WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, January 25, 2013

CHADEMA inakua, CCM inasinyaa, lakini kwa kasi ndogo!


UCHAGUZI katika kata 29 umehitimishwa wiki iliyopita, na matokeo kujulikana ambapo Chama cha Mapinduzi (CCM) kimeshinda katika kata 22 (75.8%), CHADEMA kata 5 (17.2%), huku TLP na CUF wakishinda katika kata moja moja (3%).
Kwa tathmini ya juu juu, ni rahisi kufikia hitimisho kwamba CCM kimeshinda kwa kishindo na kuwagaraza vibaya wapinzani wao, na hasa mahasimu wakubwa kisiasa, CHADEMA. Aidha kwa matokeo haya, viongozi, wanachama na wapenzi wa CCM watarukaruka kwa furaha wakishangilia si ushindi tu, lakini kile kinachoonekana kuwa ni kuendelea kupendwa pamoja na kwamba chama chao kimevurunda vibaya katika kila nyanja.
Matokeo haya pia yanaweza kuwanyong’onyesha baadhi ya viongozi, wanachama na wapenzi wa CHADEMA, kwamba pamoja na juhudi zote walizofanya katika kampeni, na muonekano wa nje wa kuchokwa kwa CCM, wameweza kuambulia kata tano tu!
Matokeo haya pia yana hatari kisaikolojia kwa upande wa upinzani. Hii ni kwa sababu wananchi wapenda mabadiliko wanaweza kurudi nyuma wakiamini kwamba kama kwa mazingira ya sasa CCM inaweza kushinda uchaguzi kwa kiwango cha asilimia 75, basi pengine chama hiki haking’oleki kutoka madarakani, na hivyo kuanza kuwa na mtazamo wa ‘kukubali yaishe’.
Hata hivyo, katika kufanya tathmini ya matokeo ya uchaguzi huu ni muhimu kuelewa vizuri mantiki ya uchaguzi mdogo kabla ya kufikia hitimisho. Mantiki ya uchaguzi mdogo ni fursa ya kutetea ushindi uliopata katika uchaguzi uliopita na kujipima nguvu upya kwa chama ambacho kilishindwa katika uchaguzi huo.
Kwa hivyo, unapofanya tathmini ya matokeo katika uchaguzi mdogo jambo la kwanza la kuangalia ni je vyama shindani vimeweza kutetea viti walivyokuwa navyo awali?
Ndiyo maana katika chaguzi za namna hii vyama vilivyoshinda awali hupigana kufa na kupona kama tulivyoona CCM ilivyopambana katika chaguzi za Igunga na Arumeru Mashariki. Ndivyo vile vile tutakavyoona jinsi CCM itakavyopigana katika Jimbo la Sumbawanga na ambavyo CHADEMA itapigana katika Jimbo la Arusha Mjini kama uchaguzi utarudiwa pia katika jimbo hili.
Sasa katika uchaguzi wa kata hizi 29 ni muhimu kukumbuka kuwa CCM ilikuwa imeshinda katika kata 26, CHADEMA kata mbili na TLP kata moja. CHADEMA na TLP wamefanikiwa kutetea kata zao walizoshinda awali huko Rombo na Mtibwa (CHADEMA) na Kilema (TLP). Zaidi ya kutetea kata zake ilizoshinda awali, CHADEMA pia wameongeza kata nyingine tatu za Daraja Mbili huko Arusha, Ipole huko Tabora na Malangali huko Ludewa, Iringa.
Ndiyo kusema, kitakwimu, CCM wamepoteza ushindi walioupata awali kwa asilimia 15.4 na CHADEMA wameongeza ushindi walioupata awali kwa asilimia 150! Kwa hiyo, kwa lugha ya kitakwimu, hakuna shaka kwamba CHADEMA wamepanda na CCM wameshuka.
Namna nyingine ya kuangalia matokeo haya kitakwimu ni idadi ya kura ambazo vyama hivi viwili wamepata. Katika ujumla wake, CCM wamepata kura 29,558 na CHADEMA wamepata jumla ya kura 20,884, ambayo ni tofauti ya kura 8,710 ambayo ni sawa na asilimia 17.3. Hii si tofauti ya kura ambazo CCM wamekuwa wakijivunia huko nyuma. Hii maana yake ni kwamba CCM hawawezi tena kushinda uchaguzi wowote kwa kishindo, na hiyo ni hatua muhimu katika kuelekea kifo chake.
Hata hivyo, kihesabu ni kwamba CCM wamepoteza viti vinne tu dhidi ya vile walivyoshinda awali, na CHADEMA wameongeza viti vitatu pekee. Kwa hiyo kwa mantiki ya kihesabu ushindi wa viti vitatu ni mdogo mno ukilinganisha na mvuto ambao CHADEMA inayo sasa hivi kwa jamii ya Watanzania. Vile vile kupoteza viti vinne kati ya viti 26 vya awali sio jambo la kutisha kwa chama kilichochokwa kama CCM.
Hivyo hitimisho ambalo tunalipata kwa matokeo haya ya udiwani ni kwamba CHADEMA inakua na CCM inasinyaa, lakini kwa kasi ndogo. Kwa kasi hii ya ukuaji wa CHADEMA na kusinyaa kwa CCM inaweza ikachukua muda mrefu wa kuing’oa CCM madarakani kuliko ‘wapenda mabadiliko’ walivyofikiria.
Wapenda mabadilikonina maanisha wale Watanzania wanaoamini kwamba CCM ni kikwazo katika jitihada zetu za kujiletea maendeleo ya dhati na katika kujenga taifa linalokua kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiutamaduni, na hasa taifa linalokumbatia demokrasia na utawala wa sheria kiukweli na kiuhalisia. Binafsi siamini hata kidogo kwamba inawezekana taifa letu likayafikia mambo haya kama CCM itaendelea kuwa madarakani.
Funzo tunalolipata katika matokeo haya ni kwamba mvuto na kura si lazima viendane, hasa katika mazingira ambamo wapiga kura wachache hujitokeza kwenda vituoni kupiga kura.
Chama cha siasa hupitia hatua kuu nne katika kufikia hatua ya kushinda uchaguzi. Hatua ya kwanza ni ya kisheria ambapo chama kinatambulika kisheria kwa kusajiliwa rasmi na kuruhusiwa kufanya shughuli za kisiasa.
Hatua ya pili ni kujulikana kwa wapiga kura, kwamba kuna chama cha siasa na kina viongozi fulani. Juhudi za viongozi katika kukiuza chama chao hukifisha chama hicho katika hatua ya tatu ambayo ni ufuasi. Ufuasi wa chama cha siasa huonekana katika mazungumzo ya kila siku ya wananchi na kwa jinsi wananchi hao wanavyoitikia mikutano na shughuli nyingine za umma kama vile kukichangia chama hicho.
Hatua ya mwisho ni kubadilisha idadi fulani ya wafuasi kuwa wafia chama, ambao ndio wanaoweza kukipatia chama ushindi, hasa katika mazingira makali ya ushindani.
Kwa sasa hivi hakuna shaka kwamba CHADEMA wameweza kupata wafuasi wengi kama inavyoonekana katika mazingira mbalimbali. Katika mazungumzo ya kila siku linapokuja suala la siasa unaona hamasa ya Watanzania kwa CHADEMA.
Kwa wale waliowahi kusafiri na gari mpya za CHADEMA (M4C) watakumbuka jinsi ambavyo wananchi huhamasika barabarani mara wazionapo gari hizi kwa kuonyesha vidole viwili. Madereva wa malori na mabasi ya abiria hawasiti kupiga honi mara wazionapo gari hizi, na hata baadhi ya askari wa barabarani hudiriki kuonyesha vidole viwili mara wazionapo gari hizi zikipita.
Mikutano ya CHADEMA imebadilika kabisa kutoka enzi za akina Mzee Mtei kuhutubia ‘miti’ na sasa mikutano hiyo ikijaza maelfu kwa maelfu ya wananchi waliojaa hamasa na hamu kubwa ya mabadiliko.
Hata hivyo, bado CHADEMA hawajifikia hatua ya nne, ambayo ni muhimu sana katika kujihakikishia ushindi. Hatua hii ni ile ya kupata wafia chama. Ili kujihakikishia ushindi ni muhimu kabisa chama cha siasa kiwe na wanachama wafia chama.
Hawa ni aina ya wanachama ambao watakipigia kura wakati wowote iwe mvua, iwe jua. Hili ni kundi muhimu sana kujihakikishia ushindi katika mazingira ambayo wananchi wengi hawajitokezi kupiga kura, ambalo limeanza kuwa jambo la kawaida katika chaguzi zetu.
Ni kundi hili ndilo ambalo limebaki kama mpira wa kupumulia kwa CCM. Hawa ni watu ambao hawatakuja kamwe kugundua ubaya wa CCM hadi kitakapotoka madarakani na ni kundi hili ambalo limeiwezesha CCM kushinda katika uchaguzi wa madiwani uliokamilika wiki jana, ambapo katika baadhi ya kata idadi ya wapiga kura waliojitokeza walikuwa chini ya asilimia 20.
Nahitimisha kwa kutoa wito kwa wapenda mabadiliko. Kwamba kupenda na kutamani tu mabadiliko hakutoshi, inabidi kushiriki katika kuyasaka hayo mabadiliko. Tabia ya baadhi ya wapenda mabadiliko kudhani kwamba kikundi fulani cha watu katika chama fulani ndio wenye jukumu la kuleta mabadiliko itatufanya tukae katika mfumo wa utawala tuliouchoka kwa muda mrefu.
source Raia Mwema: Kitila Mkumbo

No comments:

Post a Comment