WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Monday, November 12, 2012

Serikali kujenga uwanja wa ndege wa Kimataifa huko Serengeti


Picture

Mwenyekiti wa chama cha Mapinduzi Taifa (CCM) Rais Jakaya Mrisho Kikwete akilitolea ufafanuzi jambo kwa wajumbe mbalimbali waliofika katika siku ya pili ya mkutano mkuu wa nane wa CCM unaoendelea hivi sasa katika ukumbi wa Kizota mjini Dodoma. Kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, Amani Abeid Karume
RAIS Jakaya Kikwete amesema serikali  ina mpango wa kujenga uwanja wa ndege wa kimataifa katika mji wa Mugumu, wilayani Serengeti, ili kurahisisha usafiri kwa watalii waendao au kutoka kwenye vivutio vya utalii vilivyopo kanda ya kaskazini.

Amesema hayo mbele ya wajumbe wa Mkutano Mkuu wa 8 wa CCM unaoendelea mjini Dodoma.

Kauli hiyo ya mwenyekiti wa ccm ameitoa alipokuwa akifafanua kuhusu taarifa iliyosomwa na Naibu Waziri wa Uchukuzi, Dkt. Charles Tizeba, mbele ya wajumbe hao kuwa serikali itajenga kiwanja hicho.

Akitoa ufafanuzi huo, Rais Kikwete amewaeleza wajumbe hao kwamba uwanja utakaojengwa utakuwa eneo la Mugumu na sio kwenye Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

Amesema kuwa hatua hiyo ya ujenzi wa kiwanja hicho cha ndege utawawezesha watalii  uchaguzi wa ama kutua Mugumu au Uwanja wa Kimataifa wa Kilimanjaro.

Amesema kwa watalii watakaoshukia uwanja wa KIA na kutembelea hifadhi ya Tarangire, Manyara, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) wataweza kuondoka kurejea makwao kwa kutumia uwanja utakaojengwa Mugumu badala ya kurudi tena hadi KIA.

Hali kadhalika amesema, watalii watakaoshuka kwenye uwanja utakaojengwa Mugumu hawatakuwa nahaja ya kurudi tena Serengeti ili warejee makwao kwa kuwa wataendelea kutembelea vivutio vingine kwenye katika Hifadhi za Manyara, Tarangire hadi Mlima wa Kilimanjaro na kurejea makwao kwa kutumia uwanja wa KIA.

Akizungumzia kuhusu Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Songwe, dk kikwete amesema umekwishakamilika na uzinduzi wake unatarajiwa kufanyika Desemba mwaka huu.

Amesema uwanja huo uko kusini na yapo mashirika kadhaa ya ndege ya kimataifa ambayo yameomba ndege zao ziwe zinatua kwenye uwanja huo wakati zikifanya safari zake za kwenda nchi za Kusini mwa Afrika.

Aidha amesema upo mpango kabambe wa kulitumia eneo la ukanda wa Nyanda za Juu Kusini kwa kilimo kikubwa cha maua ambayo yatakuwa yakisafirishwa kwenda kuuzwa nje kupitia uwanja huo.

Ametanabaisha kuwa kwa sasa serikali itaelekeza nguvu zake katika kuhakikisha kanda ya Nyanda za Juu Kusini, inapewa  msukumo kwa kilimo kikubwa cha maua ambacho tutakipa nguvu zaidi ili yasafirishwe kwenda kwenye masoko ya nje.

 RAIS Jakaya Kikwete amesema baada ya kupatikana kwa gesi asilia kiasi cha mita za ujazo trilioni 33 , serikali kwa kuanzia inatarajia kujenga gridi ya taifa ya gesi jijini Dar es Salaam, kwa ajili ya matumizi ya viwandani na majumbani.
Amesema gesi itakayopatikana itatumika kwa matumizi ya viwandani na majumbani na kiasi kingine kitauzwa nje.

Amesema baada ya kukamilika giridi ya gesi, wakazi wa Dar es Salaam watakaohitaji kupata gesi hiyo kwa matumizi ya majumbani kwao watapelekewa.amesema utaratibu kama huo utafanyika kwa mikoa mingine.

Amesema upatikanaji wa gesi hiyo utaifanya Tanzania iweze kukuza uchumi wake kwa kuwa itatumika kwa uzalishaji wa bidhaa viwandani, mbolea na uzalishaji wa umeme.

Hata hivyo, amesema gesi itayouzwa nje itasafirishwa kwa kupitia bandari za Mtwara na Kilwa kwa kuwa itakuwa gharama kuisafirisha hadi Dar es Salaam katika lengo la kuiuza nje.

Amesema sera ya gesi inatarajiwa kukamilika hivi karibuni pamoja na kuweka miundombinu itakayowezesha kudhibiti uhujumu wa biashara hiyo nje ya nchi.


Source: 
http://www.wavuti.com

No comments:

Post a Comment