WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, June 20, 2013

Mizengo Pinda: Nasema wapigwe tu




Dodoma/Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ameagiza vyombo vya dola kuwashughulikia kwa kuwapiga wale watakaokataa kutii amri wakati wakifanya vitendo vya uvunjifu wa amani.

Akizungumza katika Kipindi cha Maswali ya Papo kwa Hapo kwa Waziri Mkuu, bungeni Dodoma jana, Pinda alisema watu wanapokaidi wanajitakia matatizo na vyombo vya dola.

Alisema hayo alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Kilwa Kaskazini (CCM), Murtaza Mangungu aliyeuliza: “Serikali ipo tayari kiasi gani kubainisha na kuchukua hatua stahiki, badala ya kusakama makundi fulani, tujue chanzo halisi cha vurugu hizi na matatizo haya na jinsi gani vyombo vya dola vinavyoshughulikia kwa sababu yapo malalamiko katika baadhi ya maeneo kama Mtwara kwamba wananchi wanapigwa na vyombo vya dola?”

Waziri Mkuu alijibu: “Ni lilelile nililosema... mwishowe unaona anasema vyombo vya dola vinapiga watu. Ukifanya fujo, umeambiwa usifanye hiki, ukaamua kukaidi, utapigwa tu... hamna namna nyingine, maana wote tukubaliane kwamba nchi hii tunaiendesha kwa misingi ya kisheria.

“Sasa kama wewe umekaidi, hutaki unaona kwamba ni imara zaidi... wewe ndiyo jeuri zaidi watakupiga tu.... Mimi nasema muwapige tu, kwa sababu hakuna namna nyingine... maana tumechoka.”

Pinda alisema Serikali imedhamiria kurejesha amani nchini ikiwamo mkoani Mtwara na kuwataka Watanzania waiache Serikali ifanye kazi hiyo. Alisema Serikali ina orodha ya watu wanaosemekana kuwa ni vyanzo vya vurugu na matatizo yaliyotokea Mtwara na kushangaa wale wanaopinga kukamatwa kwao.

“Lazima tuwakamate na kama katika kuwakamata watafanya jeuri, jeuri, watapigwa tu kabla ya kupelekwa tunapotakiwa kuwapeleka, kwa sababu hatuwezi kuendelea na hali hii, mkadhani kwamba tutafika tunapokwenda. Nami nasema vyombo vya dola vijipange imara vihakikishe vinadhibiti hali hii,” alisema.

Hata hivyo, jibu hilo lilipata upinzani wakati Mbunge wa Konde (CUF), Khatibu Said Haji alipomwuliza Waziri Mkuu: “Hapo awali umetoa kauli nzito ya kuliambia taifa hili kwamba wale raia wote, ambao watakaokuwa wakaidi wapigwe tu na watapigwa tu; naomba ninukuu Katika Ibara ya 13 na Kifungu cha 6B cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano.

“Ni marufuku kwa mtu yeyote aliyeshtakiwa kwa kosa la jinai kuteswa kama mtu mwenye kosa, mpaka itakapothibitika anayo hatia kwa kutenda kosa hilo.

“Pia ibara hiyohiyo Kifungu cha 6 E; kinasema ni marufuku kwa mtu yoyote, kuteswa, kuadhibiwa kinyama au kupewa adhabu zinazoweza kumdhalilisha. Kwa kauli yako uliyoitoa huoni kwamba umevunja Katiba?” Akijibu swali hilo, Pinda alisema ni lazima kutofautisha kati ya mtu aliyekwishakamatwa na kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria... “Mimi ninayemzungumza hapa ni mtu yule ambaye ameamua kufanya vitendo hajakamatwa na ndiyo maana nilikwambia usiandamane... hapa mahali hutakiwi kwenda wewe ukaamua kutumia mabavu kwa sababu mko wengi, ndiyo maana nikasema, hawa watu tutashughulika nao hivyohivyo.”

Mbunge huyo hakuridhishwa na majibu hayo na kumtaka Waziri Mkuu kuyafuta.

Hata hivyo, Spika wa Bunge, Anne Makinda aliingilia katika na kumweleza mbunge huyo kuwa kila mtu alikuwa amemwelewa Waziri Mkuu na hakukuwa na haja ya kuendelea na hoja hiyo

Kabla ya swali lake la nyongeza, Mangungu aliuliza: “Ukisikiliza nyimbo nyingi za taifa katika Afrika zinasema hekima, umoja na amani ndiyo ngao zetu. Je, hali ambayo imejitokeza katika nchi yetu na matatizo yaliyojitokeza Arusha na maeneo mengine kama Mtwara. Nini tamko la Serikali?

Waziri Mkuu alijibu: “Swali lililoulizwa na Mheshimiwa Mangungu ni jambo linalotugusa sisi wote. Suala la amani, ulinzi, utulivu ndiyo hasa tunu ya kila nchi ingependa kuwa nayo. Ni kweli hivi karibuni kumejitokeza vurugu za hapa na pale kwa hiyo angependa tuwaeleze Watanzania kama Serikali tunafikiria tufanye nini.

Alisema ipo haja ya jukumu hilo kuachwa kwa viongozi wa kisiasa bila ya kujali itikadi zao... “Yako mambo ambayo lazima tukubali kwamba ni jukumu letu sisi wote na kila mmoja lazima azungumze lugha moja.

Ninyi wote ni mashahidi. Chadema waliposhinda hapa, wao walikuja waziwazi, wakasema tutahakikisha nchi hii haitawaliki. Sasa, inawezekana pengine ndiyo mwendelezo wa utekelezaji wa kauli hizo.

“La pili ni upande wa Serikali, lazima tuhakikishe kwamba wale wote ambao kwa kweli wanajaribu kuvunja amani kwa namna yoyote ile, kazi kubwa tuliyonayo ni kubanana, kupambana kwelikweli kwa njia zozote zile zinazoonekana zinastahili.

“Sasa mimi ninaomba sana Watanzania, maana kila juhudi zinapoonekana zinaelekea huko, unapata watu wengine wanajitokeza, unajua...unajua. Acheni Serikali itimize wajibu wake kwa sababu jambo hili ni la msingi, lazima tulilinde kwa nguvu zetu zote.

“Rai yangu kwa Watanzania kila mmoja ajue kwamba siku tukiingia katika vurugu, hakuna mshindi. Wote tutaumia, sasa wote tuhakikishe hili jambo tunalisimamia vizuri.”

Chadema waja juu

Akizungumzia kauli hiyo, Mkurugenzi Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika alisema: “Kauli ya Pinda inakiuka Katiba ya nchi na imethibitisha kwamba matumizi mabaya ya vyombo vya dola na kusababisha mauaji ya raia yana baraka za Serikali.”

Alisema kauli ya Pinda kama ilivyokuwa ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi zinatoa mwelekeo kwamba mauaji ya Arusha yana baraka za Serikali.
Wanasheria wakerwa

Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba alisema Waziri Mkuu hakustahili kutoa kauli kama hiyo.

Alisema Pinda hapaswi kuwa na jazba, bali anatakiwa kuwa na busara na kuzungumza kwa kuzingatia sheria za nchi badala ya kutoa matamshi ambayo siyo mwafaka kwa nchi inayoongozwa kwa kufuata sheria na taratibu.

Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Francis Stola alisema kauli hiyo ya Waziri Mkuu, mbali ya kwenda kinyume cha Katiba na sheria ya nchi, inaweza kuhatarisha amani.

Stola alisema matumizi ya nguvu kupita kiasi kudhibiti hali yoyote korofi hayaruhusiwi.

source: mwananchi

1 comment:

  1. ulevi WA MADARAKA huu polisi wapi waruhusiwe? hawa ambao tayai wanapiga hata pasipo kosa ambao wameshalemea kwa sababu ya rushwa tatizo la viongozi wetu hawasomi ni wakati gani wakuongea nini kama pinda ni bright angegundua kuwa watz hawanyanyasiki tena ndio maana utaona polisi wananyukwa nyumba za zinachomwa hofu yangu dhidi ya kauli Mh Pinda ni kwamba machafuko yatakuwa maradufu maana hata pale ambako haki inatakiwa kuutndekeka. haiwezi tendeka maana kauli ya seeriklai ilishatoka nyuka tu hakuna kujitetea huoni kuwa haki yetu ya kujieleza imedhulumiwa where is place for NATURAL JUSTICE.IKUMBUKWE KUWA TANZANIA NI YETU WOTE VIONGOZI ACHENI KAULI ZA MADHARAU WHO ARE YOU PEOPLE AND WHERE ARE YOU COMING FROM TO GIVE ORDER ON KILLING OTHERS TUMKUMBUKE DAUDI MWANGOSI ALIYEFIA MIKONONI MWA POLISI HAWA WANAPRUHUSIWA KUTUNYUKA TU. OH MUNGU SAIDIA TANZANIA ONDOA VIONGOZI WOTE AMBAO MIOYONI MWAO NI WAABUDI SHETANI DNOT ZAO NI UBINSAFSI DHULUMA ,KUSAINI MIKATABA MIBOVU BALI UWABARIKA NA KUWASTAWISHA WALE WOTE HAWAPATI USINGIZI USIKU KWA AJILI YA WATANZANIA WENZAO,WAPATE MATIBABU SAHIHI ELIMU NZURI WASHINDWE WALE WOTE WOTE KAZI YAO NI KUJALI MASLAHI YAO NA YA VYAMA VYAO WAWAPO NDANI YA BUNGE AMEN.....```````?/////??????

    ReplyDelete