WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Tuesday, June 11, 2013

Maalim Seif: Ataka Zanzibar ijitenge

 
Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad
Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, amesema Wazanzibari wanataka nchi yao.
Akihutubia mkutano wa hadhara eneo la Matemwe, Mkoa wa Kasklazini Unguja juzi, Maalim Seif alisema chama chake kitaendelea kudai mamlaka kamili ya Zanzibar katika mfumo wa Muungano, ikiwamo kurejeshewa kiti chake Umoja wa Mataifa (UN) licha ya rasimu mpya ya Katiba kulibakisha suala hilo katika orodha ya mambo ya Muungano.

Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar alisema iwapo mabadiliko ya Katiba hayatazingatia suala hilo, chama chake kitaendelea kudai na wananchi ndiyo watakaokuwa waamuzi wa mwisho kupitia kura ya maoni itakayoitishwa baada ya mabaraza ya katiba na Bunge Maalum la Katiba kujadili na kupitisha rasimu hiyo.

Alisema mapendekezo ya rasimu mpya bado yana kasoro kwa vile yanainyima Zanzibar kuwa mwanachama wa UN na kujiunga na jumuiya mbalimbali za kimataifa, ikiwamo uwezo wa kujiunga na Umoja wa Afrika (AU), Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) pamoja na kuwa na hati yake ya kusafiria.

Aliwaeleza wananchi kuwa mambo saba yaliobakishwa kwenye orodha ya mambo ya Muungano bado yanahitaji kupembuliwa na mengine kuondolewa ili kuipa Zanzibar mamlaka yake, likiwamo suala la sarafu na mambo ya nje.

Alisema tayari CUF imeunda jopo la wataalamu wa sheria kupitia rasimu hiyo ya Katiba kifungu kwa kifungu.

“Tumeunda jopo la wanasheria, wenye weledi mkubwa kwa minajili ya kupitia kifungu kwa kifungu. Wakimaliza kuichambua rasimu hiyo CUF itatoa msimamo wake. Wananchi ndiyo mtakaoamua baada ya rasimu ya mwisho kutoka na kukabidhiwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema Maalim Seif, huku akishagiliwa na wafuasi wake: “Tunataka nchi yetu…tunataka nchi yetu” na kupokea pia wanachama wapya 609.

Alidai kumejitokeza hali ya wasiwasi kwa Wazanzibari wengi kushindwa kushiriki kura ya maoni na Uchaguzi Mkuu ujao kutokana na Tume mpya ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) kuanza kuandaa mizengwe ili kuwanyima wananchi haki ya kupiga kura.

Alisema amefanikiwa kupata taarifa za siri za kuwapo njama za kuwanyima vitambulisho vya Uzanzibari Mkaazi ili watu wengi wakose nafasi ya kuandikishwa kwenye daftari la kudumu la wapiga kura na kwamba, kazi hiyo inafanywa na watendaji wa ZEC.

Maalim Seif alisema uchaguzi unaokuja ana matumaini makubwa ya kuibuka mshindi na ndiyo maana ZEC imeanza kuandaa mazingira ya kupunguza wapigakura kwa njia za hila.

Alimtaka Mwenyekiti wa ZEC kufanya kazi kwa kuzingatia uadilifu na Katiba ya Zanzibar na sheria zake.

“Nchi yetu inaendeshwa kwa kuzingatia misingi ya demokrasia…mwaka 2015 mkae mkitambua kuwa hamna nusura. Mtakwenda na maji. Huenda amani ya nchi ikavunjwa na Tume ya Uchaguzi Zanzibar. Hilo lifahamike mapema,” alisema Maalim Seif.

Wakati huo huo; Katibu wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW), Yahya Khamis Hamad, alisema rasimu ya Katiba mpya ya Muungano imeonyesha mwelekeo mzuri wa kupata katiba itakayomaliza matatizo ya kero za muda mrefu ya Muungano.

Hamad alisema kitendo cha wananchi kuwa watulivu tangu rasimu hiyo kutangazwa inaonyesha kuwa wanaiunga mkono na Tume ya Rais ya Mabadiliko ya Katiba kimsingi inastahili kupongezwa na siyo kubezwa kutokana na umakini waliouonyesha.

Alisema BLW imetayarisha mpango kazi wa kuwaelimisha wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kuwa rasimu iliyotoka kabla ya kuanza kujadiliwa na Bunge la Katiba ili kuhakikisha maslahi ya pande zote yanazingatiwa.

“Mara nyingi Wazanzibari hatusemi kile tunachokitaka. Ni hodari wa kulalamika. Tuwatumie wataalamu wetu kujenga nguvu ya hoja. Nafikiri kwa rasimu hii upo uwezekano mkubwa wa kufika salama na kupata Katiba mpya bora itakayoondoa utata na mivutano isiyo na ulazima,” alisema Hamad ambaye kitaaluma ni mwanasheria visiwani humo.

Tangu Mwenyekiti wa Tume ya Katiba Mpya, Jaji Joseph Warioba, alipotangza rasimu ya Katiba Mpya Juni 3, mwaka huu ikipendekeza mfumo wa Muungano wa serikali tatu, kumekuwapo na maoni tofauti ya wananchi, wanasiasa, wanaharakati na wanasheria kuhusuiana na mfumo huo.

Baadhi wanaunga mkono muundo wa Muungano wa serikali tatu na wengine wanapinga kwa madai kwamba, utaongeza gharama za uendeshaji na kuhatarisha usalama wa Muungano, huku uchumi wa Zanzibar ukiwa ni mdogo.

Wengine wanatetea mfumo wa serikali mbili wakitaka uendelee kubaki pamoja na jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment