WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, January 24, 2013

Pinda:Madaraka ya Rais yapunguzwe



WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda ametaka Katiba Mpya impunguzie Rais madaraka hasa katika nafasi ya uteuzi.
Kauli hiyo ya Pinda inapingana na ile iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue kuhusu Katiba Mpya ambaye aliiambia Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwamba madaraka ya Rais yasiguswe akisema kama atanyang’anywa, atashindwa kuongoza nchi.
Balozi Sefue alisema nafasi ya Rais inapaswa kuwa imara na yenye uwezo wa kuwaunganisha Watanzania wote.
“Asilimia kubwa ya Watanzania, wamekuwa wakipendekeza Rais apunguziwe madaraka aliyonayo, jambo ambalo linaweza kuleta hatari mbeleni, suala hili linatupasa kuwa nalo makini,” alisema Balozi Sefue na kuongeza:
“Tusiwe wepesi wa kutamka maneno bila ya kutafakari hasara na faida zake, tunapaswa kutambua taifa letu lenye miaka 51 ya Uhuru bado maskini, kuna mataifa yenye miaka 200 hadi 400, lakini kamwe hayathubutu kumpunguzia Rais madaraka.”
Hata hivyo, jana Pinda aliiambia tume hiyo ya Mabadiliko ya Katiba: “Kuna haja ya kumpunguzia Rais madaraka kwani amekuwa na mzigo mkubwa wa kuongoza Serikali. Kitu kikubwa ambacho ningependa kiangaliwe kwenye Katiba Mpya kwa upande wa madaraka ya Rais ni katika uteuzi wa viongozi mbalimbali.”
“Nimetaka Katiba Mpya impunguzie mzigo Rais kwani amekuwa na kazi nyingi sasa ni vyema angepunguziwa mzigo huo hasa katika masuala ya uteuzi wa viongozi.”
Pinda alitoa mfano kwamba katika kazi ya uteuzi wa viongozi, Makamu wa Rais anaweza kumsaidia kazi hiyo kwa kushirikiana na vyombo vingine ambavyo Katiba itaviainisha.
Mbali na hayo, Pinda alitaka pia Katiba Mpya izuie wabunge kuwa mawaziri na Serikali za Mitaa ziwekewe mfumo sahihi wa kujiendesha na kuwe na tume itakayoshughulikia masuala ya Muungano, lakini akataka Muungano ubaki wa Serikali mbili.
Jaji Lubuva
Hata hivyo, akitoa maoni yake mbele ya tume hiyo jana, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), Jaji Mstaafu Damian Lubuva alisema kwamba muundo wa Muungano unapaswa kuangaliwa upya kikatiba, ili kuondoa malalamiko yaliyopo kwa muda mrefu.
Alisema suala la dola kwa nchi zilizoungana yaani Tanganyika na Zanzibar linapaswa kutambuliwa ili kila nchi iwe na mamlaka yake kamili.
“Kwa hali ilivyo sasa dola haiko Tanganyika wala Zanzibar, bali iko kwa Tanzania yote. Jambo hili linaleta manung’uniko mengi kwani Zanzibar kama ilivyo kwa Bara inahitaji kuwa na dola kamili.
Napendekeza mfumo wa Muungano ufuate matakwa ya wananchi kutoka kila upande, pia Katiba iainishe mambo ya Muungano ili kuondoa malalamiko kutoka kila upande,” alisema Jaji Lubuva.
Pia alisema Bunge linapaswa kuendelea na wajibu wake wa kutunga sheria na kuisimamia Serikali na siyo kufanya kazi za wizara.
Alisema kwa hali ilivyo sasa, Kamati za Bunge zimekuwa zikitoa maagizo na uamuzi kwa mambo mbalimbali kitu alichosema kuwa siyo sawa kwani hayo ni majukumu ya Serikali.
Jaji Lubuva alisema kitendo hicho kinaweza kudhoofisha utendaji wa Serikali, pia hakizingatii mgawanyo wa madaraka kwa mihimili ya dola.
Alisema Katiba Mpya inapaswa kueleza kwa upana nini maana ya Bunge kuisimamia Serikali, ili kuondoa uwezekano wa Bunge kufanya kazi za Serikali au kuchukua madaraka yasiyo yake.
“Kuhusu misingi ya Katiba nimependekeza Katiba ijayo itambue uwepo wa Mwenyezi Mungu kuwa muumba wa vitu vyote katika sehemu ya mwanzo kabisa ya Katiba. Maneno haya ya kumtambua Mwenyezi Mungu hayawezi kuathiri dhana ya Serikali kuwa haina dini,” alisema Jaji Lubuva.
Aidha, alisema Katiba Mpya inapaswa kutamka kuwa Kiswahili ni Lugha ya Taifa na itatumika katika shughuli zote za kitaifa na katika taasisi mbalimbali za umma na binafsi. Alisema nchi kama Kenya na Uganda zimetamka wazi lugha zao za Taifa katika Katiba hivyo Tanzania nayo haina budi kukitambua Kiswahili kuwa Lugha ya Taifa.
Balozi Karume: Serikali mbili
Balozi Ali Karume amesema Muungano wa Serikali mbili kama ulivyo sasa unatosha. Pia amependekeza nafasi ya Rais wa Zanzibar na ile ya Makamu wa Rais zibaki kama zilivyo.
“Hoja ya Rais wa Zanzibar kuwa Makamu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania siiungi mkono, naona bora ibaki hivyohivyo kama ilivyo sasa asiwe Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu huwezi kujua Rais wa Tanzania akifa na upinzani ukija kuchukua nafasi ?”
Akizungumza muda mfupi baada ya kutoa maoni katika ofisi ya tume hiyo Maisara, Unguja, Balozi Karume alisema katika maoni yake ametaka urais wa Tanzania uwe kwa zamu ndani ya Katiba Mpya.
Imeandikwa na Matern Kayera na Aidan Mhando, Dar na Salma Said, Zanzibar

No comments:

Post a Comment