WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, March 14, 2014

Wanawake Bunge la Katiba piganieni haki za msingi siyo madaraka`


Marchi 4,  mwaka huu, ni siku ambayo wanawake ambao ni wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba, walisimama ndani ya ukumbi huo na kuimba wimbo wa 'tunataka haki zetu' wakitaka uwepo wa uwiano wa nafasi za uongozi katika kuongoza Bunge hilo.
Ilikuwa ni mpambano kati ya wanaume na wanawake, huku wanaume wakitaka usawa huo ujikite katika sifa na uwezo ili kukidhi matakwa ya demokrasia na si kwa sababu ya jinsia ya mtu.

Mjadala huo uliibuka wakati wa kujadili vifungu vya kanuni za kuongoza Bunge hilo.

Kifungu cha 23 fasili ya pili ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kinaeleza namna mwenyekiti na makamu wake watakavyochaguliwa.

Kifungu cha 23 (2) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura ya 83, inaeleza kuwa mwenyekiti na makamu wake wa watachaguliwa kutoka miongoni mwa wajumbe wa Bunge Maalum kwa misingi kwamba endapo Mwenyekiti anatoka upande mmoja wa Jamhuri ya Muungano basi Makamu Mwenyekiti atakuwa mtu anayetoka upande mwingine wa Jamhuri ya Muungano.

Sheria hiyo imetaja uwiano wa pande za Muungano, na kukosa uwiano wa kijinsia na wanawake waliopo kwenye ukumbi huo walipinga vikali na kutaka kuwe na uwiano wa kijinsia kwenye nafasi zote za uongozi wa Bunge hilo.

Wakati wanawake hao wakipingana vikali kutaka usawa kwenye uongozi, hao hao baadhi walishindwa kumuunga mkono mwanamke pekee aliyegombea nafasi ya Mwenyekiti wa Muda, Margreth Rwebangira, akiwa ni kati ya wagombe watatu wa nafasi hiyo.

Bunge hilo lina wajumbe wanawake zaidi ya 250, lakini mwanamke mwenzao aliambulia kura 84 pekee zikiwa zimejumuisha wanawake na wanaume.

Wachambuzi wa msuala ya kisiasa na jinsia wanatafsiri mchakato huo kama unafiki miongoni mwa wanawake unaowafanya kuendeleza usemi wa kuwa adui wa mwanamke ni mwanamke mwenyewe.

Walikuwa na nafasi ya kumuwezesha Rebangira kuongoza Bunge hilo na kuweka historia, lakini walishindwa kufanya hivyo.

Cha msingi wanachopaswa wanawake kupigania ni masuala muhim u yanayowahusu ili yaingizwe katika Katiba Mpya na siyo ya kutaka kuwekwa katika nafasi za uongozi.

Kwa mfano, kuna masuala ya wanawake kurithi mali, kubaguliwa katika kupata ardhi, kupigwa pamoja na  wasichana kupata mimba na kufukuzwa shule.

Masuala hayo wanawake ambao ni wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba walipaswa kuyapigania zaidi, na sio kutaka wachaguliwe katika nafasi za uongozi, ambazo kiuhalisia hazimsaidii mwanamke aliyopo vijijini.

Lazima wanawake wapiganie vitu ambavyo vinawasaidia wanawake wote hapa nchini, lakini waking'ang'ania kupatiwa nafasi za uongozi badao wanaendeleza ubinafsi na kuwanyia wanawake wenzao wanaowawakilisha huko bungeni.

Mara zote wanawake waliokuwepo kwenye ukumbi huo walilipuka kwa kelele kupinga kifungu chochote cha uongozi wa Bunge hilo kutotambua usawa wa jinsia.

Mjumbe wa Kamati ya kumshauri Mwenyekiti wa muda, Rwebangira, alifafanua kuwa uwepo wa usawa wa pande za muungano unatosheleza kwa kuwa ni vigumu kuweka usawa mwingine kwa kuwa kimahesabu haikai sawa.

Mjumbe wa Kamati hiyo, Tulia Ackson, anasema ni vigumu kuwa na uwiano wa aina mbili kwa kuwa upande ambao utatoa jinsia fulani utalazimika kutoa nafasi hiyo kwa mtu wa jinsia nyingine na hivyo kutokuwa sawa.

Mjumbe Eva-Maria Semakafu, anataka Bunge hilo kutenda haki kwa wanawake kwa kuwa Bunge linaundwa na jinsia zote mbili na Katiba inayotengenezwa ni ya wanawake na wanaume.

Anasema uteuzi wa wajumbe wa Bunge hilo ulizingatia usawa wa kijinsia, pande za Muungano, hivyo ni lazima sheria ikatamka uwepo wa usawa wa kijinsia kwenye uongozi.

Dk. Asha-Rose Migiro, anasema Sheria ya Mabadiliko ya Katiba imesema Mwenyekiti akitoka upande mmoja, Makamu wake anatoka upande mwingine na haijakataza kuzingatia matakwa ya jinsia.

"Kwa maana hiyo, waheshimiwa wajumbe mkikubali na mkaridhia inawezekana kabisa kanuni hii kubeba kionjo hicho bila ya kukiuka sheria, naomba kutoa rai wajumbe wa kiume na wa kike tuungane katika suala hili ili tuweze kuweka kipengele hicho...na kama ninanusa vizuri nadhani tunakwenda vizuri," anasema huku akishangiliwa na wajumbe.

Hali ilikuwa tofauti pale, Mjumbe Ezekia Wenje, aliposema nafasi za uongozi zisiangaliwe kwa usawa wa kijinsia pekee bali kwa uwezo wa mtu wa kielimu na uongozi kwa kuwa ndiyo mahitaji ya demokrasia.

Anna Abdallah ambaye ni Mbunge wa Bunge la Jamhuri, alibadili hali ya hewa ukumbini baada ya kuwaeleza kwamba  wabunge waliopitisha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ndiyo walikosea kwa kuwa walishindwa kutetea sheria kutamka usawa wa kijinsia.


Anasema wabunge wa Bunge la Jamhuri ambao ndiyo walitunga sheria hizo walikuwa na mamalaka ya kuingiza kionjo hicho, lakini hawakufanya hivyo na mwishowe sheria kutamka usawa wa pande za Muungano pekee.

Mwanasiasa huyo anasema wanawake wa Bunge la Jamhuri ndiyo wa kulaumiwa kwa kuwa walikuwa na nafasi ya kupigania hilo na kwa hatua iliyopo huwezi kutunga kanuni inayokidhana na sheria, hivyo kinachotakiwa kuweza kufikia muafaka ni maridhiano ya pande zote.

"Tunachopaswa kufanya hapa ni maridhiano kwa kuwa tulikosea tangu mwanzo, kuwa iwapo Mwenyekiti wa kudumu atakuwa mwanaume basi makamu awe mwanamke, na hiyo hivyo kwenye Kamati 12 za kujadili Rasimu ya Katiba," alifafanua.

 
CHANZO: NIPASHE: Na Salome Kitomary

No comments:

Post a Comment