WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Saturday, March 8, 2014

Historia itamhukumu vipi Rais Kikwete kuhusu Katiba Mpya?




BUNGE Maalumu la Katiba ndio limeanza na kwa karibu miezi mitatu hivi tutashuhudia malumbano, mabishano, michango na mijadala motomoto na mingine iliyopoa wakati wajumbe wa Bunge hilo watakapokuwa wanapitia ibara na vifungu mbalimbali vya rasimu ya Katiba Mpya. Mwishowe, watawaletea Watanzania Katiba inayopendekezwa ili wao wachukue uamuzi wa kuikubali au kuikataa. Na endapo wataikubali basi Tanzania itakuwa na Katiba Mpya miezi michache tu ijayo. Endapo hata hivyo Watanzania wataamua kuikataa basi Katiba ya sasa itaendelea kutumika.

Katika mchakato mzima hakuna mtu ambaye ameweka hadhi, heshima, jina, ujiko na sifa yake rehani kama Rais Kikwete. Vyovyote utakavyokwisha mchakato huu, Rais Kikwete ama atakumbukwa kwa kuwaachia Watanzania Katiba Mpya ambayo itadumisha taifa au anaweza kujikuta jina lake linatajwa katika historia kama kiongozi ambaye kutokana na uamuzi wake alisababisha taifa la Tanzania kufa.

Kikwete kama Gorbachev?
Muungano wa Jamhuri za Kisoshalisti za Kisovieti za Urusi (USSR) ulipata Rais wake wa mwisho chini ya Muungano huo, ambaye kutokana na uamuzi wake alisababisha (au alichangia kwa kiasi kikubwa) kuvunjika kwa Muungano huo. Huyo si mwingine bali ni Mikhail Gorbachev (83). Kuna watu wanamuona Gorbachev kama shujaa na wengine wanaona kama mtu aliyevunja sifa na taifa la Urusi kwa kuleta yale mabadiliko makubwa ya kimfumo, utawala, kisiasa na kiuchumi.

Lakini kubwa zaidi ni kuwa ilikuwa chini yake Urusi iliyokuwa taifa kubwa na lenye nguvu duniani ilivunjika na kusababisha kuzaliwa kwa mataifa mengine madogo na pia kusababisha mivurugano na hata vita katika zilizokuwa jamhuri za kisovieti. Kile kilichokuwa nia “njema” ya kuleta mabadiliko ili kuwaingiza Warusi katika ulimwengu wa kisasa wa demokrasia kilienda na uzuri wake na ubaya wake.

Kikwete asipoangalia – na sijui kama kuna namna ya kubadili – kuna uwezekano kabisa kuwa mwisho wa mchakato huu wa Katiba ama Tanzania itakuwepo au atajikuta amesababisha mvurugano mkubwa sana baina ya watoto wa taifa hili na yeye kama Gorbachev akijikuta anabakia kupewa tuzo, kusifiwa duniani na kuishia kualikwa kutoa hotuba za kuelezea “mafanikio” yake.

Mchakato huu ni uamuzi wa Kikwete
Ni vizuri kukumbuka kuwa mchakato huu wa Katiba ulianzishwa na Rais Kikwete peke yake; hakukuwa na kikao chochote cha kiserikali au chama ambacho kilipitisha uamuzi huu. Yawezekana alishauriana na watu wachache lakini hakuna ushahidi wowote kuwa ulikuwa ni uamuzi wa kisera wa chama chake au serikali yake. Ni kana kwamba aliamka usiku mmoja na kuamua kuwa ni bora awapatie wananchi Katiba Mpya kabla ya kuondoka. Uamuzi huu unaweza ukaandikwa kama uamuzi wa kijasiri zaidi au mojawapo ya uamuzi wa kibabe uliowahi kuchukuliwa na viongozi wetu.

Kikwete hakuwa na madaraka ya kuanzisha mchakato wa Katiba Mpya, mojawapo ya mambo ambayo labda wanafunzi wetu wa sheria itabidi waje kujifunza ni kuhusu madaraka ya Rais (Presidential Powers) na mambo yale ambayo Rais pekee anaweza kuyafanya (Presidential prerogatives).

Matokeo yake ni kuwa mchakato mzima ulikuwa umeandaliwa na kumzunguka Rais mwenyewe na sitoshangaa siku chache zijazo mambo yakiwa magumu Dodoma, utasikia watu wanamuita Rais “aingilie kati”!

Kuelekea Tanganyika
Sina uhakika kama Rais Kikwete alikuwa miongoni mwa wabunge wa kundi la wabunge 55, maarufu kama G55 ambao walijiandikisha na kuweka majina yao wakiongozwa na aliyekuwa Mbunge wa Chunya (kabla haijagawanywa), Njelu Kasaka.

Vyovyote vile ilivyokuwa mchakato huu umewarudisha katika kurasa za siasa za nchi yetu watu ambao walipoteza nafasi ya kuirudisha Tanganyika kwa mbinde, mwaka 1993.

Kwa vile mchakato huu ulibuniwa vibaya na umeendeshwa vibaya na una kila dalili ya kuleta mijadala mikali kuna uwezekano kuwa Bunge la Katiba linaweza kujikuta linakwama na kugawanyika kwa namna ambayo ‘magenius’ wetu hawakufikiria mwanzoni.

Sijui ni kwa kiasi gani Rais Kikwete ataweza kuokoa hasa ukizingatia kuwa hivi sasa hakuna namna yoyote ya Rais kuingilia mchakato huu; hawezi kuuzuia, hawezi kuwaita wajumbe na hawawezi kuuahirisha zaidi ya kuuacha ufuate mkondo wake.

Ni kwa sababu hiyo, kama nchi na serikali ya Tanganyika vitarudi suala kubwa litakuwa ni kwa namna gani hivyo viwili vitaweza kuwa ndani ya Muungano na jinsi gani Watanganyika watataka kuendelea kuwa ndani ya Muungano na Zanzibar. Kwa vile mchakato huu kuna uwezekano utasababisha kurudi kwa Tanganyika – kama baadhi ya watu wanavyotamani – Rais Kikwete ama atakuwa shujaa au historia itamhukumu vibaya.

Ni vizuri kukumbuka kuwa hata Urusi ilivyogawanyika mojawapo ya matokeo yake wanasiasa wake wakajikuta wanatafuta wapi wakagombee uongozi na wengine kweli wakapata sifa zaidi katika nchi mpya ujiko (sifa)  ambazo wasingeweza kupata ndani ya Urusi.

Hili litatokea baadaye kwani licha ya kuwa mfumo huu utatengeneza nafasi kwa utumishi wa Serikali ya Muungano, lakini naamini ujiko mkubwa na nguvu kubwa katika hilo Shirikisho linalopendekezwa itakuwa ni kwa Tanganyika. Sijui ni kwa kiasi wanasiasa waliojazana bungeni watakapokuwa wanazungumza watakuwa wanazungumza kwa ajili ya uzalendo hasa au wakipigia hesabu ulaji mpya ambao wanajiandaa kujitengenezea!?

Vyovyote vile ilivyo, kufanikiwa kwa mchakato huu au kuharibika kwake kutaamua kwa kiasi gani historia itamhukumu Rais Kikwete. Anaweza akasifiwa kwa mengi katika uchumi, jamii na mengine lakini ni hili la Katiba Mpya litaamua kwa vizazi vijavyo ni kwa kiasi gani alikuwa kiongozi mwenye maono, mwenye kulinda taifa na ambaye aliweka maslahi ya taifa mbele kuliko kitu kingine chochote. Kinyume cha hapo, historia haitakuwa na huruma.

No comments:

Post a Comment