WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, October 26, 2012

Hotuba ya Dk Shein Baraza la Idd el Hajj leo



HOTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI,  MHESHIMIWA DKT. ALI MOHAMED SHEIN, KWENYE BARAZA LA IDD EL HAJJ  TAREHE 26 OKTOBA, 2012

 
Bismillah Rahman Rahim

Shukrani zote anastahiki Mwenyezi Mungu Mtukufu, Subhanahu Wataala, Aliyetupa uhai na uzima tulionao tukaweza kuitikia wito wake, alioutoa tangu zama za Nabii Ibrahim (AS). Katika Kur-ani imeelezwa kwamba Nabii Ibrahim ameamriwa kuwatangazia watu  kwenda kuhiji na watakuja kutoka kila upande wa dunia na kwa kila kipando. Mwenyezi Mungu ndie aliyewakirimu Waislamu wenzetu kwa mamilioni, kuitikia wito huo na kuwapa uwezo wa kwenda kuizuru nyumba tukufu ya Alkaaba huko Makka mwaka huu wakiwa wamoja, kwa wakati mmoja kwa lengo la kumuabudu Yeye Mola wetu Mmoja.
Tunashuhudia kuwa hapana anaepaswa kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah (SW), Ambaye ndiye Mmiliki wa vyote na Kwake vyote vitarejea.  Sala na salamu zimshukie Hashimu, Mtume wa Mwenyezi Mungu, Bwana wetu Muhammad (SAW) na wafuasi wake walioshikamana na mwenendo wake na mafundisho, na wakaongoka. Inshaalla Mwenyezi Mungu atujaaliye na sisi tuwe miongoni mwao - Amin.
Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad,
Makamu wa Kwanza wa Rais;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Idd,
Makamu wa Pili wa Rais;
Mheshimiwa  Dk. Amani Abeid Karume, na Mama Shadya Karume,
Rais Mstaafu wa Zanzibar;
Mheshimiwa Pandu Ameir Kificho,
Spika wa Baraza la Wawakilishi;
Mheshimiwa Omar Othman Makungu,
Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar,
Othman Masoud;
Mheshimiwa Sheikh Khamis Haji Khamis,
Kadhi Mkuu;
Mheshimiwa Naibu Mufti
Sheikh Mahmoud Mussa Wadi
Waheshimiwa Mawaziri,
Waheshimiwa Mabalozi,
Waheshimiwa Wabunge na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi,
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama Vya Siasa mbali mbali,
Ndugu Wageni Waalikwa,
Mabibi na Mabwana.     
Assalamu Alaykum Warahmatullah Taala Wabarakatuhu
IDD MUBARAK
Namshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema na Utukufu, Muumba wa Mbingu na Ardhi na vyote viliomo na Mfalme wa siku ya Mwisho kwa ukarimu wake kwetu; Ametukarimu neema ya uhai tukaweza kuhudhuria hafla hii adhimu. Ni uwezo wake Yeye tu Subhanahu Wataala ndio uliotuwezesha kukutana hapa kwa kujumuika na kuungana na Waislamu wenzetu walioko huko katika mji Mtakatifu wa Makka ambao wanaitekeleza nguzo ya tano ya dini ya Kiislamu; Ibada ya Hijja.
Kwa hakika, tuna wajibu wa kuwatakia kheri na baraka ndugu zetu na Waislamu wote ambao Mwenyezi Mungu amewaruzuku uwezo wa kwenda Hijja mwaka huu. Tumuombe Mola wetu azitakabalie ibada zao na awarudishe nyumbani kwa salama ili waungane tena na familia zao, ndugu zao, jamaa zao na majirani zao na huku wakiendeleza mafunzo waliyoyapata katika mkusanyiko huo wa kila mwaka wa waislamu duniani.
Ndugu Wananchi,
Wakati huu ambao tumo katika furaha ya kusherehekea sikukuu hii, tunapaswa tuzingatie mambo ambayo tunajifunza kutokana na sikukuu hii muhimu kwa waislamu wote duniani.  Ni dhahiri kuwa miongoni mwa mafunzo muhimu tunayopata, ni kwa watu kuwa pamoja katika hali ya amani na kutii amri ya Mola wetu bila ya kujali tofauti tulizonazo za utaifa, jinsia na uwezo wa kiuchumi. Ni uwezo na utukufu wa Mola wetu kutuwekea mkusanyiko huu mkubwa kwani anajua udhaifu wa wanadamu unaopelekea kuibuka kwa migogoro na mivutano miongoni mwetu jambo ambalo tayari alikwishatuelekeza katika aya ya 13 ya Suratush-Shuura kwa kusema:
“Amekupeni Sharia ya Dini ile aliyomuusia Nuhu na tuliyokufunulia wewe na tuliyowausia Ibrahim na Mussa na Issa, kwamba simamisheni Dini wala msifarikiane kwayo, (kwa ajili ya dini); ni ngumu kwa wenye kushirikisha (dini hii) unayowaitia; Mwenyezi Mungu humchagua Kwake amtakaye na humuongoza Kwake aelekeaye (Kwake).
Ndugu Wananchi,
Mafunzo mengine tunayopata kupitia ibada ya Hijja ni utii wa Waislamu kwa Mola wao katika kuzitumia neema za uwezo wa mali na siha kwa ajili ya kutafuta radhi za Mwenyezi Mungu. Watu ambao, wameahidiwa fadhila kubwa kama inavyothibitika kwenye aya ya 69 ya Suratul An-nisaa
“Na wenye kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume, basi hao watakuwa pamoja na wale aliowaneemesha Mwenyezi Mungu, Manabii na Masidiki na Mashahidi na Masalih (watu wema)….. “
Sote ni mashahidi kuwa si kila mwenye uwezo wa mali au siha hudiriki kutekeleza ibada hii. Wenzetu hawa Mwenyezi Mungu amewaafikishia kutekeleza nia zao na wamefaulu kumshinda iblisi ambaye hupenda kuwazaini wanadamu katika njia ya Mwenyezi Mungu ili watumie neema alizowapa katika kumuasi.
Tumuombe Mwenyezi Mungu atujaalie kuyatumia mafunzo yote yanayopatikana kwenye ibada zetu katika kulikamilisha lengo la kuumbwa kwetu na kuletwa duniani. Awajaalie mahujaji wote na sisi tuzitumie vyema neema alizoturuzuku Allah.
Ndugu Wananchi,
Tuna wajibu mkubwa wa kumshukuru Mola wetu (SW) kwa neema zisizomithilika alizoturuzuku sisi wanadamu na kutufanya tuwe viumbe bora na Makhalifa wa dunia.  Katika kuweza kumudu jukumu hilo, Allah ameturuzuku akili tuitumie kupambanua utukufu wake katika kuiumba dunia na viliomo na kuvitumia katika kumtukuza Yeye katika maisha yetu ya hapa duniani ili tupate mafanikio mema huko Akhera.
Mwenyezi Mungu anatubainishia hayo katika aya ya 15 ya Suratul Mulk kuhusu kuitumia vyema neema ya ardhi aliyotupa kwa kusema,
“Yeye ndiye aliyefanya ardhi iweze kutumika kwa ajili yenu. Basi nendeni katika pande zake zote na kuleni katika riziki zake, na kwake Yeye ndiyo marejeo (yenu nyote)”.
Ndugu Wananchi,
Mwenyezi Mungu ametujaalia nchi ndogo yenye watu wenye uhusiano wa karibu wa udugu, tuna watu wenye maarifa makubwa ya elimu mbali mbali na afya za kiwiliwili.   Kadhalika,
tuna rasilimali ya bahari, misitu, ardhi ya kilimo na maliasili nyenginezo ambazo wenzetu wengine hawajabahatika kuwa nazo.  Serikali zote duniani hujiwekea mipango ambayo huwa ndiyo dira ya kufuata katika matumizi ya rasilimali zake.
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tangu Awamu ya Kwanza hadi sasa imejitahidi kupanga mipango mbali mbali ya maendeleo katika vipindi tofauti, ili kuweza kuzitumia vyema rasilimali ziliopo kwa lengo la kuinua uchumi wetu na kuleta ustawi bora wa wananchi wa Zanzibar. Sote tunakiri kuwa nchi yetu imepiga hatua ya kupigiwa mfano katika maendeleo kwenye nyanja za uchumi na ustawi wa jamii tangu Mapinduzi ya Zanzibar ya tarehe 12 Januari, 1964.
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba, ilipoingia madarakani miaka miwili iliyopita, iliahidi kuendeleza mipango hiyo na kudumisha mafanikio yake. Miongoni mwa mpango mkuu wa Serikali ni DIRA 2020 ambayo sasa imeshatimia miaka 12 katika utekelezaji wake na kubakiwa na miaka minane.
Dira hii ndiyo iliyotuwezesha kuandaa mikakati mbali mbali ya kitaifa ya muda tofauti ukiwemo Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini Zanzibar (MKUZA). Hivi sasa tuna mpango wa uchumi unaotokana na MKUZA II uliotayarishwa kwa kipindi cha miaka 5 ulioanza mwaka 2010 hadi mwaka 2015, na baada ya hapo utapangwa mpango mwengine wa miaka mitano utaokaoanza mwaka 2015 hadi kufikia mwaka 2020.
Ndugu Wananchi,
Ripoti ya mapitio ya Dira 2020 iliyotolewa hivi karibuni imeonesha kwamba yapo mafanikio ya kutia moyo yaliyopatikana katika utekelezaji wa Dira ya 2020, lakini bado tuna kazi kubwa ya kufanya ili tuweze kuyafikia malengo yetu kwa muda uliobakia. Malengo hayo yatafikiwa iwapo kila mtu atafahamu kuwa ushiriki wake katika utekelezaji ni sehemu ya mafanikio ya utekelezaji wa mipango hiyo.
Kadhalika, kila mtu mahali alipo aongeze bidii ya kufanya kazi kwa kuongeza uzalishaji na utoaji wa huduma. Wakulima, wavuvi na wafugaji waongeze bidhaa wanazozizalisha kwa kutumia fursa zilizokwishaandaliwa na Serikali. Wafanyakazi katika sekta mbali mbali ikiwemo sekta ya elimu, afya, biashara, mawasiliano, nishati, maji na nyenginezo waimarishe utoaji wa huduma zao ili kwa pamoja ziwe kichocheo cha kuleta ustawi bora wa jamii na kupunguza umasikini. Tutilie maanani usemi maarufu kuwa “juhudi ndiyo siri ya mafanikio”.
Ndugu Wananchi,
Tunapozungumzia haja ya kushirikiana katika utekelezaji wa mipango ya Serikali, tunapaswa pia tuzingatie matumizi bora ya rasilimali tulizonazo ili ziwe endelevu. Nchi yetu ina ardhi ndogo isiyoongezeka lakini idadi yetu inaongezeka kwa wastani wa asilimia 3.1 kila mwaka. Hali kama hii inasababisha kuendelea kuwepo kwa mahitaji makubwa ya ardhi ya kujenga makaazi na matumizi makubwa ya rasilimali ikiwemo misitu na rasilimali nyengine zisizorejesheka.
Katika kukabiliana na changamoto kama hizi, ndipo Serikali inapolazimika kuandaa taratibu, sheria na sera mbali mbali za kusimamia matumizi bora ya rasilimali.  Mathalan, Serikali imeandaa Sheria ya matumizi ya Ardhi na pia Sheria ya Mipango Miji, ili ardhi yetu itumike kwa utaratibu mzuri.  Kadhalika, Sheria ya kuzuia uvuvi haramu ina madhumuni ya kuifanya amali hiyo ambayo ni tegemeo la wananchi wengi hapa Zanzibar iwe endelevu, yenye tija na itufae tuliopo na watakaokuja.  Kwa hakika, hii itakuwa namna bora ya kuzitumia neema hizi alizoturuzuku Mwenyezi Mungu.
Ndugu Wananchi,
Dini yetu ya Kiislamu inatufundisha kuwafikiria wengine hasa katika mambo ya neema na kheri na kuwaepusha na matatizo.  Ndiyo maana tunaamrishwa kutoa sadaka ambayo siri yake kuu ni kujiepusha na ubinafsi na kumkuza mja kuwa na roho ya imani kwa wengine.  Sadaka huitakasa nafsi ya mja na kumwelekeza mtu kwenye imani na kufanya ihsani.  Mwenyezi Mungu amesema kwenye kitabu kitukufu cha Kur-ani aya ya 90 ya Suratun Nahl:
Kwa hakika Mwenyezi Mungu anaamrisha uadilifu, na kufanya hisani na kuwapa jamaa (na wengineo); na anakataza uchafu na uovu, na dhulma.  Anakunasihini ili mupate kufahamu (mfuate).”
Katika kukamilisha sherehe ya Idd hii huwa tunahimizwa kuchinja na kuwapa haki tuliowajibishwa wakiwemo masikini na marafiki. Suna hii ikiwa ni kiashirio cha utii aliouonesha Nabii Ibrahim (AS) katika kumchinja mwanawe Ismail kwa kuonesha utii kwa Mola wake. Basi katika kufikiria wenzetu, tugawe nyama hiyo tunayochinja kama inavyoelezwa na kuwafikiria zaidi masikini.
Ndugu Wananchi,
Tuzitumie vizuri rasilimali ziliopo nchini kwa ajili ya maendeleo yetu hivi sasa, lakini wakati huo huo tuoneshe imani zetu kwa kuwafikiria wenzetu wengine watakaozihitaji rasilimali hizi katika miaka ijayo. Kwa mfano tunapokata misitu ovyo, kukata miti kwenye vianzio vya maji, kuchimba mchanga bila ya taratibu na kuchimba mawe na matofali ni baadhi tu ya shughuli ambazo huharibu sana mazingira yetu na kuviachia vizazi vijavyo mazingira yasiyo na ubora.
Serikali kupitia taasisi zake mbali mbali imeweka taratibu na sheria za kukabiliana na vitendo vinavyosababisha uharibifu wa mazingira. Hivyo, ni wajibu wa wananchi kufuata taratibu hizo na kuzingatia ushauri wa kitaalamu ili mazingira yetu yawe endelevu kama ni njia moja ya kubainisha imani zetu kwa kuwafikiria wengine.
Ndugu Wananchi,
Serikali itaendelea kuwaelimisha wananchi umuhimu wa kufuata taratibu kama hatua muhimu ya kuimarisha utawala bora nchini.  Hata hivyo, suala la kusimamia taratibu na kuona kuwa Sheria zetu zinazingatiwa ni la kila mwananchi na siyo la Serikali peke yake. Kwa mfano, Serikali imetumia fedha nyingi katika kujenga miundombinu ya barabara, kuweka nguzo za kupitishia umeme mkubwa na vifaa mbali mbali vya kupitishia mtandao wa “e-government” katika maeneo mbali mbali ya nchi yetu. Lakini taarifa nilizonazo ni kuwa kuna baadhi ya wananchi wenye tamaa na wanaoweka mbele maslahi yao na kwa hivyo, wameanza kuihujumu miundombinu hii kwa namna mbali mbali zikiwemo kuchimba mchanga chini ya nguzo kuu za umeme na kukata waya za umeme kwa ajili ya kuuza shaba. Kadhalika, viguzo na paipu zitakazotumika kupitishia waya za mtandao zimeanza kuharibiwa kwa namna tofauti wakati huu ambao Serikali inakaribia kuizindua miradi hiyo muhimu kwa maendeleo yetu.
Zaidi ya hayo, katika nyakati tofauti baina ya mwezi wa Mei, Julai na Oktoba, 2012; tumeshuhudia barabara zetu kadhaa zimeharibiwa kwa kuchomwa moto mipira mibovu ya gari katika mji wa Unguja.  Vile vile, miti iliyopandwa pembeni mwa barabara ilikatwa matawi na mengine kung’olewa kwa hasira na jazba zisizo na tija.  Mambo yote haya yaliyofanyika yameitia hasara Serikali.  Kwa upande wake, Serikali itaendelea kuwachukulia hatua za kisheria wale wote wanaosababisha uharibifu na kuitia hasara Serikali.
Ndugu Wananchi,
Wakati huu tunaposherehekea sikukuu ya Eid el Hajj tayari tumo kwenye Msimu wa mvua za Vuli. Katika wiki chache zilizopita tulianza kuziona mvua zikinyesha kwenye maeneo machache kwa kiwango kidogo na taarifa za utabiri, zilisema kuwa tutarajie kupata mvua nyingi. Siri halisi anayejua ni Mwenyezi Mungu (SW). Hata hivyo, ingawa mvua bado hazijaanza kwa kasi tunapaswa kujitayarisha hasa katika shughuli za kilimo. Serikali kupitia Wizara ya Kilimo na Maliasili tayari imeshaanza kuwahudumia wakulima kwa kuwachimbulia mashamba yao kote Unguja na Pemba.
Katika Msimu huu, lengo letu ni kulima hekta 40,000. Serikali imeshaagiza tani 1500 za mbolea na lita 30,000 za dawa ya kuulia magugu. Hivi sasa kuna idadi ya matrekta 37 na tayari Serikali imeshaagizia matrekta mapya 20 ili kuimarisha upatikanaji wa huduma zake.
Nawasihi wakulima wote wazingatie taratibu zilizowekwa na Serikali katika kuwapatia huduma za matrekta na pembejeo nyengine za kilimo. Serikali itajitahidi kuzifanyia kazi changamoto zote zilizo ndani ya uwezo wake ili kuwasaidia wakulima na kuelekea katika lengo kuu la Serikali la kuimarisha sekta ya kilimo kwa lengo la kuyafanikisha Mapinduzi ya Kilimo nchini.
Ndugu Wananchi,
Napenda kutoa pongezi na shukurani kwa wakulima wote nchini kwa kuhamasika kuzitumia fursa zilizowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kutoa ruzuku katika huduma na pembejeo za kilimo.
Pamoja na kuwepo uchache wa mvua kwa msimu uliopita, baadhi ya maeneo hapa nchini yameonesha kunufaika na azma hiyo njema iliyowekwa na Serikali.  Zaidi ya hayo, tumeweza kupata mafanikio kwenye uzalishaji wa mazao ya chakula zikiwemo ndizi, muhogo, viazi vitamu na vyenginevyo, mazao ambayo yalisaidia sana kupunguza mfumko wa bei za vyakula.
Natoa wito kwa wakulima na wananchi wote wazitumie mvua za Vuli pale zitakapokuwa zinanyesha kwa ajili ya kilimo na pia kwa ajili ya upandaji wa miti ya misitu, biashara na matunda. Naelewa kuwa tayari kuna miche mingi ya aina mbali mbali ya miti, katika vitalu vinavyomilikiwa na Serikali na vile vya watu binafsi inayosubiri ichukuliwe na ipandwe mashambani. Tutakapozitumia mvua hizi za vuli kwa shughuli za kilimo na upandaji miti tutakuwa tumeitumia vyema neema hii aliyoturuzuku Mwenyezi Mungu na pia tutayaimarisha mazingira yetu yanayozidi kuharibiwa. Kila mwananchi aweke azma ya kupanda miti kabla ya kukata mti.
Kadhalika, taarifa za uwezekano wa kuwepo mvua nyingi ni kauli ya tahadhari kwa wananchi wanaoishi mabondeni yakiwemo mabonde ya mpunga. Wenzetu hao wanapaswa kuzingatia usemi mashuhuri wa “Tahadhari kabla ya athari” au “kinga ni bora kuliko tiba”. Vile vile, napenda kuzikumbusha taasisi zetu zinazoshughulikia majanga ikiwemo Idara ya Kukabiliana na Maafa na Kikosi chetu cha Zimamoto na Uokozi kufanya matayarisho ili tuweze kukabiliana na hali hiyo itakapotokea pamoja na kuendelea kuwaelimisha wananchi namna bora ya kupambana na maafa.
Ndugu Wananchi,
Napenda kuwanasihi wananchi wote juu ya umuhimu wa kuimarisha umoja na mshikamano wetu ambao ndio msingi mkubwa wa amani na utulivu tulionao.  Ni wajibu wetu tuiendeleze amani yetu na mshikamano ambao ndiyo siri kubwa ya mafanikio tunayoendelea kuyapata.
Tuna wajibu wa kumshukuru Mola wetu (SW) kwa kuturuzuku neema hii ambayo tumeitafuta kwa muda mrefu.  Mwenyezi Mungu anatupa habari ya jambo kama hili katika aya ya 61 ya Suratul Anfal kwa kusema:
“Na kama, wakielekea katika amani, nawe pia elekea na mtegemee Mwenyezi Mungu.  Hakika Yeye ndiye Asikiaye na Ajuaye”.
Na pia akasema katika aya ya 63 ya sura hio hio kwamba:
“Na akaziunga nyoyo zao; hata kama ungalitoa vyote vilivyomo ardhini usingaliweza kuziunga nyoyo zao, lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaunganisha.  Hakika Yeye ni Mbora na Mwenye hekima”.
Nasi Mola wetu kwa hekima zake ameshaziunganisha nyoyo zetu na tunaishi kwa amani.  Kwa hivyo, kuishukuru neema hii, ni kuilinda na kuiendeleza na kujiepusha na vitendo vyote vitakavyoweza kuiondosha na kuturudisha nyuma tulikotoka.
Ndugu Wananchi,
Katika hotuba yangu niliyoitoa katika Baraza la Idd el Fitr mwezi Mosi Mfungo Mosi mwaka 1433 Hijriya sawa na tarehe 19 Agosti, 2012; nililizungumza kwa urefu suala la kuilinda na kuiendeleza amani, utulivu na mshikamano wetu. Nilielezea kuwa mambo haya ndio siri kubwa ya mafanikio yetu tunayoendelea kuyapata.  Nilielezea ukweli kuhusu jamii yetu kwa kusema kuwa ni jamii ya watu waliochanganyika sana kwa mambo mbali mbali ya kijamii na katika maisha yetu ya kila siku.  Mwisho nilielezea kwamba katika siku za hivi karibuni nchi yetu imekabiliwa na vitisho vya kuondoka kwa amani, utulivu na mshikamano na niliyakumbusha matukio mawili makubwa. 
Tukio la kwanza ni lile la tarehe 26, 27 na 28 mwezi wa Mei na la pili ni lile la tarehe 20 Julai, 2012.  Nilisema wazi kwamba matukio haya yameitia doa jamii yetu na nchi yetu, ambayo imejijengea sifa nzuri ya amani na utulivu. Hatimae, nilitoa wito kwa kuwataka wananchi wote wajiepushe na vitendo vya uvunjaji wa amani na vinavyopelekea kuwaathiri watu na mali zao.  Nilisisitiza athari ya  vitendo hivi na shughuli zetu za maendeleo na ukuaji wa uchumi hasa katika kuimarisha sekta ya utalii na kuwakimbiza wageni wetu.
Ndugu Wananchi,
Takriban miezi miwili baada ya hotuba yangu hiyo, kwa mara nyengine tena, hapo tarehe 17 Oktoba limetokea tukio jengine la tatu la kusikitisha la kutaka kuivunja amani yetu. Maeneo mbali mbali ya mji wetu wa Zanzibar yalikumbwa na vitendo vya fujo na vurugu.
Taarifa rasmi ya Serikali iliyotolewa tarehe 17 Oktoba na 24 Oktoba na zile zilizotolewa na Jeshi la Polisi baina ya tarehe 17 hadi 19 Oktoba, kufuatia vitendo hivyo, zilielezea hatua za haraka zilizochukuliwa katika kurejesha hali ya amani.  Kadhalika, taarifa hizo zilielezea sababu za kutokea fujo na vurugu hizo, uharibifu, hasara na madhara yaliyojitokeza siku hiyo ya tarehe 17 Oktoba, 2012.
Fujo na vurugu hizo zilipelekea kuchomwa moto kwa maskani za CCM, kuvunjwa maduka, kuporwa kwa mali za watu na kuharibu miundombinu ya barabara na kadhalika.  Vile vile, fujo na vurugu hizo zilipelekea kuuliwa kwa askari wetu wa polisi wa kikosi cha FFU Namba F2105, Koplo Said Abdulrahman. Nawapa pole wafiwa, ndugu na jamaa wa marehemu, Mungu amlaze mahala pema Peponi.  Waliohusika kufanya fujo na vurugu hizo ilisadikiwa kuwa wafuasi wa Sheikh Farid Hadi, kiongozi wa UAMSHO, wakidai kuwa Sheikh wao haonekani na hivyo kudhania kuwa anashikiliwa na vyombo vya dola. Hata hivyo, madai hayo kama nyote mnavyojua hayakuwa ya kweli na yalikanushwa na Jeshi la Polisi. Na kwa hivyo vyombo vya dola havikumteka Sheikh Farid.
Ndugu Wananchi,
Napenda kukuhakikishieni wananchi nyote kwamba Serikali itaendelea kuchukua hatua madhubuti dhidi ya watakaotishia amani ya nchi yetu.  Jeshi letu la Polisi na vyombo vya Ulinzi na Usalama viko imara katika kuvidhibiti vitendo vya fujo na vurugu.  Serikali itafanya kila linalowezekana ili kuhakikisha kwamba wanaohatarisha usalama na amani yetu wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.  Tutazitumia sheria na taratibu ziliopo ili kuvishughulikia vitendo vya uvunjaji wa amani vitakavyofanywa au kuchochewa na kikundi chochote.  Hapana hata mtu mmoja alie juu ya sheria, kila mtu anapaswa kufuata sheria.
Nataka niwaeleze rasmin. Serikali haitowavumilia na kwamba ustahamilivu na uvumilivu wa Serikali umefikia kiwango cha mwisho. Hapa tulipofika basi tena. Ni jukumu letu sote tushirikiane na Serikali katika kuwakana na kutoa tamko zito kila mmoja wetu kwa vikundi hivyo.
Tutamshughulikia ipasavyo mtu yo yote yule atakaevunja sheria.
Nataka nirudie tena tutamshughulikia ipasavyo mtu yo yote atakaevunja sheria. Ustahamilivu na utulivu sio udhaifu ni heshima kubwa ya kutii amri ya MwenyeziMungu. Wanasema wazungu ‘enough is enough’.
Kama mjuavyo hivi sasa, hatua za kisheria zimeshaanza kuchukuliwa.  Viongozi wanane wa UAMSHO wamepelekwa mahakamani.  Wengine waliokamatwa na polisi kwa kufanya fujo nao pia wameshafikishwa mahakamani. Wakati huo huo, Jeshi letu la Polisi na vyombo vya Ulinzi na Usalama vinaendelea na doria katika mitaa mbali mbali ili kuhakikisha kuwa wananchi wanaishi kwa amani. Mali za watu na maisha yao yataendelea kulindwa. Wageni wetu wanahakikishiwa usalama wao na pia mazingira mazuri ya utalii yataendelea kuwepo.
Ndugu Wananchi,
Ninakuombeni sana kwamba nyote muendelee kuwa wastahamilivu na wenye subira ili kwa pamoja na Serikali yenu tuendelee kushirikiana katika kuidumisha amani katika nchi yetu.  Jeshi letu la Polisi na vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama vitaendelea kuimarisha ulinzi.  Kwa mara nyengine tena nawasihi wale wananchi wachache wenye nia ya kufanya fujo na vurugu, waache kujiingiza kwenye vitendo hivyo.  Kwani kufanya vitendo hivyo ni kufanya kosa kwa mujibu wa sheria na Serikali haitowavumilia kwani ina wajibu wa kusimamia sheria na kuwalinda wananchi wote.
Kwa dhati kabisa, ninakupongezeni wananchi wote kwa uvumilivu na ustahamilivu wenu. Kadhalika, ninalipongeza Jeshi letu la Polisi na vyombo vya Ulinzi na Usalama kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kuilinda amani ya nchi yetu.
Nachukua fursa hii kutoa pole kwa wananchi wote waliopoteza mali zao au kupata athari ya aina yo yote ile kutokana na fujo na vurugu hizo.
Ndugu Wananchi,
Kwa kumalizia nasaha zangu, napenda kuipongeza Kamati ya maandalizi kwa matayarisho na utaratibu mzuri wa sherehe hizi za Idd el Hajj.
Kwa namna ya pekee, napenda kuwashukuru wananchi wote  kwa ushirikiano wenu, ihsani, mapenzi makubwa na insafu mnayoionesha katika kuisherehekea sikukuu hii. Tumuombe Mwenyezi Mungu azidi kuulinda umoja wetu na atuwezeshe kuisherehekea Idd hii na nyengine kwa salama na amani. Atuzidishie neema za kila aina nchini mwetu na atujaaliye mvua zenye kheri na baraka ya mazao mengi.
Kwa baraka ya siku hii, Allah awajaaliye afya njema wagonjwa wetu na wazee wetu walioko majumbani na hospitalini. Tunamuomba Mwenyezi Mungu awape safari njema ya kurudi nyumbani mahujaji wetu na wakubaliwe Hijja yao na sisi aturejeshe majumbani kwa salama. Awarehemu na awasamehe makosa yao wazee, ndugu, jamaa na waislamu wote waliotangulia mbele ya haki. Awape malazi mema Peponi na sisi tulio hai atupe khatima njema na kwa pamoja tuwe miongoni mwa waja wake wema siku ya Kiama - Amin.
Nawasihi watumiaji wa vyombo vya barabarani kuchukua hadhari zaidi na kujali usalama.  Aidha, wazazi wawe waangalifu kwa watoto wao katika siku hizi za sikukuu.
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
Idd Mubarak
Kullu Aam Waantum Bikheir.

 




Imewekwa na MAPARA

No comments:

Post a Comment