WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, October 4, 2012

Taarifa rasmi: NIDA kuanza usajili Vitambulisho vya Kitaifa Zanzibar Oktoba 10


 

HOTUBA YA MKURUGENZI WA MAMLAKA YA VITAMBULISHO VYA TAIFA OFISI YA ZANZIBAR, KWA WAHARIRI NA WAANDISHI WA HABARI ZANZIBAR 03/10/2012

Picture

Mkurugenzi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa NIDA. Vuai Mussa Suleiman.

Ndugu Wahariri na waandishi wa habari
Maafisa toka Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA)
Mabibi na Mabwana,
Assalamu - alaykum

Utangulizi
Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, kwa kutuwezesha kukutana hapa tukiwa na afya njema katika kushirikishana hatua muhimu katika utekelezaji wa jambo muhimu la kihistoria katika mustakabali wa Nchi yetu, kwa kuanza mchakato wa usajili na Utambuzi wa watu, unaolenga hatimaye kutoa vitambulisho vya Taifa. 

Ni wazi wazo la kuwa na Vitambulisho vya Taifa limechukua muda mrefu sasa na kwa muda mrefu serikali imekuwa ikijitahidi kuhakikisha kuwa jambo hili linakamilika na mchakato unaanza. Na leo ndugu wanahabari, naomba kuwajulisha Usajili wa wananchi kwa upande wa Zanzibar unaanza rasmi 15/10/2012 baada ya kukamilika kwa usajili wa watumishi wa Umma. 

Kwa hakika tuna kila sababu ya kuipongeza serikali  ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa namna ya pekee, sekikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya Rais wetu Mheshimiwa Ali Mohamed Shein. Kwa hakika jitihada kubwa mlizozifanya kuhakikisha mradi huu unafanikiwa na kutekelezeka mnapaswa kupongezwa.

Ndugu Wanahabari,

Zanzibar tunakusudia kuanza shughuli ya usajili na utambuzi wa Watu rasmi kama hakutakuwa na mabadiliko yeyote tarehe 15/10/2012 na utaratibu tuliojiwekea ni kusajili kiwilaya na kila Wilaya imepangiwa siku 10 za usajili.

Ni imani yangu kubwa wananchi, Viongozi wa dini, masheha na wanasiasa kwa jumla, tutatoa ushirikiano kwa maafisa wetu wasajili ambao watakuwa katika kila shahia kufanya usajili, na kila mmoja wetu aone ana jukumu kubwa la kulipa kipaumbele suala hili kwani ni kwa maendeleo yetu na kwa mstakabali wa Taifa letu.

Ratiba ya wilaya itakayoanza mpaka kuhitimisha, tutaitoa katika vyombo vya habari ili kila mtu kufahamu ratiba yake na kujiandaa kwa usajili.

UNGUJA


WILAYA
TAREHE
WILAYA
TAREHE
WILAYA
TAREHE
Kusini
15–26/10/2012
Kati
29/10 – 09/11/2012
Magharibi
12 – 23/11/2012
Mjini
26/11 – 07/12/2012
Kask B
10 – 21/12/2012
Kask A
24/12/2012 – 04/01/2013

PEMBA
Mkoani
07 -18/01/2013
Micheweni
21/01 – 01/02/2013
Wete
04 – 15/02/2013
Chake Chake
18/02 – 01/03/2013

Vitambulisho hivi vitatolewa kwa makundi makuu matatu, wananchi kwa ambao ni raia, wageni na wakimbizi. Hapa kwetu Zanzibar tunaishi na wageni na hata wakimbizi. Rai yangu wote wajitokeze kujisajili kwa kufuata taratibu na sheria  za nchi, na tusikubali kupindisha sheria kutoa kitambulisho cha uraia kwa wageni kwani sote tunafahamu madhara yake, na umuhimu wa kila kundi kupewa kitambulisho chake kwa kadiri ya stahiki zake.

Ndugu zangu tukifanya makosa katika hili la kitambulisho tutajikuta nchi yetu kesho ikitawaliwa na wageni..tujifunze kwa yaliyotokea kwa wenzetu, Tanzania yasitukute.

Ndugu Wanahabari,

Zipo faida nyingi sana za kuwa na kitambulisho cha Taifa, kama ilivyo kwa kitambulisho cha Mzanzibari mkaazi.

Wengi wetu tutakuwa tukijiuliza mfumo huu wa Utambuzi na usajili wa watu utakuwa na faida gani kwetu kama Taifa na kama wazanzibari?

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikipata hasara nyingi kwa kushindwa kuwatambua watu wanaishio nchini kutokana na kutokuwa na mfumo wa utambuzi na usajili wa watu Kitaifa. Baadhi ya hasara hizo ni kama zifuatavyo:-

1.   Wananchi kuendelea kuwa katika umasikini kwa kushindwa kupata mikopo katika benki na  taasisi za fedha. Faida ya zoezi hili, ni kuwasaidia wananchikujikwamua kiuchumi. Aidha, baadhi ya benki zimekuwa zinatoza riba kubwa kufidia hasara wanayoipata kutokana na baadhi ya watu kutorudisha mikopo kwasababu hawatambuliki.

2.   Bodi ya mikopo ya wanafunzi wa Elimu ya Juu imekuwa inapata matatizo na malalamiko mengi kwa kushindwa kumtambua mwanafunzi yupi anastahili  mkopo na kwa kiasi gani. Aidha, urudishwaji wa mikopo hii umekuwa ni mgumu kwa kushindwa kuwapata wadaiwa mara baada ya kumaliza vyuo na hivyo kuingizia hasara Serikali. Sasa kitambulisho cha Taifa kitawezesha vijana wengi zaidi kupata mikopo ya elimu ya juu na hivyo kutoa fursa kwa vijana wengi zaidi kuendelea kimasomo

3.   Kuongezeka kwa vitendo vya uhalifu na hasa unaofanywa na raia kutoka nchi jirani na wafungwa waliomaliza adhabu zao au kuachiwa huru kwa msamaha waRais. Ni wazi kuwa udhibiti wao umekuwa mgumu kutokana na kushindwa kuwatambua.

4.   Kuongezeka kwa mrundikano wa wafungwa katika magereza mbalimbali kutokana na kutokuwepo kwa udhibiti wa wafungwa wa kifungo cha nje.

5.   Serikali imeendelea kubeba mzigo mkubwa wa gharama wakati wa zoezi la kupiga kura. Kwakuwa na kitambulisho cha Taifa, kutapunguza gharama kubwa za kuhuisha daftari la wapiga kura kila inapohitajika

6.   Serikali imekuwa inapoteza fedha nyingi kila mwaka kwa kulipa watumishi hewa katika mfumo wa mishahara ya watumishi wa Serikali. Sasa kwa kuwa na daftari lenye kumbukumbu sahihi za watu, serikali itadhibiti upotevu wa fedha nyingi ambazo wamekuwa wakilipwa watumishi hewa kwani hawatambuliki

7.   Pamoja na hayo, Serikali imekuwa inapata matatizo na kuingia migogoro na wananchi wakati wa mazoezi ya kuwalipa fidia kutokana na kuchukua ardhi au kubomolewa nyumba zao kwa sababu ya kushindwa kumtambua mmiliki sahihi na anachokimiliki.

8.   Mfumo huu pia utarahisisha na kuwawezesha vijana na watu wengi zaidi kuweza kumiliki hati ya kusafiria (Passport) tofauti na hali ilivyo sasa ambayo inalazimu mwombaji kuwa na vielelezo vingi kutokana na kutotambuana. Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeanzisha Mfumo huu wa Vitambulisho vya Taifa kwa sababu mbali mbali ikiwa ni pamoja na hizi zifuatazo:

1.   Kuweza kuwatambua raia na wageni waishio Tanzania.

2.   Kusaidia kumtambua mhusika anapohitaji kupatiwa huduma katika Taasisi mbalimbali kama vile benki, taasisi za mikopo na huduma za afya.

3.   Kumtambua mtu pale anapofanya uhalifu wa aina fulani. Jambo hili litasaidia sana katika kupambana na uhalifu.

4.   Kuwatambua wakwepaji wa kurejesha mikopo kutoka kwenye benki mbali mbali nchini.

5.   Kuweka kumbukumbu za matukio ya uhalifu katika daftari.

6.   Kumtambua mtu anapofanya biashara au shughuli nyingine kwa kutumia majina tofauti.
7.  Kuhakikisha kuwa mtu anapata stahili zake za jamii. Kwa mfano, kupata malipo ya pensheni, haki za matibabu, haki za kujiunga na masomo ikiwa ni pamoja na stahili zozote ambazo raia wa Tanzania anastahili.

8.   Kusaidia katika kuondoa watumishi hewa kwenye "payroll" ya Serikali.

9.  Kuimarisha utendaji kazi Serikalini kwa kuwa na kumbukumbu sahihi za watumishi na malipo ya stahili zao, hasa pale wanapostaafu.

10.  Kurahisisha zoezi la kuhesabu watu (sensa).
11.  Kurahisisha zoezi la kutengeneza daftari la wapiga kura.

12.  Kwakuwa kitambulisho hiki kitakuwa cha teknolojia ya hali ya juu yaani (smart Card) na kuweza kuhifadhi taarifa nyingi za mtu binafsi zikiwemo taarifa za kibailojia, Kitambulisho cha Taifa kitasaidia kutambua watu panapotokea majanga kama vile ajali n.k na kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa haraka.

Ndugu wanahabari,

Shughuli hii ni mtambuka kwa maana ina mgusa kila mtu kwa nafasi yake, hivyo sitegemea zoezi hili kuchukuliwa kuwa la kisiasa, kidini au kikabila, kwani lina linda maslahi ya kila mmoja wetu. Huu sasa ni wakati wa kujenga umoja wa Kitaifa. Na maamini Watanzania kwa hili tunaweza, na wazanzibari tutaonyesha mfano.

Rai kwa Wananchi wote

Napenda kuchukua fursa hii kuwaomba Wananchi  wote na wakazi wa Zanzibar mnaoishi kihalali  kujiandaa na kujitokeza katika shughuli hii kwa kuhakikisha kuwa wale wote wenye umri wa miaka 18 na zaidi wanaandaa na kutunza nyaraka zote muhimu zenye kumbukumbu zao binafsi ili kurahisisha ushiriki wao katika zoezi hili kama watakavyoelekezwa.

Vyombo vya habari tunawaomba ushiriki wenu wa karibu katika  kuhakikisha kuwa wananchi wanapata taarifa sahihi na kwa wakati ili wasipoteze fursa hii muhimu kwao ikiwa ni haki yao msingi kama raia.

Pia, napenda kutoa wito kwa Taasisi zote za serikali wakiwemo wadau wote muhimu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) ambao ni  RGO, ZAN-ID, UHAMIAJI na TAMISEMI tushirikiane kwa pamoja ili wananchi wote na wageni wanaoshi nchini kihalali kusajiliwa.

Mwisho NIDA inawahakikishia wananchi wote, usiri mkubwa wa taarifa zitakazotolewa na utunzaji wa taarifa hizo muhimu wakati wote wa zoezi hili, mpaka kupatokana kwa Vitambulisho.

Asanteni sana kunisikiliza.

Vuai Mussa Suleiman,
Mkurugenzi
Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa
Zanzibar.
03/10/2012


No comments:

Post a Comment