WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, November 23, 2012

Mawaziri wazomewa mbele ya Kinana



KATIBU Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana 
Na Na Abdallah Bakari, Mtwara na Raymond Kaminyoge, Sumbawanga   

MAWAZIRI watatu wa Rais Jakaya Kikwete juzi walizomewa baada ya kupanda jukwaani kujibu kero mbalimbali za wananchi katika mkutano wa kwanza wa viongozi wapya wa CCM taifa, ulioongozwa na Katibu Mkuu wake, Abdulrahaman Kinana.

Tukio hilo lilitokea juzi mkoani Mtwara ambako Kinana na mawaziri hao walikuwa katika ziara ya chama kujibu kero mbalimbali za wananchi.Mawaziri waliokumbwa na dhahama hiyo ni Christopher Chiza wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Hawa Ghasia (Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa - Tamisemi) Naibu wake, Aggrey Mwanri.

Chiza ndio alikuwa wa kwanza kukumbana na zomeazomea hiyo, lakini mambo yalikuwa magumu zaidi kwa Ghasia ambaye alizomewa tangu alipoanza kuzungumza mpaka alipomaliza.Ghasia ambaye pia ni mbunge wa Mtwara Vijijini, alirushiwa makombora na Rukia Ismail Athumani ambaye alimshutumu yeye pamoja na Mbunge wa Mtwara mjini, Asnein Murji kwamba waliruhusu gesi kupelekwa Dar es Salaam wakati wananchi wa mkoa huo hawajafaidika nayo.

“Ghasia na Murji kwanini mnaudanganya umma kwa kupeleka gesi Dar es Salaam, sisi hatuna ubaya na chama ila hatutaki gesi iende huko” alisema Athumani huku akishangiliwa na mamia ya watu waliohudhuria mkutano huo.Kabla ya dada huyo kuteka hisia za wananchi kwa kuwasilisha kero hiyo, Kinana alimruhusu mwananchi mwingine, Issa Kambona ambaye pia alieleza kuwa hakubaliani na suala la gesi hiyo kupelekwa Dar es Salaam.

Kinana alisema amesikia hoja hizo za wananchi na kwamba atamueleza Waziri wa Nishati na Madini azungumze na wananchi wa Mtwara kuhusu gesi hiyo.Baada ya mambo kuzidi kuwa magumu, Ghasia alilazimika kupanda jukwaani kujibu makombora aliyokuwa akirushiwa na wananchi waliofika katika mkutano huo.

“Sio kweli kwamba hatutetei maslahi yenu, gesi iliyopo ni nyingi hamuwezi kuitumia na kuimaliza, kuna futi za ujazo trilioni 20,000 na tunaweza kuitumia kwa zaidi ya miaka 90, hata hivyo, Wizara ya Nishati na Madini imetoa ofa ya kuwalipia chuo vijana 150 kila mwaka,” alisema Ghasia, lakini wananchi hao waliendelea kumzomea.“Uongo, uongo, hatutaki, hatutaki, huyoo, huyooo” walisikika wakisema wananchi hao, hali iliyomfanya Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye kuingilia kati, kujaribu kuwatuliza.

“Kelele unazozisikia dada (Ghasia) zinaashiria kuna jambo, nafasi hizo 150 hawazipati, kama zinatolewa basi kwa upendeleo,” alisema Nape huku akishangiliwa na wananchi hao.Baada ya hali kutulia kiasi, Ghasia alijaribu kuendelea kutoa ufafanuzi, lakini kitendo cha kuanza kuzungumza, wananchi hao walianza tena kuzomea.

“Kila mtu amelelewa katika mazingira tofauti, hilo halinihusu…watu wangu wa Mtwara vijijini wamenielewa,” alisema Ghasia na kuteremka jukwaani hali iliyozidisha kelele za kumzomea.Nape alisawazisha mambo kwa kusema, hoja ya wananchi hao imechukuliwa na itawasilishwa kwa Serikali ili kuona namna ambavyo inaweza kukaa na wananchi hao na kuweka maslahi yao mbele.

Ilivyoanza
Panzia la zomea zomea lilifunguliwa na Chiza alipopanda jukwaani kujibu hoja ya kuyumba kwa soko la zao la korosho, ambapo wananchi walimpinga baadhi ya kauli alizozitoa.“Tatizo la korosho ni baadhi ya viongozi wa vyama vya ushirika na wengine ni watendaji wa Serikali …nipo hapa na wala siondoki, nitalishughulikia hili ili korosho zinunuliwe” alisema Chiza huku sauti za wananchi zikimpinga kwa kusema “uongooo”.

Hata hivyo, Chiza aliweza kukabiliana na hali ya zomeazomea jukwaani baada ya watuliza wananchi kwa kusisitiza kuwa ataendelea kuwapo Mtwara, kushughulikia tatizo hilo ili ununuzi uendelee.Naibu Waziri wa Tamisemi, Mwanri alipata wakati mgumu mara alipopanda jukwaani na kuanza kuzungumzia namna ya kumaliza kero ndogondogo zinazoletwa na mamlaka zake, wananchi walikuwa wanazoea “huyoo…hatutaki” lakini baada ya kuanza kuongea alionekana kuiteka hadhira na mambo yakawa shwari. “

“Tumesema wauza vitumbua, wasibughudhiwe … mkurugenzi njoo jukwani, nakuagiza kuanzia leo marufuku wanafunzi kurudishwa shuleni kwa sababu ya michango” alisema Mwanri huku akishangiliwa.Awali Kinana alisema mkutano huo unalenga kuzipatia ufumbuzi kero za wananchi ambazo zinawezakuwa kikwazo kwa chama hicho kuingia madarakani mwaka 2015.

Katibu mkuu huyo wa chama tawala alisema umefika wakati wa chama kusimamia utendaji wa Serikali kutatua kero za wananchi wa mkoa wa Mtwara ikiwa ni pamoja na kuyumba kwa soko la korosho na gesi.“Najua hapa kuna kero kubwa mbili, korosho na gesi, nimekuja na Mawaziri hapa watatoa majibu leo” alisema Kinana huku akishangiliwa na umati mkubwa wa watu ulioudhuria mkutano huo.

Sifa mgombea urais
Katika hatua nyingine, Kinana amevunja ukimya kuhusu mbio za urais mwaka 2015 na kusema CCM itamtosa bila kumuonea haya mwanachama yeyote atakayeomba kuteuuliwa kugombea urais kwa tiketi yake, huku akiwa kinara wa kutegemea makundi kumwigiza katika nafasi hiyo.Badala yake akaeleza kuwa chama hicho kitamteua mgombea mwadilifu, anayekubalika na watu na asiye na makundi.

Mbali na sifa hizo Kinana pia ameeleza kuwa mgombea huyo wa CCM atakuwa msafi, makini, mchapakazi, mzalendo ambaye anajali maslahi ya wananchi na kwamba Mei 2015 wataanza kutoa fomu kwa wana CCM wanaowania nafasi hiyo.Kinana alisema hayo jana katika kijiji cha Isesa, Sumbawanga Mjini wakati akifungua tawi la CCM na kuzungumza na wanachama.

Katika kipindi cha kuuliza maswali, wanachama hao walitaka kufahamu namna chama hicho kilichojipanga kumpata mgombea urais makini ambaye hatakuwa mzigo kumnadi dhidi ya wapinzani.“Tumejipanga vizuri, atapatikana mgombea urais bora, vigezo vipo wazi tunataka mgombea urais mwadilifu, makini, mchapakazi, mzalendo ambaye anakubalika na wananchi,”alisema Kinana.

Aliongeza kwamba chama hicho kitatoa fomu kwa wanaotaka kuwania nafasi hiyo na vikao vya chama ndivyo vitakavyoamua,”alisema Kinana.“Tuna utaratibu mzuri wa kupata wagombea urais bora kwa sababu vigezo vyote viko wazi na kwamba wagombea hao watapimwa kwa vigezo hivyo,” alisema Kinana.

Alisema Wanasumbawanga wasiwe na wasiwasi watampata mgombea ambaye atakuwa mwiba kwa vyama vya upinzani.Alisema kiongozi mwenye makundi na asiyekuwa mwadilifu hatakuwa na nafasi ya kuteuliwa na chama hicho kugombea urais.“Haya si maneno yangu bali ni vigezo vya chama vilivyo wazi ambavyo vinatumiwa kwa kila mgombea wa nafasi hiyo kubwa kushinda zote,” alisema

Alisema anakifahamu chama hicho na kwamba kitavitumia vigezo hivyo ili kupata mgombea urais ambaye wananchi wanamkubali.Awali wanachama wa chama hicho wakiongea kwa hisia kali, walisema wanataka chama hicho kimsimamishe mgombea urais atakayekuwa mwiba kwa wapinzani.

“Tunayasikia majina ya watu wanaowania nafasi hizo, chonde chonde katibu mkuu tunaomba apatikane kiongozi ambaye hatatupatia kazi ya kumnadi, awe mwadilifu ambaye akitangazwa watu wafurahi bila kunung’unika,” alisema Peter Lilata.Alisema, “tukikosea kuteua kiongozi bora tutakuja kujuta hapo baadaye.”

Vijana CCM, Chadema nusura wazipige
Katika ufunguzi wa tawi la CCM la Isesa nusura vijana CCM na wa Chadema watwangane makonde baada ya vijana wa Chadema kuwatuhumu CCM kwamba wamewaibia bendera ya chama chao.

Mabishano kuhusu bendera hiyo yaliendelea katika kipindi chote ambacho Kinana alikuwa akizungumza na wanachama wa tawi hilo.“Hawa CCM wameng’oa bendera yetu hapa huo siyo ustaraabu ni lazima mturudishie bendera yetu vinginevyo patakuwa hapatoshi,” mmoja wa vijana wa Chadema alisikika akisema.
Hata hivyo, busara za askari polisi waliokuwa katika mkutano huo zilisaidia kuzima hasira zavijana wa Chadema
.

source: mwananchi

No comments:

Post a Comment