WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, March 14, 2014

Profesa Mahalu: Nimetua mzigo mzito



Dodoma. Huwezi kuzungumzia mafanikio ya Bunge Maalumu la Katiba bila kumtaja aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kupitia Kanuni za Uendeshaji wake, Profesa Costa Mahalu.
Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya gazeti hili na profesa huyo.
Mwananchi: Nini siri ya mafanikio yako katika kuiongoza Kamati ya Kanuni tena kwenye kipindi cha misukosuko mingi ya kikanuni?
 Profesa Mahalu: Siri ya mafanikio yangu ni Mungu. Nilimwomba Mungu ili aniwezeshe kuongoza kamati yenye mchanganyiko wa wajumbe kutoka makundi mbalimbali. Pia siri yetu ya mafanikio ni ‘teamwork’(kufanya kazi kwa pamoja) tumefanya kazi kama timu. Baadhi ya wajumbe ninawafahamu vizuri na wengine siwafahamu lakini Mungu mwema, tumekuwa kitu kimoja.
 Tuliazimia wote kuwa kitu kimoja na kiukweli tumeweka rekodi kubwa duniani ya kumaliza kazi ya kutayarisha kanuni za Bunge la Katiba kwa majuma matatu. Nchi nyingine zilitumia mpaka miaka kutengeneza kanuni tu.
Nafurahia umoja wetu na ninaamini hautaishia kwenye mchakato wa Katiba pekee.
Mwananchi: Kitu gani kilikukera zaidi wakati wa mchakato huo wa kutengeneza kanuni?
 Profesa Mahalu: Mimi ni mfuasi wa dhana ya saba mara sabini. Inawezekana kabisa lugha zilipishana lakini tayari nimesamehe na naamini hata wajumbe wameisamehe kamati yangu.
Mwananchi: Kipi ulikipenda sana katika kazi ile ya kutengeneza kanuni?
 Profesa Mahalu: Nilipenda sana ushirikiano niliupata kutoka kwa wajumbe wenzangu wa kamati. Mwanzoni niliogopa kufanya kazi na watu ambao nilijua wana masilahi tofauti. Lakini kadiri muda ulivyosonga, nikagundua kuwa wote ni wamoja, labda ni kwa sababu wote tumetoka kwenye taaluma moja ya sheria.
 Mwananchi: Nini maoni yako kuhusu kanuni ya 37 na 38 zinazozungumzia aina ya kura ambazo kamati yako ilishindwa kufikia mwafaka?
Profesa Mahalu: Ukiangalia kwa jicho la sheria hakuna utata wa ufafanuzi. Kura ya siri au ya wazi zote ni kura katika mchakato wa kidemokrasia. Lakini  hilo ni suala ambalo kamati haiwezi kufanyia uamuzi kwa kuwa bado watu wanavutana. Natoa wito kwa wajumbe wa kamati, kuliangalia suala hilo kwa makini ili lisitupotezee muda.
Mwananchi: Unakumbuka kusukumwa na kikundi chochote ambacho labda kilitaka masilahi yake yaingizwe kwenye kanuni wakati wa kuandaa kanuni hizo?
 Profesa Mahalu:  Hakuna kikundi kilichotushawishi kwa namna yoyote ile. Tulifanya kazi yetu kwa uhuru, weledi na amani kubwa. Nina hakika tumevunja rekodi ya dunia katika kutengeneza Rasimu ya Kanuni kwa muda mfupi.
Mwananchi: Una maoni gani kuhusu tofauti za kimtazamo zinazojitokeza kwenye mchakato huo wa Bunge la Katiba?
Profesa Mahalu: Tofauti za kimtazamo ni msingi wa demokrasia na sheria inatambua hilo. Ila katika mchakato muhimu kama huu wa kutengeneza Katiba, lazima wanaopingana kimtazamo wafikie mwafaka.
Mwananchi: Unatoa wito gani kwa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba?
 Profesa Mahalu: Wito wangu ni kuwataka tushirikiane katika kazi hii ya kihistoria. Tuache tofauti zetu za kiitikadi tumwangalie Mungu na waja wake, raia wa Tanzania.
Nawakumbusha wenzangu kwamba Katiba tunayoitengeneza siyo mali yetu, ni mali ya watoto na wajukuu wetu. Mungu aliondolee Taifa letu ubinafsi, ili tuwe pamoja katika mchakato huu wa kihistoria.
Historia yake
Profesa Mahalu alizaliwa Julai 9, 1948 katika Kijiji Cha Katunguru wilayani Sengerema katika Mkoa wa Geita.
 Zamani eneo hilo lilikuwa likijulikana kama Wilaya ya Geita.
 Baada ya kumaliza elimu ya msingi katika Shule ya Msingi Geita, Profesa Mahalu alijiunga na masomo ya sekondari katika Shule ya Sekondari  Kibaha, mkoani Pwani ambako alimaliza kidato cha nne, kabla ya kujiunga na masomo ya kidato cha tano katika Shule ya Sekondari ya Mkwawa.
 Mwaka 1971 alijiunga na mafunzo ya jeshi katika Kambi ya Makutupora, mkoani Dodoma na baadaye mwaka 1974 alijiiunga na masomo ya Shahada ya Kwanza ya Sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Mwaka 1975, aliajiriwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kama Mkufunzi Msaidizi katika Kitengo cha Sheria kabla hajaanza masomo yake ya Shahada ya pili ya sheria kati ya mwaka 1976 na 1978 huku akiendelea kufundisha.
Mwaka 1979 alikwenda Hamburg, Ujerumani Magharibi ambako alisomea na kuhitimu udaktari wa sheria mwaka 1983. 
Alirudi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kuendelea na kazi yake kama Mhadhiri Mwandamizi.
“Baadaye nikawa Mkuu wa Kitivo cha Sheria wakati tayari nikiwa Profesa mshiriki. Mwaka 1990, nilikwenda Ujerumani kufundisha na mwaka 1991 nilirudi tena Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kama Profesa wa Sheria, nikafanya kazi kwa muda wa mwaka mmoja na nusu, kabla sijateuliwa kuwa Mkurugenzi wa Elimu ya Juu mwaka 1992 hadi 1996,” alisema Profesa Mahalu na kuongeza; 
“Mwezi Oktoba, mwaka huo huo 1996, nilihamishiwa katika Wizara ya Mambo ya Nje na baadaye nikapelekwa Ujerumani kuwa msaidizi wa balozi mwaka 1997. Mwaka 1999 niliteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia,  kazi ambayo niliifanya kuanzia mwaka 2000 hadi 2006.”
Kwa sasa Profesa Mahalu ni Mhadhiri wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine mkoani Mwanza. 
Katika maisha anaamini katika kumcha Mungu na kuwa muwazi.

source: mwananchi

No comments:

Post a Comment