WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Wednesday, November 21, 2012

Ili kurudisha utamaduni wa kusoma vitabu, tuanzishe utaratibu wa kuwasomea watoto


Utamaduni wa kujisomea huanza tangu utotoni 
kama anavyoonekana mtoto Magdalena Hiluka


BISHOP HILUKA

Dar es Salaam

KUSOMA vitabu ni jambo zuri na muhimu sana katika maisha ya binadamu kwani mambo mengi muhimu katika dunia hii yapo katika maandishi, iwe kwenye vitabu au mitandao ya jamii, yakiwemo maneno ya Mungu kwa wale wenye imani za kiroho. Yote haya utayakuta katika maandishi, ndani ya vitabu. Kama huna utamaduni wa kujisomea vitabu au kuperuzi katika mitandao ya intaneti, basi usitegemee kupata habari nzuri, kuelimika zaidi na kujua mengi yanayotokea duniani.

Wiki chache zilizopita katika kuperuzi kwangu baadhi ya machapisho nikiwa na lengo la kujaribu kuongeza maarifa, nilikutana na makala moja kuhusu usomaji wa vitabu ambao Watanzania tumeuacha siku hizi, ingawa jambo hili limekuwa likiandikwa sana lakini nikiri tu kuwa makala hii ilinivutia sana, ndiyo maana leo nimeamua kuja na hoja hii.

Makala hii iliandikwa na mmoja wa waandishi wa vitabu wakongwe, Profesa Joseph Mbele, Mtanzania anayeishi Northfield,Minnesota, nchini Marekani. Profesa huyo aliandika akihimiza wazazi kupenda kuwasomea watoto wao vitabu ili kuwavutia kupenda kusoma, akifananisha na enzi zile za mababu na mabibi zetu, ambapo ilikuwa ni kawaida kwa wazee hao kukaa na watoto au wajukuu jioni na kuwasimulia hadithi.

Utamaduni huu ulikuwa ni sehemu ya maisha, na ingawa watoto walichukulia kama kitu cha kawaida lakini ilikuwa ni sehemu ya elimu waliyopewa hao watoto. Hapakuwa na shule tulizonazo leo, wala vitabu, lakini wazee walikuwa walimu bora, waliotumia mbinu mbalimbali, kama hizi hadithi, katika kuwaelimisha watoto.

Lakini siku hizi, japo tuna vitabu na shule karibu kila mtaa, lakini tunashindwa kutumia fursa ya kutumia vitabu kuendeleza elimu ya watoto! Sijui tatizo ni nini? 

Hivi tatizo ni nini hata pale tunapokosa uwezo wa kuwasimulia hadithi kwa mtindo wa mababu na mabibi zetu, tunayo fursa ya kuwasomea vitabu, lakini tunashindwa kuitumia na kujikuta tukiuendeleza ule msamiati ambao binafsi umekuwa ukiniudhisana, wa “Watanzania hatuna utamaduni wa kusoma vitabu”.

Katika nchi za wenzetu, kama nchi aliyoitolea mfano Profesa Mbele ya Marekani, wamekuwa wanaendeleza utamaduni huu kwa kuwasomea watoto hadithi za vitabuni. Watoto wa Kimarekani wanategemea mzazi awasomee vitabu. Ni kawaida kwa mzazi kumsomea mtoto kitabu kabla hajalala.

Wamarekani wanajali sana utamaduni wa kusoma vitabu. Utawaona wazee, watu wazima, wake kwa waume, vijana, na watoto katika maduka ya vitabu. Utawaona wazazi wakiwa wanakuja na watoto wao. Utawasikia wakiongea na watoto kuhusu vitabu, wakiwasomea watoto vitabu, wakijibu maswali ya watoto, na kadhalika.

Hali hii ni tofauti sana na iliyopo hapa nchini mwetu Tanzania. Leo ni Ijumaa. Je, ni mzazi gani Mtanzania ambaye siku kama ya leo anaenda kwenye duka la vitabu? Ni mzazi gani ambaye anampeleka mtoto wake kwenye duka la vitabu?
Imewekwa na Mkereketwa 

No comments:

Post a Comment