizingatia sisi viongozi ni ‘wanted’ (tunatafutwa), mabomu yanaendelea kupigwa kila eneo na vyombo vya ulinzi na usalama vinaendelea kutekeleza kazi yake.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mtwara, Mohamed Sinani, alisema alipata taarifa za kuchomwa kwa ofisi ya CCM Wilaya ya Mtwara.

“Hivi sasa nipo Dar es Salaam, lakini nimepewa taarifa kwamba ofisi ya CCM imechomwa moto, lakini sijafahamu sababu hasa za wananchi kufanya tukio hilo,” alisema Sinani.

SHULE ZAFUNGWA
Taarifa zaidi ambazo NIPASHE ilizipata zilieleza kuwa kutokana na vurugu hizo, shule za msingi za Shangani na Chikongola zilifungwa kwa muda na wanafunzi waliruhusiwa kurejea kwao hadi hapo watakapotangaziwa tena.

Mwalimu Charles Makolo  wa Shule ya Msingi Shangani, alisema wamewarejesha wanafunzi majumbani kwao kwa siku mbili hadi hapo hali ya usalama itakapotengamaa.

Mwalimu Joseph Kandeo wa Shule ya Msingi Chokongola, alisema waliwarejesha wanafunzi kwao hadi hapo watakapotangaziwa tena.

Taarifa zinaeleza kuwa dalili za kutokea machafuko hayo zilianza baada ya kusitishwa ghafla kwa matangazo ya TBC katika mji wa Mtwara saa 2:00 wakati wananchi hao wakifuatilia mkutano wa Bunge.

Wananchi walianza vurugu hizo kwa kuchoma matairi barabara na mitaani hali iliyolilazimu Jeshi la Polisi kupiga mabomu kuwatawanya, lakini vurugu hizo zilisambaa katika maeneo mengi ya mji huo.

“Ona sasa hata matangazo ya bunge wamekata, wanamaanisha nini wakati sisi tunahitaji kufahamu hatma yetu,” alisema Ali Hamis mfanyabiashara wa Soko Kuu.

Hamis alidai kuwa kusitishwa kwa matangazo ya moja kwa moja ya mkutano wa Bunge ni njama za serikali ili wananchi wa mikoa ya kusini wasiweze kusikiliza suala la gesi.
Hata hivyo, ilipofika saa 3:55 asubuhi matangazo ya Bunge ambayo yanarushwa na TBC kutoka mjini Dodoma yalirejea.

Kwa mujibu wa ratiba ya Bunge, vikao huanza saa 3:00 asubuhi kwa kipindi cha maswali na majibu hadi saa 4:00 asubuhi. Hotuba na miswada mingine ya serikali hufuata baada ya kipindi hicho kuanzia saa 4:00.

Jana hotuba ya Waziri wa Nishati na madini ilianza kusomwa takribani saa 4:20.

Ilipofika saa 6:00 mchana askari waliokuwa katika doria maeneo ya Soko Kuu la Mtwara  vijana walilizunguka huku wakiwazomea kwa kuwarushia mawe.

Vurugu hizo ziliendelea kwa wananchi kufunga barabara kuu ya Mtwara-Dar es Salaam kwa kuweka mawe na magogo katikati katika eneo la Mkanaledi na baadaye polisi walifika eneo hilo na kufungua barabara hiyo.

Aidha, waandishi wa habari mkoani hapa walipata wakati mgumu kutekeleza majukumu yao kutokana na wananchi madai kuwa baadhi ya wananchi walitaka kuwadhuru kwa kuwatuhumu kuwa  wanaandika taarifa kuegemea upande wa serikali.

HALI YA USAFIRI
Machafuko hayo yalisababisha mji wa Mtwara kukumbwa na tatizo la usafiri kutokana na vyombo vinavyotoa huduma ya usafiri kusitisha huduma.
Salum Juma, mwendesha boda boda mjini Mtwara, alisema kuwa alipokea vitisho kutoka kwa wananchi wakimtaka kuacha kupakia abiria na kuwa atakayekaidi atalazimisha pikipiki yake itachomwa moto.

UPORAJI
Diwani wa Kata ya Likombe, Mukhusin Komba, alisema wananchi walivamia nyumba yake na kuvunja duka, kuiba vitanda vitatu na magodolo manne.

Meneja wa Posta tawi la Mtwara, Omari Kilimo, alisema kuwa toka asubuhi hakukuwa na mteja aliyefika katika ofisi yake kwa ajili ya kupata huduma.

HOSPITALI YA RUFAA LIGULA
Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Ligula, Mohamed Kodi, alithibitisha kupokea maiti ya mtu mmoja ambaye inadaiwa alifariki katika vurugu hizo.

Alibainisha kuwa walipokea majeruhi kadhaa ambao idadi yao haikufahamika na kuwa wamelazwa katika hospitalini hapo.

Naye Mkuu wa Chuo Kikuu cha Stella Maris Mkoa wa Mtwara, Dk. Longino Rutagwelela,  alisema kuwa waliamua kusitisha masoma baada ya wanachuo kuhofia hali ya usalama wao. 

JK AONYA
Rais Jakaya Kikwete amesema amepata taarifa za vurugu mkoani Mtwara na kwamba wahusika watakamatwa na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Alisema wananchi lazima watambue kuwa rasilimali za nchi hii ni za watu wote, hivyo wanaodai gesi isiende kokote hayo ni maajabu.

Rais Kikwete alisema serikali haijaisahau mikoa ya kusini ukiwamo Mtwara kama wanavyodhani baadhi ya watu kwani ipo miradi mikubwa ambayo imepelekwa mkoani humo.

BUNGE LASITISHWA
Bunge jana lilishindwa kuendelea na kikao cha jioni na kuahirishwa hadi leo ili kuipa nafasi Kamati ya Uongozi wa Bunge kukaa na kuangalia uwezekano wa  Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwenda mkoani Mtwara.

Hatua hiyo ilitangazwa jana jioni na Spika wa Bunge, Anne Makinda, wakati wabunge walipoingia kuendelea mjadala wa hotuba ya bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini.

Aliitaka Serikali kutoa taarifa kuhusiana na tukio hilo leo asubuhi kwa kuwa wabunge hawawezi kujadili kitu ambacho hawana taarifa za kutosha.

WANAJESHI WATATU WAFA
Habari tulizozipata wakati tunakwenda mitamboni, zilieleza kuwa wanajeshi watatu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ)  walifariki dunia kwa ajali wakiwa njiani kuelekea Mtwara kwa operesheni maalum.

Habari za mitandao ya kijamii zilisema kuwa askari hao walikufa wilayani Nachingwea wakitoka Lindi kwenda Mtwara, wengine 23 wamejeruhiwa katika ajali hiyo.

Hata hivyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Lindi, George Mwakajinga, alisema hana taarifa kamili za vifo ingawa alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kwamba askari polisi walikua wanaelekea katika eneo la ajali.

 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment