WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Tuesday, January 29, 2013

Hatari: Wasichana wauzwa kama njugu


NA THOBIAS MWANAKATWE

  Mawakala wakunja Dola 5,000 kwa kichwa
  Kwa siku wanapita hadi wanane bandarini
Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka

Biashara ya binadamu imeibuka kwa kasi nchini na kutishia usalama wa nchi kutokana na watoto wenye umri kati ya miaka 8-15 baadhi yao wakiwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari  kusafirishwa kinyemela kwenda katika nchi za Uarabuni.

Uchunguzi wa kina uliofanywa na NIPASHE kwa takribani wiki mbili, umebaini kuwa biashara hiyo imeibuka kuanzia Desemba mwaka jana na imeshika kasi Januari mwaka huu na wanaosafirishwa  wengi ni watoto wa kike kutoka mikoa mbalimbali nchini. Wapo wachache wa kiume pia.

Kamanda wa Polisi Kikosi cha Maji, Mboje Kanga, alipoulizwa na NIPASHE alithibitisha kupata taarifa za kuwapo kwa biashara hiyo ingawa alisema kuwa hana takwimu za watoto ambao wamekamatwa wakitaka kusafirishwa.

“Tatizo la kusafirisha watoto lipo, lakini nina watu ambao wanashughulikia suala hilo pale bandarini, nitafute kesho (leo) nitakupa takwimu zote kuhusiana na biashara hiyo baada ya kuwasiliana na watu wangu,” alisema Kamanda Kanga.

Uchunguzi zaidi wa gazeti hili umebaini kuwa mikoa ambayo watoto hao wananunuliwa na mawakala maalum kabla ya kusafirishwa kupelekwa nchi za Uarabuni kufanya kazi mbalimbali zikiwamo za ndani ni Mtwara, Lindi, Manyara, Pwani, Tabora, Ruvuma, Tanga na Shinyanga. 

Taarifa zinaonyesha kuwa mawakala hao wakishafanikiwa kuwapata watoto hao kutoka katika mikoa hiyo huwapeleka Jijini Dar es Salaam na baadaye kusafirishwa kwa usafiri wa majini kutoka Bandari ya Dar es Salaam kwenda Zanzibar.

Uchaunguzi umebaini kuwa watoto hao wakifikishwa Zanzibar hukutanana watu maalum ambao huwapokea na kufawanyia mipango ya kuwasafirisha kwa usafiri wa ndege au wa majini kwenda Uarabuni ambako hutumikishwa katika kazi mbalimbali.

Mawakala hao wakishafanikiwa kuwasafirisha kutoka Bandari ya Dar es Salaam, hulipwa wastani wa Dola za Marekani 5,000 (Sh. milioni 8) kwa kila mtoto wanayefanikisha kumvusha kutoka Tanzania Bara kwenda Zanzibar.

Kwa mujibu wa uchunguzi huo, ili kuhalalisha safari za kuwasafirisha watoto hao, mawakala wanakula njama na baadhi ya wenyeviti wa serikali za mitaa kwa kuandika barua zinazoelezea sababu za watoto hao kwenda Zanzibar.

Barua hizo ambazo imebainika ni za kughushi, nyingi zinaandikwa na kupigwa mihuri ya wenyeviti wa serikali za mitaa wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, jijini Dar es Salaam.

“Tunaomba mtoto huyu asitiliwe mashaka (shaka) bali apewe ushirikiano, anasafiri kwenda Zanzibar kusalimia ndugu zake walioko huko ambao watampokea,” inaeleza sehemu ya barua hizo ambazo NIPASHE ilifanikiwa kuona nakala yake.

Kutokana na biashara hiyo kushika kasi, wastani wa watoto kati ya watano hadi 10 hufika katika Bandari ya Dar es Salaam kwa ajili ya kusafiri kwenda Zanzibar kila siku.
Hata hivyo, askari wa kikosi cha maji (Police Marine) ambao wamekuwa wakilinda hali ya usalama wa usafiri bandarini hapo tangu mwanzoni mwa Januari mwaka huu, wameanza kushtukia kasi ya watoto kusafiri kwenda Zanzibar na hivyo wanachukua hatua za kuwakamata na kuwazuia kusafiri.

Polisi hao wanashtukia safari za watoto hao ambao wengi huvalishwa mavazi ya hijabu kwa sababu wengi wanakuwa hawana nyaraka za kutosha zinazoelezea sababu za safari zao, barua za wenyeviti wa serikali za mitaa kuwa za kughushi na kutokuwa na watu wa kuwasindikiza bandarini.

Uchunguzi zaidi umebaini kuwa mawakala kazi yao kubwa wanayoifanya ni kuwatafuta kutoka mikoani na kuwapeleka Dar es Salaam na wakishawafikisha wanafanya njama za kupata barua kutoka kwa wenyeviti wa serikali za mitaa na baada ya kukamilisha mchako huo huwapeleka bandarini na kuwapa maelekezo ya namna ya kufanikiwa kusafiri kwenda Zanzibar wakiwa peke yao.

Watoto hao wakishafikishwa bandarini, wale ambao wanakwama kusafiri baada ya kutiliwa shaka na polisi, mawakala hupanga njama na baadhi ya polisi kwa kuwapa kitu kidogo ili waruhusiwe kusafiri.

Aidha, uchunguzi umebaini kuwa Januari 23, mwaka huu waliotiliwa shaka na polisi na kuzuiwa kusafiri ni watoto wanne ambao walifunguliwa jalada la upelelezi kituo cha Polisi Maji ambazo ni MUD/RB/40/2013 na MUD/RB/36/2013.

Watoto hao majina tunayasitiri kwa sasa kwa sababu za kimaadili wana umri wa miaka 14 na 15 wote kutoka kijiji cha Nakapanya Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma; mmoja mwenye umri wa miaka minane anatoka mkoa wa Tabora; wakati mwingine wa kiume mwenye umri wa  miaka 15 anatoka kijiji cha Mkangula Mkoa wa Mtwara, ilahali  mwenzake kutoka kijiji cha  Mbembaleo mkoani Mtwara ana umri wa miaka 14.

Januari 25, mwaka huu watoto waliokamatwa bandarini wakitaka kusafiri kwenda Zanzibar ni binti mwenye umri wa miaka 13 kutoka kijiji cha Manoro Wilaya ya Lushoto Mkoa wa Tanga; mvulana mwenye umri wa miaka 13 kutoka Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma na binti mwenye umri wa miaka 12 kutoka Tunduru Mjini. 

Wengine ni binti mwenye umri wa miaka 14 kutoka kijiji cha Namalumbusi Wilaya ya Masasi Mkoa wa Mtwara, mvulana mwenye umri wa miaka 12 kutoka Mkoa wa Manyara na mvulana mwingine mwenye umri wa miaka 10 kutoka Wilaya ya Nachingwea Mkoa wa Lindi.

Watoto waliokamatwa Januari 26, mwaka huu binti mwenye umri wa miaka 12 kutoka kijiji cha Ndanda Mkoa wa Mtwara; binti mwenye umri wa miaka 13 kutoka kijiji cha Mteruka wilayani Nachingwea Mkoa wa Lindi na mwingine mwenye umri wa miaka 13 kutoka kijiji cha Mnazi mmoja Mkoa wa Mtwara.

Wengine ni binti (13) kutoka kijiji cha Mnazi Mmoja mkoani Mtwara, binti (14) kutoka Mkoa wa Manyara na binti (17) ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha tatu kutoka kijiji cha Kokoro wilayani Kishapu Mkoa wa Shinyanga. 

Januari 27, mwaka huu alikamatwa binti (14) mkazi wa Manispaa ya Iringa mkoani Iringa.
Taarifa kutoka ndani ya kituo cha kikosi cha Polisi Maji, zinaeleza kuwa watoto hao wakishakamatwa na kuzuiwa kusafiri, wamekuwa wakichukuliwa maelezo na baadaye kuachiwa warejee walikotoka, lakini wengine hushindwa kurejea kutokana na kukosa nauli hivyo mawakala kupanga njama za kuwasafirisha kinyemela.

“Tukishawakamata tukawahoji tunawaachia kwa sababu hatuwezi kuendelea kukaa nao hapa wakati hatuna pesa za kuwalisha chakula,” alisema askari mmoja ambaye aliomba jina lake lisitajwe kwa kuwa siyo msemaji wa jeshi.

Baadhi ya watoto waliozungumza na NIPASHE, walisema kuwa mawakala walizungumza na wazazi wao na kukubaliana kuwa wanakwenda kuwatafutia kazi Dar es Salaam na hivyo kuwaruhusu kufuatana nao bila kueleza kuwa wanawapeleka nje ya nchi.

Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka, alipoulizwa juu ya suala hilo, alisema alipata taarifa za kushamiri kwa biashara hiyo kupitia kwa maofisa wa Uhamiaji waliopo uwanja wa ndege jijini Dar es Salaam.

Alisema kuwa alielezwa kwamba kuna watoto wanawakamata uwanja wa ndege wakitaka kusafirishwa kwenda nje kufanya kazi na baada ya hapo serikali kupitia wizara hiyo iliandika barua kwa Wakala wa Huduma za Ajira Tanzania (Tahesa) kutoa maelekezo ya namna ya kupata ajira nje ya nchi.

“Hili suala la watoto kuanza kusafirishwa kwenda nje kupitia bandari ya Dar es Salaam naliona ni jipya kwangu, isipokuwa taarifa ambazo wizara ilizipata ni kwamba watoto hao walikuwa wakisafirishwa kwenda nje kwa ndege, lakini baada ya kudhibiti hivi sasa suala hilo limepungua,” alisema Kabaka.

Hata hivyo, alisema baada ya kupata taarifa hizo atafuatilia haraka polisi wa bandari ili hatua zichukuliwe na kwamba wananchi wasaidie kutoa ushirikiano kwa serikali ili mawakala wanaofanya kazi hiyo wafahamike.

“Kwanza nikupe hongera sana kwa kuonyesha uzalendo na kuibua suala hili, nakuhakikishia serikali itafutailia kwa karibu sana na kukomesha biashara hiyo,” alisema Kabaka.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philip Mulugo, alisema wizara yake haina taarifa za wanafunzi kusafirishwa kwenda nje kutafutiwa kazi na kuahidi kulifanyia kazi haraka.

“Jambo hili kwanza limenishtua sana kama wapo wanafunzi ambao kweli wanasafirishwa kwenda nje tutapenda tufahamu wanatoka shule zipi ili tufahamu je, wakuu wa shule husika wana taarifa gani za wanafunzi hao?” alisema Mulugo.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba, alisema wizara yake haina taarifa za kuwapo kwa biashara hiyo na kwamba atawasiliana na Wizara ya Kazi na Ajira ili kupata taarifa kama wanalifahamu.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment