WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Monday, October 1, 2012

Wassira sasa amlipua Slaa *Amtaka aache kuita wake za watu chumbani *Dovutwa: CHADEMA inamuogopa Lowassa



Na Mwandishi Wetu, Bunda na Dar

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Bw. Stephen Wassira, amesema watoto wa kaka yake ambao juzi walitangaza kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bi. Lilian na Bi. Esther Wassira, wana haki ya kujiunga na chama chochote cha siasa.


Alisema kitendo cha Katibu Mkuu wa chama hicho Dkt. Willibrod  Slaa kutumia jina na cheo chake wakati akiwapa kadi wanachama hao ni upotoshaji unaofanywa na CHADEMA ili kujipatia umaarufu.


Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Bunda, mkoani Mara, Bw. Wassira alimshukia Dkt. Slaa na kumtaka awe makini kuwaita wake za watu chumbani na kuwapa kadi bila maofisa wengine wa chama hicho kushuhudia tukio hilo.

Namhadharisha Dkt. Slaa kwani alichokifanya kinaweza kuleta mtafaruku katika ndoa za watu, Lilian na Esther ni watoto wa kaka yangu George Wassira si mimi, hawa ni watu wazima na wote wana haki ya kuchagua chama wanachokitaka,” alisema.

Aliongeza kuwa, Dkt, Slaa anaishi kwa kutafuta matukio bila kutumia akili ambapo mume wa Bi. Lilian ni mwanachama wa CHADEMA hivyo uamuzi aliochukua mkewe hauna uhusiano wowote na ukoo wao.

“Hata Makongoro Nyerere awliwahi kujiunga NCCR-Magezui wakati hayati Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere (baba yake), akiwa hai, je, tatizo lilikuwa wapi na yeye ni mtu mzima,” alisema.

Alisema siku zote Dkt. Slaa na viongozi wengine wa CHADEMA wamekuwa wakichukizwa na jinsi anavyojibu hoja zao hivyo wanachokifanya ni kumtafutia tuhuma lakini wameshindwa kufanikiwa hivyo wamezna kuwachonganisha katika ukoo.

“Wanachukizwa ninavyojibu mambo yao hasa wanayosema katika majukwaa na kuhatarisha amani, mimi ni mzalendo wa kweli ambaye nalitumikia Taifa lengu kikamilifu na sina tuhuma za ufisadi ambao Dkt. Slaa ameufanya kuwa wimbo,” alisema.

Hata hivyo, aliwataka Watanzania waelewe kuwa ukoo wao msingi wake si vyama vya siasa bali kila mtu ana haki ya kuingia na kutoka katika chama chochote.

Alisema kitendo cha Dkt. Slaa kuhusisha ukoo huo na tukio la watoto hao kujiunga CHADEMA ni kuwadanganya Watanzania kuwa ukoo huo umegawanyika jambo ambalo si kweli.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha United Peoples Democratic Party (UPDP) Taifa, Bw. Fahmi Dovutwa, naye amemshukia Dkt. Slaa kutokana na kauli yake kuwa CCM kinakufa.

Bw. Dovutwa aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema hivi karibuni, gazeti moja (si Majira), lilimnukuu Dkt. Slaa akisema CCM kimeonesha kila dalili ya kufa baada ya kushindwa kuwaengua wagombea wawili (aliowaita watuhumiwa wa ufisadi), katika nafasi walizowania ndani ya chama hicho. 

Wagombea hao ni Mbunge wa Bariadi Magharibi, Bw. Andrew Chenge ambaye amepitishwa kuwania ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Wilaya ya Bariadi, mkoani Simiyu.

Mwingine ni Waziri Mkuu aliyejiuzulu Bw. Edward Lowassa, ambaye chama chake kimempitisha kuwania ujumbe wa NEC, Wilaya ya Monduli, mkoani Manyara.

Kauli ya Dkt. Slaa imenishangaza na imevitia doa vyama vya upinzani, yeye hakupaswa kuihadarisha CCM ili isianguke katika Uchaguzi Mkuu 2015, nilitegemea afurahie chama tawala kianguke ili CHADEMA kiingie Ikulu.

“Kutokana na kauli yake, inaonesha CHADEMA kinamuogopa Bw. Lowassa ambaye kama ataamua kugombea Urais 2015, Dkt. Slaa anaamini chama chake hakitafurukuta,” alisema.

Alisema Dkt. Slaa aliamua kuondoka CCM mwaka 1995 na kuhamia CHADEMA ili akajifariji baada ya jina lake kuenguliwa katika kura za maoni mwaka hivyo bado ana mapenzi na chama tawala ndio maana anawajibika kukipa ushauri.

“Ni wazi kuwa Dkt. Slaa hajui chochote kuhusu haki za binadamu kwani katiba ya nchi ya mwaka 1977 ibara ya 13 (6) (b), inasema ni marufuku kwa mtu aliyeshtakiwa kwa kosa la jinai kutendewa kama mtu mwenye kosa hadi itakapothititika kuwa anayo hatia ya kutenda kosa hilo,” alisema Bw. Dovutwa.

Alisema kwa mujibu wa kifungo hicho pamoja na Dkt. Slaa kuwataja mafisadi katika Viwanja vya Mwembe Yanga, Dar es Salaam, hapaswi kuendeleza tuhuma dhidi yao kwani yeye si polisi, Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI), wala mahakama.

Bw. Dovutwa alisema inaonesha baada Dkt. Slaa kutoa tuhuma hizo, yeye ndie aliyefanya uchunguzi, kuandaa kesi na kuwatia hatiani.

“Madai ya Dkt. Slaa kuwa kabla hajaondoka bungeni alimwambia Bw. Lowassa kwamba kwa vile amejiuzulu Uwaziri Mkuu kwa madai ya kuwajibika, ina maana alikuwa anamjua aliyesababisha achukue uamuzi huo hivyo alimtaja amtaje ili wamsafishe na kushindwa kumtaja ni siasa za kutishiana ambazo hazina tija.

“Kwa kauli hiyo, baada ya Bw. Lowessa kukataa kumtaja, anachokifanya Dkt. Slaa ni siasa za chuki ambazo haziwezi kukubalika hata kidogo kwa masilahi yake,” alisema.

Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu ili kujibu madai hayo, Dkt. Slaa aliangua na kusema kuwa “ Mimi sitaki kujibu, waulize waliokuwepo wakueleza kama tulikuwepo peke yetu”.

Wewe ulikuwepo? alihoji Dkt. Slaa akimuuliza mwandishi wa wetu na baada ya kujibiwa hakuwepo, alisema atafutwe aliyekuwepo ili azungumzie ukweli wa madai hayo.

Akizungumzia madai ya Bw. Duvutwa, alisema kiongozi huyo wa UPDP si saizi yake. “Siwezi kujibizana na mtu ambaye hana hata Mwenyekiti mmoja wa mtaa...nijibizane naye nini? kibinadamu sina sababu ya kumjibu,” alisema Dkt. Slaa.


Majira

No comments:

Post a Comment