WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Sunday, January 20, 2013

Mtwara vurugu tupu...viongozi wazomewa


NA MWANDISHI WETU

Wananchi waliojeruhiwa wakiwa wanavuja damu kufuatia vurugu kubwa iliyozuka kati ya wananchi hao na Polisi katika viwanja vya Mashujaa mjini Mtwara jana.
 Watu wawili wamejeruhiwa kwa kufyatuliwa mabomu baada ya polisi mjini hapa kuingilia kati maandamano ya wananchi waliokuwa wakiwafuata wafanyabiashara waliokaidi kufunga biashara zao ili kuhudhuria mkutano wa kukabidhi malalamiko yao kupinga gesi kutoka Mtwara kupelekwa Dar es Salaam.
Malalamiko hayo walikuwa wayakabidhi kwa wabunge wa mkoa huo ambao ni Asnein Murji wa Chama cha Mapindunzi (CCM) na Said Baruani kutoka Chama cha Wananchi (CUF). Hata hivyo, hadi tunakwenda mitammboni Murji alikuwa hajafika eneo hilo la mkutano kwa madai kuwa alikuwa amekwama baada ya gari lake kuharibika.

Aidha, maandamano hayo pia yalikuwa yakielekea ofisi za Shirika la Umeme (Tanesco) mkoani hapa, kupinga kukatika kwa umeme uliokwamisha mkutano wao uliokuwa unafanyika katika Uwanja wa Mashujaa.

Waliojeruhiwa katika vurugu hizo wametajwa kuwa ni wakazi wa Manispaa ya Mtwara Mikindani, Rashid Mohamed na Mustafa Hasan.

Vurugu hizo zilianza baada ya wananchi hao waliokuwa wakitokea Uwanja wa Mashujaa kwa kuwafuata wafanyabiashara wa maduka, hoteli na baa ambao hawakutii amri ya kufunga biashara zao na kujumuika katika maandamano hayo.

Maandamano hayo yalisababisha polisi wa kikosi cha kutuliza ghasia, kuingilia kati na kurusha kufyatua mabomu hayo ili kuwatawanya wananchi waliokuwa wakiwabugudhi wafanyabiashara.
Wananchi hao walisikika wakitoa amri kwa wafanyabiashara ya kuwataka wafunge biashara zao kwa muda na kisha kujumuika kwenye maandamano hayo.

“Funga duka lako…funga baa yako, funga lounge yako…sisi wananchi wa Mtwara twendeni tukatetee gesi yetu… na gesi kwanza uhai baadae…mpaka kieleweke…,” walisikika wananchi hao wakiamrisha wafanyabiashara hao.
Wakazi waliojeruhiwa walisema kuwa walikuwa wakikimbilia gari la aliyewahi kuwa mgombea wa ubunge jimbo la Tandahimba kwa tiketi ya CUF, Katani Ahmed Katani, kwa ushabiki wa kumfurahia kiongozi huyo ambae kwa madai yao ni mwanamapinduzi wa kutetea rasilimali gesi .

“Sisi tulikuwa tukilifuata gari la Katani huku tukimfurahia Katani…na sio kama tulikuwa tukifanya fujo ila cha kushangaza jeshi la polisi liliamua kutufyatulia mabomu miguuni na angalia jinsi tulivyoumia…,” alisema mmoja wa majeruhi hao.

Majeruhi hao walikimbizwa katika hospitali ya Mkoa wa Ligula na hali zao zinaendelea vizuri.

Kamanda wa polisi Mkoa wa Mtwara, Maria Nzuki, alipoulizwa kwa njia ya simu ya mkononi kuhusu watu hao kujeruhiwa, alikana kuwepo kwa tukio hilo na kukata simu yake.

DC, VIONGOZI WA CCM (W) YA NACHINGWEA WAZOMEWA.
Wakazi wa mji mdogo wa Nachingwea, mkoani Lindi, wamewazomea viongozi watatu wa wilaya hiyo, akiwemo mmoja wa Serikali na wawili wa kisiasa kwa madai ya kutoridhishwa na ushawishi wao wa kuwataka wasiwaunge mkono wananchi wa mkoa wa Mtwara, wanaopinga mpango wa Serikali wa kuisafirisha gesi kwenda Dar es salaam.

Viongozi waliokumbwa na zomeazomea hiyo ni mkuu wa wilaya hiyo, Reginal Chonjo, Mwenyekiti wa CCM, Albert Mnali na mjumbe wa Halmashauri kuu ya Taifa ya Chama hicho, Fadhili Liwaka.

Tukio hilo limetokea mwanzoni mwa wiki hii, kwenye mkutano wa hadhara ulioitishwa na viongozi hao uliofanyika viwanja vya kituo cha mabasi cha mji mdogo wa Nachingwea.

Wakiwa wanahutubia umati mkubwa wa watu katika eneo hilo, kwa nyakati tofauti viongozi hao, waliwataka wananchi wa wilaya hiyo, kutowaunga mkono mgogoro wa gesi unaoendelea mkoani humo, kwa madai kwamba hauna maslahi kwa wakazi hao.

Zomeazomea hiyo, ilikuja muda mfupi, baada ya Mkuu wa wilaya hiyo kusimamana kuanza kuhutubia huku akiwataka kutojiingiza kwenye maandamano yanayoandaliwa hivi karibuni katika miji ya Mtwara na Lindi, kuishinikiza Serikali kutoihamisha gesi iliyogundulika mkoani Mtwara.
Katika mkutano huo Chonjo alisema wakazi wa wilaya ya Nachingwea hawana sababu ya kushiriki migogoro hiyo, kwa madai kwamba tangu awali wananchi hao wamekuwa wanatumia raslimali zilizo nje ya wilaya na mkoa wao wa Mtwara.

Mkuu huyo wa wilaya ya Nachingwea, alizitaja baadhi ya raslimali ambazo wana Mtwara wanazitumia kutoka nje ya maeneo yao kuwa ni pamoja na umeme na barabara ya Kibiti hadi Lindi, ambao ujenzi wake umetokana na raslimali alizodai ni za nchi nzima.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments:

Post a Comment