WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Tuesday, March 4, 2014

Kura ya ndiyo, siri bado mwiba bungeni

Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba wakiwa ndani ya ukumbi wa Bunge hilo mjini Dodoma.
Bunge Maalum la Katiba limeendelea kugawanyika kutokana na wajumbe kutoafikiana kuhusu utaratibu wa kupitisha vifungu vya Rasimu ya Kanuni za Bunge hilo, huku Mwenyekiti wa Muda, Pandu Ameir Kificho, akitaka rasimu hiyo ipitishwe kwa kuhojiwa kwa uwazi wanaosema ‘ndiyo au hapa.’
Hali hiyo ilianza kujitokeza jana asubuhi baada ya Kificho kuwaeleza wajumbe kuhusu utaratibu utakaotumika kuboresha Rasimu ya Kanuni hiyo.

Akiwa amechelewa kwa muda wa dakika 45 wakati lilitakiwa kuanza saa 4:00, Kificho alisema: “Tumechelewa kuanza kwa sababu tulikuwa na kikao na Mwenyekiti wa Kamati ya Kumshauri Mwenyekiti wa Muda kuhusu Rasimu ya Kanuni za Bunge Maalum, Profesa Costa Ricky Mahalu.”

Pia alisema: “Tulichokubaliana na Mwenyekiti wa Kamati, twende sura kwa sura ili tupate mwelekeo panapohitaji marekebisho yawekwe vizuri kwa kuchapishwa au kuandikwa kwa mkono...wenye marekebisho wayaandike na kuyawasilisha kwa kamati kabla ya saa 7:00 na kamati itayawasilisha kwenye semina hii saa 11:00 jioni (jana).

“Unapofanya kazi ambazo hazina utaratibu (kanuni) lazima ufikiri utaratibu utakaofaa kutumika, baada ya kujadiliana na Profesa tumeona utaratibu huu unafaa kutupitisha eneo hilo na pia yakizungumziwa humu bungeni yatachukuliwa kwenye hansard kwa ajili ya kumbukumbu.”

Alisema wakirejea saa 11 jioni (jana) watapitisha marekebisho na vifungu vya rasimu hiyo.

SENDEKA

Baada ya Kificho kutoa utaratibu huo, Mjumbe Christopher Ole Sendeka, aliunga mkono utaratibu uliotolewa na Mwenyekiti wa kuwapa muda wajumbe kuandika marekebisho na kuyawasilisha kwa wakati aliosema kwani utaweka utaratibu mzuri na kutopoteza muda.

“Vinginevyo kila mjumbe akitaka kuzungumza hapa akisema ondoa kifungu hiki na weka hivi na wajumbe wakiwa zaidi ya 50 wakaomba kutoa maoni katika kifungu kimoja tutakaa hapa bila kumaliza,” alisema.

Akizungumzia kuhusu Ole Sendeka, Kificho alisema alichofanya mjumbe huyo ni kuunga mkono wazo lililotolewa awali la kuwataka wajumbe wawasilishe mapendekezo yao kimaandishi, vinginevyo itakuwa ngumu kufikia mwafaka.

KAWAWA
Kwa upande wake, Vita Kawawa, alisema wiki iliyopita wachangiaji walitoa mapendekezo ya vifungu mbalimbali na kamati ilitolea ufafanuzi vifungu vyenye maelezo makubwa tu  lakini haikutoa ufafanuzi kwa mawazo ya watu wachache.

“Majumuisho yaliyotolewa kwenye kamati yalikuwa ni akidi, kura za siri au wazi, hoja kinzani, uwasilishaji na matokeo, hivyo tunaomba kamati izingatie sana mawazo ya vifungu vya wachache,” alisema.

MANYANYA
Mjumbe mwingine, Stella Manyanya, alisema kuna baadhi ya mambo ambayo yalitolewa ufafanuzi vizuri na kamati ya Profesa Mahalu wiki iliyopo na wajumbe baadhi waliyapokea kwa mtazamo chanya.

“Lakini tulipowaomba waende wakatuandike tumekuja kuona kuna mambo tofauti kabisa ya vile ambavyo walikuwa wametolea ufafanuzi. Sasa mimi naanza kupata wasiwasi na kamati yenyewe,” alisema na kuongeza:

“Tunataka tupate nakala za hansard ili tufanye ulinganisho wa yale yaliyochangiwa bungeni na rasimu hii,” alisema Manyanya.

Hata hivyo, Mwenyekiti Kificho alisema mjumbe ambaye ameona kwamba hoja yake imeripotiwa tofauti kwenye rasimu hiyo basi anaweza kuomba nakala ya hansard na siyo kwa wajumbe wote.

MWIJAGE
Charles Mwijage, aliunga mkono pendekezo la kuwataka wajumbe wawasilishe mapendekezo yao kimaandishi, lakini alishauri kwamba wafanye hivyo ukurasa hadi ukurasa.

OLUOCHI NA DOVUTWA
Wajumbe Fahmi Dovutwa na Ezekile Oluochi, walitaka kamati izingatie hoja za makundi ya watu wachache ili sauti zao ziweze kusikika.

Walisema kwa muda mrefu makundi hayo hayajasikika.

NZEMBA
Mjumbe kutoka kundi la watu wenye ulemavu, Vinvent Nzemba, alisema kamati iwahakikishie yale watakayoyawasilisha kimaandishi kama taarifa zao zitajumuishwa kwani awali walifanya hivyo, lakini hazijajumuishwa.

DK. MICHAEL

Dk. Francis Michael, aliunga  mkono mawazo ya Sendeka na Oluochi  ya kuwasilisha mapendekezo yao ukurasa kwa ukurasa wa Rasimu ya Kanuni, lakini akataka kujua namna gani wanaweza kupiga kura.

“Napenda tujue hapa tutakapofika kwenye kupiga kura tunafanyaje, tumekuwa tukizungumza uwazi na siri kwa siku nzima, hivyo ni vema tukalimaliza hapa kabla hatujatoka,” alisema.

GHASIA
Mjumbe Hawa Ghasia alimtaka Mwenyekiti kuahirisha kikao hadi jioni ili wajumbe wapate muda wa kuandika marekebisho yao na kuyawasilisha.

“Uturuhusu kupata muda, vinginevyo hatutafikia mwafaka hapa bila kuandika, huo ndio utaratibu wa Bunge,” alisema.

ADHARI YA KIFICHO
Mwenyekiti Kificho alisema: “Unaipitishaje rasimu. Ili iwezekane kuifanya practically (kwa vitendo) mimi nitawauliza, "kifungu hicho kimeafikiwa, nanyi mtajibu ndiyo au hapa.”

“Lile la uwazi au siri tukitaka lianze kwenye rasimu hii hatutafika. Nataka rasimu ile (Rasimu ya Katiba) ndiyo tuanze. Tuliangalie kiutendaji wake, hili jambo hili mnalolizungumza lina uzito mkubwa sana,” alisema na kuongeza:

“Vipo vifungu 87 katika rasimu hii, sasa niwaambie makatibu watayarishe karatasi za kura kwa wajumbe 600 kwa kila kifungu ni kazi kubwa sana.”

LIPUMBA

Profesa Lipumba, alisema dhamira ya kura ya wazi au ya siri ni muhimu sana na wanatakiwa kufikia mwafaka kwanza kuhusu dhamira hiyo.

Alinukuu kifungu cha 4 cha Rasimu ya Kanuni za Bunge Maalum kinachozungumzia uhuru wa mawazo na maoni katika mijadala ya Bunge Maalum.

Pia alisema kifungu hicho kinataka kila mjumbe wa bunge hilo kutekeleza majukumu yake kwa uhuru na hatashurutishwa na kwamba hatashinikizwa wala kupokea maelekezo kutoka kwa mtu au chombo chochote.

Lakini, alisema kwa hali ilivyo bungeni humo imekuwa tofauti na akataka suala la kura ya siri au uwazi ni jambo la msingi katika kupitisha vifungu.

“Haiwezekani suala kwamba tunapigaje kura lipitishwe kwa kuulizwa wabunge, je,  mmekubali au ama hamkubali.  Ni jambo la msingi lipitishwe kwa maridhiano ya kidemokrasia,” alisema na kuongeza:

“Misingi ya kidemokrasia inaweza kuwalinda watu wanaodhani kwamba kutakuwa na vitisho.”

“Utaratibu wa kidemokrasia ni kuwa na kura ya siri inayoonyesha dhamira ya kila mjumbe,” alisema na kuongeza: “Hali imeonyesha tayari kuna shurutisho kwa maelekezo ya kichama.”
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment