WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, October 11, 2012

Kauli Ya Awali Ya Waziri Kivuli Mambo Ya Ndani, Juu Ya Mauaji Ya Mwangosi


 

KAULI YA AWALI YA VINCENT NYERERE (MB) WAZIRI KIVULI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI KUHUSU RIPOTI YA UCHUNGUZI WA MAUAJI YA MWANDISHI WA HABARI WA CHANNEL TEN, DAUDI MWANGOSI.

 SERIKALI kupitia Kamati iliyoundwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dkt Emmanuel Nchimbi, na kutoa taarifa yake tarehe 9, Oktoba 2012, imetoa hadharani kwa umma kile ilichoita kuwa ni Ripoti ya Uchunguzi wa kifo cha Mwandishi wa Habari wa Channel Ten, Bw. Daudi Mwangosi ambayo imelenga kulisafisha Jeshi la Polisi.

Licha ya Ripoti hiyo kuacha maswali mengi yasiyokuwa na majibu hasa juu ya uwezo na umakini wa serikali hii ya CCM kupitia Waziri Nchimbi, ni kwamba waziri pia ameshindwa kuthamini na kusimamia haki ya kuishi kwa mujibu wa katiba ya nchi na ni ushahidi wa matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi. 

 Moja ya sababu kubwa inayonifanya nifikie hitimisho hilo ni kitendo cha Waziri Nchimbi kupokea ripoti hiyo mbovu, kuikubali, na kuitetea huku akijua kuwa polisi walihusika na mauaji hayo na hivyo ameamua kuwalinda kwa udhalimu waliofanya kwa kisingizio cha suala kuwa mahakamani. 

 Wizara ya Mambo ya Ndani ingeweza kabisa kutoa ripoti yote hadharani bila kuingilia kesi iliyoko mahakamani kwa kuwa taarifa hiyo haielekezi mahakama itoe hukumu gani bali ilipaswa kueleza matokeo ya uchunguzi wa chanzo cha mauaji ya kinyama na masuala mengine ya ukiukwaji wa sheria na haki za binadamu yaliyofanyika.

 Kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani nilitarajia ripoti hiyo ianike namna Jeshi la Polisi lilivyoingiliwa na viongozi waandamizi wa serikali na kutumiwa kisiasa kufanya operesheni zenye kuvunja sheria ya vyama vya siasa na kuweka bayana chanzo cha polisi kuamua kufanya mauaji ya kinyama ya mwanahabari Daud Mwagosi.

 Aidha, ripoti hiyo imeshindwa kueleza ukweli kuhusu matendo ya uvunjaji wa sheria yaliyofanywa na Kamanda wa Polisi Mkoa Iringa Michael Kamuhanda kutoa agizo kinyume cha sheria kusitisha shughuli halali za CHADEMA bila kuzingatia matakwa ya sheria ya vyama vya siasa.

 Kwa upande mwingine ripoti imekwepa kueleza ukweli kuwa Msajili wa Vyama vya Siasa John Tendwa kukiuka masharti ya sheria ya sensa, masuala ambayo ndiyo yaliyosababisha polisi kupewa amri ya kufanya operesheni iliyopelekea mauaji ya Mwanahabari Daud Mwangosi, kujeruhi raia wengine wasio na hatia na kusababisha uharibifu wa mali. 

Kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani nilitarajia kwamba pamoja na kueleza kwa ukweli chanzo cha mauaji, ripoti hiyo ingetoa mapendekezo ya wazi ya hatua za kisheria kuchukuliwa kwa wote waliovunja sheria na kusababisha mauaji na kuwajibishwa kwa mtandao mzima uliohusika na operesheni hizo zilizovunja haki za binadamu za kuishi na kujumuika pamoja na kukiuka misingi ya utawala bora bila kujali vyeo vyao katika Wizara ya Mambo ya Ndani pamoja na Jeshi la Polisi.

 Kutokana na Waziri kuonekana wazi kuwalinda na kuwatetea waliohusika na mauaji nalazimika kuamini kwamba Serikali haina nia ya dhati ya kupiga vita vitendo viovu vinavyofanywa na Jeshi la polisi dhidi ya raia hali ambayo inatoa picha kwamba vitendo hivyo vimesababishwa na maagizo kutoka kwa viongozi wengine waandamizi wa serikali na vyombo vya ulinzi na usalama. 

 Itakumbukwa kwamba wakati nikiwasilisha Maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Wizara ya Mambo ya Ndani katika mkutano wa nane wa Bunge mwaka huu, katika bunge la bajeti mwaka huu nilizuiliwa kusoma kipengele cha MAUAJI YA RAIA YENYE SURA YA KISIASA kwa kisingizio cha masuala kuwa mahakamani, hivyo bunge lilikoseshwa fursa ya kuisimamia serikali kuepusha hali hiyo kuendelea.

 Matokeo yake ni Wizara ya Mambo ya Ndani na Jeshi la Polisi kutokuwajibika na hatimaye kusababisha mauaji mengine yenye sura ya kisiasa katika Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Iringa mara baada ya mkutano huo wa Bunge.

 Katika muktadha huo, kutokana na kukithiri kwa matukio haya ya kigaidi ya kuteka, kutesa, na kuua raia wasio na hatia hapa nchini, na kutokana na kuundwa kwa kamati mbalimbali za uchunguzi na Wizara ya Mambo ya Ndani au na Jeshi la Polisi ambazo matokeo yake hayafanyiwi kazi au kamati hizo kutoa ripoti zenye kuficha ukweli; kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani:-

 Mosi; natoa mwito kwa Rais Jakaya Kikwete kumfukuza kazi Waziri wa Mambo ya Ndani Dr Emmauel Nchimbi kwa matumizi mabaya ya madaraka kwa kuruhusu ufujaji wa fedha za umma kufanya uchunguzi usiokidhi mahitaji na wenye kuficha ukweli na kulisafisha jeshi la polisi dhidi ya tuhuma za mauaji pamoja na kukwepa kueleza uvunjaji wa Sheria uliofanywa na Kamanda wa Polisi Michael Kamuhanda, Msajili wa vyama vya siasa John Tendwa na wote waliohusika kwa namna moja au nyingine kuvunja sheria, kusababisha mauaji na kukiuka haki za msingi za kikatiba.

 Aidha, Rais Kikwete aagize hatua za kisheria kuchukuliwa kwa mtandao mzima ulioshiriki katika kumpiga na hatimaye kusababisha mauaji ya Daudi Mwangosi. 

 Pili; kutokana tatizo hili la mauaji yenye sura ya kisiasa kuendelezwa bila Serikali kuonesha kukerwa nalo na kuchukua hatua madhubuti za kukomesa ugaidi huu; nitapeleka ripoti zote tatu za uchunguzi wa kifo cha Mwangosi, yaani Kamati ya iliyoundwa na Waziri Nchimbi, Baraza la Habari Tanzania (MCT) na Tume ya Haki za Binadamu kwa Baraza Kivuli la Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kuzijadili na kufanya maamuzi kwa ajili ya hatua za ziada za kibunge kuchukuliwa. 

Imetolewa tarehe 11 Oktoba 2012 na: Vicent Nyerere (Mb) Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani

No comments:

Post a Comment