WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, February 22, 2013

FBI kusaka waliomuua Padri



Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi 
MAOFISA wa Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI), wamekubali kufanya upelelezi wa mauaji ya Padri Evaristus Mushi yaliyotokea Zanzibar Februari 17, mwaka huu.

Kwa mujibu wa habari za kuaminika zilizopatikana jana maofisa hao wako nchini na tayari wamekutana na baadhi ya viongozi wa Serikali kwa ajili ya kuanza kazi hiyo.

Chanzo chetu cha habari kimeeleza kuwa maofisa hao walikutana na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi kwa ajili ya kuangalia ni namna gani watafanya shughuli zao katika upelelezi huo.

Kutua kwa maofisa hao kumekuja baada ya kauli iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete katika salamu zake za rambirambi baada ya mauaji ya Padri Mushi kuwa ameliagiza Jeshi la Polisi kutumia nguvu zake zote pamoja na kushirikiana na vyombo vingine vya usalama vya hapa nchini na mashirika ya upelelezi ya nchi rafiki katika kufanya uchunguzi wa mauaji hayo.

Pamoja na ushiriki wa FBI, pia Serikali inazungumza na nchi nyingine rafiki ili kushirikiana nao katika upelelezi ya matukio mengine ya mauaji ya hivi karibuni.

Taarifa zinaeleza kuwa maofisa wa Serikali wamezungumza na taasisi za upelelezi za nchi tano ili kuongeza nguvu katika kazi hiyo.
Taasisi nyingine inayotajwa kwamba huenda ikashiriki katika uchunguzi huo ni Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai ya Uingereza ya Scotland Yard.

Hatua hizi zinakuja baada ya Dk Nchimbi kutoa tamko la Serikali, Jumapili iliyopita, akidai kuwa mauaji ya Padri Mushi yalikuwa ya kigaidi hivyo Serikali itachukua hatua kali kuhakikisha waliohusika wanakamatwa.

Haitakuwa mara ya kwanza kwa Serikali ya Tanzania kushirikiana na asasi za kimataifa katika ku chunguza matukio ya uhalifu na yale ya kigaidi.
Hii itakuwa mara ya pili kwa FBI kuja nchini kufanya operesheni kubwa ya upelelezi. Mwaka 1998, walifika kuchunguza kulipuliwa kwa Ubalozi wa Marekani na kugundua ilikuwa kazi ya Kundi la Al-Qaeda.

Pia mwaka 1984 walikuja wapelelezi kutoka Scotland Yard kuchunguza kuungua kwa Benki Kuu ya Tanzania (BOT).

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Ame Silima alithibitisha Serikali kuanza mazungumzo na mashirika mbalimbali ya upelelezi duniani kwa ajili ya kushirikiana nayo kuchunguza mauaji ya Padri Mushi.
Alisema tayari wameanza kufanya mazungumzo na mashirika hayo kutoka nchi mbalimbali, lakini alisema ni mapema mno kuyataja... “Ila
tukikamilisha kila kitu tutawaiteni na kuwaeleza hatua tuliyofikia, ila tumeanza kufanya mazungumzo nayo. Kama unavyojua Rais Kikwete alitoa agizo hilo, sisi tumeanza kulitekeleza.”
Waziri Silima alisema kwanza wataanza kuchunguza mauaji ya Padri Mushi... “Tutaanza kuchunguza kwanza chanzo cha mauaji haya ili tujue kila kitu.”

Watuhumiwa wakamatwa
Polisi Zanzibar inawashikilia watu kadhaa wakihusishwa na mauaji ya Padri Mushi.

“Tumekamata watu kadhaa kuhusiana na kifo cha Padri na tunaendelea kuwahoji na wengine tutawaachia,” alisema Kamishna wa Polisi wa Zanzibar, Mussa Ali Mussa jana.
Kamishna Mussa hakutaka kutaja idadi ya watu waliowakamata hadi sasa na kuwahoji akisema: “Tunakamata na kuhoji na kuachia.”
Wananchi a wa Zanzibar wamepunguza matembezi ya usiku tangu Jumapili wakihofia kukamatwa na vyombo vya ulinzi ambavyo vimeimarisha ulinzi kutokana na tukio hilo.

Jimbo la Bububu ambalo ndiko marehemu alikouawa linaongoza kwa wananchi kujifungia mapema majumbani mwao kwa hofu hiyo ya kukumbwa na mikono ya maofisa usalama.

Kanisa la Mtakatifu Teresia lililopo Beit el Raas, nje kidogo ya Mji wa Zanzibar limefungwa tangu Jumapili baada ya Padre Mushi kuuawa kwa kupigwa risasi alipokuwa akienda kuongoza ibada katika kanisa hilo.
Padri Mushi aliyekuwa kiongozi katika Kanisa la Minara Miwili, alizikwa Kitope Mkoa wa Kaskazini Unguja kwenye makaburi ya viongozi wa kanisa hilo juzi.

Kuuawa kwake ni tukio la tatu kubwa la kushambuliwa kwa viongozi wa dini baada ya kumwagiwa tindikali kwa Katibu wa Mufti wa Zanzibar, Sheikh Fadhil Soraga na kushambuliwa kwa risasi Padri Ambros Mkenda wa Kanisa Katoliki mwaka jana.

Aidha, viti vya Kanisa la Sloam liliopo Kianga, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja vilichomwa moto na watu wasiojulikana alfajiri ya Jumanne iliyopita.

Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment