WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Saturday, April 26, 2014

JK: Muungano uko salama

Watakaochezea Muungano kukiona cha mtemakuni
Awashangaa Ukawa kususa…Awashauri warudi bungeni

Rais Dk.Jakaya Kikwete wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akiwa na Rais wa Zanzibar, Dk.Ali Mohamed Shein jana, baada ya kupokea picha za waasisi wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar,hayati Mwl.Julius Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume kwenye viwanja vya Saba Saba kupitia wananchi wa Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano huo. (Picha Tryphon Mweji).
Rais Jakaya Kikwete amesema Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uko salama na watakaouchezea watakiona cha mtemakuni.
Rais Kikwete alitoa kauli hiyo jana wakati alipokuwa akiwahutubia wananchi wa Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanzania.

“Nimeamua kuzungumzia jambo hili leo ili kesho watu wapate kujimwaya kwenye sherehe za Muungano… Muungano uko salama na atakaye uchezea ataona cha mtema makuni”.

Alisema katika historia ya Jamhuri ya Muungano hakuna budi kukumbuka kitendo cha historia na cha kijasiri kilichofanyika Ikulu ya Zanzibar kwa aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Tanganyika  kwa kutia saini hati ya Muungano.

Alisema hati hiyo ndiyo makubaliano na mkataba rasmi wa Muungano. Rais Kikwete alisema hati hiyo imefafanua kuhusu muundo wa Muungano, mambo ya Muungano na mfumo mzima wa utawala.

Akielezea historia ya Muungano huo, alisema Desemba 10, 1964 jina rasmi la Tanzania liliidhinishwa baada ya kubuniwa na kijana wa miaka 18 mwenye asili ya kihindi aliyekuwa akisoma shule ya Aga khan Morogoro, baada yakufanyika mashindano ya kubuni jina.

“Watanzania tuna kila sababu ya kusheherekea jubilee ya zahabu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Miaka 50 ni mafanikio makubwa sana. Wapo wenzetu walioungana Afrika lakini hawakufanikiwa. Wapo wengine mpaka leo wanaendelea kujadiliana muungano lakini hawajafanikiwa,” alisema.

Alisema wengi wanamjua Kambarage Nyerere hakuwa mtu wa kujigamba, lakini katika Muungano alisema Tanzania ni lulu ya pekee iliyoundwa kwa juhudi za wananchi wenyewe.

Aliongeza kuwa hata Umoja wa nchi za Afrika Mashariki  na Umoja wa Nchi za Afrika unaweza kuwepo ikiwepo nia thabiti. “Sisi tumeweza na wenzetu pia wanaweza.

Alisema wapo wanaojiuliza Muungano kati ya Zanzibar na Tanganyika umewezekanaje na umewezaje kudumu kwa muda mrefu kiasi hiki. Alisema majibu ya maswali haya ni muhimu  kwa Watanzania kwa kuwa  unaendelea kudumu na kustawi.

Rais Kikwete alisema asilimia 91 ya Watanzania walizaliwa baada ya Muungano, na wale waliokuwepo baada ya Muungano wamebakia  kuwa asilimia 9 tu na kwamba majibu ya swali hilo yana umuhimu wa pekee na yatawasaidia wale waliozaliwa baada ya Muungano, kuelewa.

MIONGO MITANO YA MUUNGANO

Alisema  waasisi,  Nyerere na Karume walikuwa waumini wa dhati wa Muungano wa nchi zao kuungana. Walikuwa washiriki wa vuguvugu la ukombozi la Afrika ili kujenga umoja, mshikamano na ushirikiano. Pia kuunganisha nchi zao baada ya uhuru.

Uamuzi wa waasisi hao haukuwa jambo la ghafla ulianza tangu harakati za kupata uhuru Alisema  waasisi hao, walitanguliza maslahi ya taifa mbele kabla ya mambo yao binafsi.
Waliunganisha nchi hizo zikiwa na muda mfupi tu baada ya uhuru na ukombozi kwa sababu ya imani yao na ujasiri mkubwa wa kuunganisha nchi zao. Ni uamuzi mkubwa ulioweza kufanywa na viongozi hao.
Alisema watu wa Tanganyika ni watu wamoja, lakini kwa bahati mbaya  wakoloni ndio waliowatenganisha na kujiona waishi katika nchi mbili.

WANAOTAKA MUUNGANO UVUNJIKE WANA LAO JAMBO

Alisema wako watu wachache wenye roho mbaya wanaochukia Muungano, lakini ni kidogo sana. Alisema Watanzania wengi wanataka kuona changamoto za Muungano zinatatuliwa.  “Wanaopenda Muungano uvunjike wana lao jambo si wenzetu.”

Aliongeza kuwa katika miaka 50 ya Muungano kumekuwa na muingiliano wa watu kutoka upande mmoja kwenda upande mwingine na kuwa kwao na kwao  kwa asili wanakwenda kusalimia.

Alisema watu wapatao 600,000 wenye asili ya Zanzibar wanaishi Bara na Watu wapatao 100,000 wenye asili ya Bara wanaishi Zanzibar na kwamba wakati wa Muungano Zanzibar ilikuwa na watu 300,000 tu. Uhusiano wa kiuchumi, kibiashara na kijamii umekuwa wa kawaida na kufanya safari nyingi kwa siku kati ya Zanzibar na Bara.

Mwaka 2013 abiria waliosafiri kwa meli kati ya Zanzibar na Dar es Salaam ni  1,492,571, Usafiri wa ndege abiria mwaka 2012 ni 386,048.

“Tutakuwa tumetenda dhambi kubwa sisi viongozi kwa wananchi hawa kama tutakuwa  chanzo cha chokochoko ya kudhoofisha muungano huu na kuvunjika,” alisema na kuongeza  wananchi ndiyo watakaoumia na kusumbuka.

Viongozi watafanya mambo yao raha mstarehe kwa kupokelewa uwanja wa ndege kwa watu maalum ( VIP)  kwa kupigiwa mizinga. Alisema Muungano ndio ulioleta uhusiano wa karibu wa viongozi wa siasa na vyama vya siasa wa Tanganyika na Zanzibar.

Wakoloni waliwalazimisha wananchi kuwa katika makundi kutokana na rangi zao. Ndiyo maana kuna maeneo yanaitwa  uzunguni, uhindini na usawahilini.

 Waarabu na Wahindi walikuwa daraja la kwanza,  wwa ajili hiyo watu wakalazimishwa kuunda vyama vya kutetea maslahi yao ya kijamii. Vyama hivyo viliundwa kwa misingi ya rangi ndio maana kulikuwa na Pan African Association (PAA) na Tanganyika African Association (TAA).

Baadaye kukawana Afro Shiraz Part (ASP) ambayo ilifanya mapinduzi kuondoa dhuluma kwa upande wa Zanzibar na Tanganyika African National Union (TANU) ambavyo viliungana Februari 5, 1977 na kuzaliwa Chama cha Mapinduzi (CCM).

Alisema katika vikao vya vyama hivyo, masuala ya Muungano yalikuwa yakizungumzwa na kufanya kuwa sehemu kubwa ya kudumisha Muungano huo.Alisema katika miaka 50 ya Muungano pia kumekuwa na matatizo ya ustawi wa Muungano huo lakini hatua mbalimbali zimekuwa zikuchukuliwa na kufanikiwa kupata ufumbuzi.

Mwaka 1993 wakati mzee Ali Hassan Mwinyi alipokuwa Rais, aliunda Tume ya Shelukindo kushughulikia mambo ya Muungano. Mwaka 2006 kati ya kero 31 za Muungano zilibaki 13 na katika vikao vya pamoja vya serikali mbili yamebaki mambo sita.

Alisema suala la ajira ya watumishi kutoka Zanzibar limeshapatiwa ufumbuzi. Serikali mbili zimekubaliana fomula  na kwamba kero iliyobaki ni mgawanyo wa mapato na mgao wa Zanzibar katika benki na masuala ya vyombo vya moto ambalo linazungumzwa kiutawala na kuahidi kuwa baada ya muda mfupi litapatiwa ufumbuzi.

HATI YA MUUNGANO
Amewashangaa wanaosema sahihi ya Nyerere ni sawa lakini ya Karume imeghushiwa. Alisema kama kughushiwa basi atakuwa ameghushi Nyerere.

“Unaposema sahihi ya Karume imeghushiwa, basi aliyegushi ni Nyerere, hivi watu walipokuwa wanashuhudia ni kwamba mzee Karume alikuwa asaini chochote pale,” alihoji. Alisema hati ile ni suala muhimu sana ndiyo maana  Nyerere alipostaafu alimuachia Mwinyi,  na Mwinyi alipostaafu alimuachia Mkapa na Mkapa alipostaafu alimuache yeye (Kikwete). Hati hiyo inahifadhiwa na Rais na ndiye mwenye dhamana nayo.

MCHAKATO WA KATIBA
Alisema dhamira yakuanzisha mchakato wa Katiba mpya ni kuwapa Watanzania fursa yakujadili kwa uwazi , kwa kina na kuyatambua matatizo ili yanayohitaji kuingizwa kwenye Katiba yaingizwe.

Alisema ni matumaini yake kuwa Wajumbe wa Bunge la Katiba watatumia vyema fursa hiyp kutunga Katiba iliyo nzuri.

Akizungumzia kitendo cha Umoja wa Katiba ya Wananchi(UKAWA) kususia bunge hilo kwa madai ya kwenda kushtaki kwa wananchi aliusihi urudi bungeni kujadili Rasimu ya Katiba na kuwataka wajumbe kutumia lugha ya staha na kuacha kukejeli waasisi wa Muungano

Amesema hatua ya Ukawa kususa vikao vya bunge na  kwenda kwa wananchi, wakati wake haujafika kwani  kazi ya kujadili Rasimu inafanywa bungeni na sio kwenye mikutano ya hadhara.

 “Nimekitika kusikia wanazunguka nchi nzima kwenda kushitaki kwa wananchi, sijui wanakwenda kushataki jambo gani,” alihoji na kuongeza “napenda kujumuika na watu wengi kuwahisi warudi bungeni.”

Alisema hivi  sasa ni wakati wa kujadili Rasimu na kutunga Katiba mpya ,kazi ambayo inafanyiwa bungeni na sio kwenye mihadhara ya wananchi wasiokuwepo bungeni. “Hawawatendei  haki wananchi waliowachagua na wale wa kundi 201 hawatutendei haki sisi wawili tuliowateua na kuwapendekeza.”

Aliwasisi kuwa wasipoteze fursa hiyo muhimu na kuwaeleza kuwa baada ya bunge kumaliza kazi yake wajumbe wa bunge hilo watatakiwa kwenda kwa wananchi kuwashawishi waunge mkono maamuzi  yao.

“Huko nje waendako siko, na siku yake sio sasa ipo siku watakwenda kwa wananchi ila wakati wake bado.  Hivi sasa ni kwakati wa kujadili Rasimu na kutunga Katiba mpya. Kazi hiyo inayofanywa bungeni na sio kwenye mikutano.” Alisema.

Alisema watu wanajua kuwa Wajumbe wa Bunge la Maalumu wana matatizo na tatizo lao kubwa ni uhusiano miongoni mwao na kwamba ufumbuzi wake wanao wenyewe.

“Kambi hii na kambi hii wakienda kwa wananchi hakuna jawabu,  wananchi hawahusiki na hawana la kuwasaidia…Majawabu ya matatizo yao yako bungeni kupitia mfumo wa bunge walioutengeneza wao wenyewe kupitia kamati zao za uongozi na maridhiano,” alisisitiza.

Alisema wananchi wanajua nani ni nani, nani kasema nini na nani kafanya nini kwa sababu mkutano wao unaonyeshwa moja kwa moja na televisheni. Alisema lugha za matusi  alishawasihi wasiache wakati alipokuwa akilizindua bunge hilo. “Maana hata wakati wanatunga kanuni nanga zinapaa… Tatizo kubwa la wajumbe ni lugha zisizokuwa na staha kwa pande zote mbili.”

Aidha, alisema inahuzunisha na kukasirisha kuona na kusikia wajumbe wanapotukana  waasisi waliounda Muungano wa Tanzania ambapo alisema hali hiyo haikubaliki na kwamba huo sioo uhuru wa kutoa mawazo.

Imeandikiwa na Beatrice Bandawe, Romana Mallya na Beatrice Shayo
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment