WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, March 7, 2014

VIDEO:Ngumi mkononi Bunge la Katiba



Ngumi mkononi ndilo neno jepesi ambalo linafaa kutumika baada ya vurugu kubwa kutokea jana ndani ya Ukumbi wa Bunge Maalumu la Katiba kiasi cha kumlazimisha Mwenyekiti wa Muda, Pandu Ameir Kificho kuahirisha semina kabla ya wakati wake.
Semina ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, imekuwa ikianza saa 4:00 asubuhi hadi saa 7:00 mchana kabla ya kuendelea tena kuanzia saa 11:00 jioni hadi saa 3:00 usiku. Jana, katika kipindi cha asubuhi, semina hiyo iliahirishwa saa 6:17 licha ya kuanza saa tano asubuhi kabla ya kurejea tena saa 10 jioni.
Ngumi zilitaka kupigwa baada ya Waziri wa Katiba na Sheria wa Zanzibar, Abubakari Hamis Bakari kuhoji uhalali wa Christopher Ole Sendeka na Ummy Mwalimu kuchangia wakati hawakuwamo katika orodha ya wachangiaji jambo ambalo liliibua mjadala mkali na kurushiana maneno kabla ya Mwenyekiti Pandu Ameir Kificho kuahirisha semina hiyo.
Chanzo cha vurugu
Kificho alimpa Ole Sendeka nafasi ya kuchangia Kifungu namba 58 cha rasimu ya kanuni na baada ya kutoa mchango wake, Hamisi ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Kanuni, alisimama na kumtaka Mwenyekiti Kificho kuacha kuwateua watu ambao hawamo katika orodha ya wachangiaji.
Kificho hakumsikiliza na badala yake, alimpa nafasi mjumbe mwingine wa Bunge hilo Ummy Mwalimu ambaye pia ni Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, kuchangia. Hata hivyo kabla hajafanya hivyo, Bakari alisimama tena na kumzuia kuchangia kwa madai kuwa hakuwamo kwenye orodha ya wachangiaji.
"Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutaendelea na utaratibu huu suala la kuchangia kanuni linaweza kutupeleka hadi miezi sita bila ya kumaliza. Haya majina hayakuwemo kwenye orodha ya wachangiaji na huyo aliyemaliza sasa Ole Sendeka, naye hakuwamo, naomba tuache mchezo huu," alisema Bakari.
Aliendelea: "Sekretarieti inakuchomekea majina mwenyekiti na kama hivyo ndivyo, basi tunatakiwa kuwachukulia hatua kali hawa kwani tunataka kujadili hoja ambazo hazimo."
Bakari alisema wajumbe waliotakiwa kuchangia ni wale ambao walipeleka majina kwa makatibu wa Bunge hilo pamoja na michango yao kwa maandishi ili wapewe nafasi ya kuzungumza, lakini Kificho alikuwa akiwateua wajumbe ambao hawamo katika orodha hiyo.
Kificho ajibu
"Mimi sina tatizo na jambo hilo, mkisema tuendelee basi sawa, lakini mkitaka tufanye mambo kwa uzuri inawezekana pia, jambo la muhimu ni kuwa tupo hapa kutengeneza Katiba ya wananchi siyo ya vyama."
Kelele zilianza kusikika huku wajumbe wakiimba kuwa mwenyekiti anayumba... na kumtaka mwenyekiti atoke nje na kukiacha kiti, kwani anafanya upendeleo.
 Kelele hizo ziliambatana na wajumbe hao kuwasha vipaza sauti bila utaratibu. Mjumbe Sadifa Juma Khamis ndiye aliyekuwa wa kwanza kuwasha kipaza sauti chake na kusimama wakati wote akisema anataka kuchangia, huku akiungwa mkono na wajumbe wengine kadhaa.
Kutokana na tukio hilo, Kificho alilazimika kumwita Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni, Profesa Costa Mahalu ambaye alikiri kuwa yako majina ambayo hayakuwamo kwenye orodha, lakini kwa mwenyekiti yalionekana.
Moto zaidi uliwaka baada ya Ole Sendeka kusimama hata bila ya kupewa nafasi na kusema anazijua kanuni vizuri na kwamba asingeweza kuzivunja.
"Nilijua hayo yote na mimi siyo dhaifu wa kanuni kwani najua kila kitu na tulikwenda tangu mwanzo; mimi, Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Peter Serukamba, ndiyo maana majina yetu yamo humo ila kama mapigo yetu yanawakwaza wengine waseme, siyo jukumu la mimi kupeleka mapendekezo yangu kwa Bakari, labda kama wewe una msimamo wako na chama chako," alisema Ole Sendeka.
Kauli hiyo ilizusha kelele za wajumbe ndani ya ukumbi, huku Kificho akiwatuliza na kusema Ole Sendeka aliteleza ulimi na kumtaka aombe radhi kama anataka, lakini mjumbe huyo aligoma kwa kuonyesha ishara ya mikono, jambo ambalo lilimfanya Bakari kusimama tena.
Bakari alisimama na kueleza uzoefu wake wa miaka 34 kwenye Bunge akijisifu kuwa yeye ni zaidi ya Ole Sendeka.
"Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sihitaji kuombwa msamaha na Ole Sendeka, nimekuwa kwenye mabunge haya tangu mwaka 1980, leo hii mtu kutoka Simanjiro miaka 10 iliyopita hawezi kunitisha," alisema Bakari.
Wengine nusura wapigane
Kauli hiyo iliwafanya wajumbe wengi bungeni kusimama, huku wengine wakitaka kupigana ngumi baadhi wakisema: "Twende nje tukapigane, twende nje tukapigane..."
Waliokuwa wakibishana zaidi ni Abdalla Sharia ambaye alitaka kupigana na Khatibu Haji kabla ya kuzuiwa na wenzao, huku Tauhida Nyimbo akitaka kuzikunja na Seleman Bungara (Bwege).
Wakati Bunge likiwa limechafuka na kukiwa na kelele nyingi, mwandishi wa habari hizi alimuona, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Anne Makinda akimuonyesha kwa ishara ya mikono Kificho kuahirisha semina.
"Naahirisha semina hii mpaka saa kumi jioni," alisema Kificho na kuwafanya wajumbe kupiga kelele huku wengine wakishangilia na baadhi wakiguna.
Nje ya ukumbi
Wakiwa nje ya ukumbi, Ole Sendeka alisema hoja zake ni nzito na haziwezi kuzimwa na Bakari ambaye anaonekana kuwa na masilahi binafsi.
Alisema yeye pamoja na wenzake (Ummy na Serukamba), bado wanatarajia kuwasha moto kwa kila kifungu ili mambo yaweze kukaa vizuri na kuwa kilichotokea kwake ni burudani.

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema tatizo kubwa lililosababisha mambo hayo ni misimamo ya mwenyekiti kuyumba wakati wote.

Hata hivyo, alilaani kitendo cha wajumbe wengine kuwa na hoja alizoziita za kitoto kwa kuzomeazomea akisema hata kama kiti kinayumba, bado walipaswa kuwa watulivu na kuangalia kilichowapeleka Dodoma.
Mjumbe mwingine, Charles Tzeba ambaye pia ni Naibu Waziri wa Uchukuzi, alitetea kauli ya Sendeka na kusema hata kama hakuwa kwenye orodha alipaswa kuchangia kwani hiyo ilikuwa ni semina ambayo kila mtu anayo haki ya kuchangia wakati wowote.

Bunge liliporejea jioni, wajumbe wawili-James Mbatia na Profesa Mark Mwandosya walisimama na kutoa nasaha za kutuliza jazba pale wajumbe wanapokwaruzana, huku Mwenyekiti Kificho akisema kilichotokea asubuhi kilitokana na yeye kutokujua kwamba baadhi ya wajumbe hawakuwa katika orodha.(P.T)

Chanzo:Mwananchi

No comments:

Post a Comment