WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Sunday, April 21, 2013

Wabunge na utajiri wa maskini usioonekana

3 4f803

Uchumi mnao, lakini mmeukalia!" – Julius Nyerere.
Bunge la Bajeti linaendelea kule Dodoma. Kwa mengine tunayoyaona yakitokea ndani ya Bunge wakati mwingine unawaza na kujiuliza; hivi ni Bunge la Wanasiasa au Bunge la Wananchi?

Maana, waliomo ndani bungeni wametumwa na wananchi. Inakuwaje basi, wanatumia muda mwingi pia kujadili mambo yasiyo na masilahi kwa wananchi? Watanzania wengi wana hali mbaya za kiuchumi. Wanataka kupiga hatua za maendeleo ya kiuchumi. Wanahitaji sana kuona yanazungumzwa masuala ya msingi kwa maendeleo yao.

Pia kauli ya ' Uchumi mnao, mmeukalia!' Inanikumbusha utotoni pia. Nilipata kusikia redioni kauli hii ya Mwalimu . Tulipokuwa shuleni tulifundishwa na hata kuimba kwamba ili tuendelea tunahitaji vitu vinne; Watu, Ardhi, Siasa safi na Uongozi bora.

Ni dhahiri kwamba, watu tunao, tena wengi sana. Ardhi tunayo, tena kubwa sana. Hivyo viwili nilivyovitaja ndiyo mtaji mkubwa tulio nao. Huo ndiyo utajiri wa maskini, lakini hauonekani. Huenda kinachokosekana ni Siasa safi na Uongozi bora katika kuuendeleza mtaji tulio nao. Kuna Mtanzania mwenzetu aliyebainisha kuwa mtaji wa maskini ni nguvu zake mwenyewe. Labda nyongeza hapa ni kuwa; mtaji wa nchi ni watu wake wenyewe.

Nchi kupitia vyanzo vyake vya mapato, siasa safi na uongozi bora na zaidi utawala bora, vina wajibu wa kujenga misingi ya jamii bora. Jamii bora ni ishara ya kuwepo kwa taifa bora. Taifa bora ni taifa lenye nguvu. Hilo litafanikiwa kama dola itaweka kipaumbele katika kuwaendeleza watu wake. Muhimu na la kwanza kabisa ni kuwekeza katika elimu. Huko ni kuuendeleza mtaji muhimu kwa maendeleo ya taifa.

Angalia hapa, wasichana hawa wenye kupata mimba na kufukuzwa shule ndiyo sehemu ya makabwela tunaotaka kuwawezesha. Hawa ndiyo wazazi wa kesho. Kuwapa nafasi ya pili katika maisha yao angalau tu wamalizie elimu yao ya shule ya msingi ni moja ya njia za kuwawezesha wanawake hawa ili nao waje kuwa walezi bora wa watoto wao ambao pia ni taifa la kesho.

Hebu tujikite zaidi kwenye elimu. Ni ukweli, kuwa Serikali kwa kupitia mpango wake wa MMEM (Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi) ilifanikiwa katika ujenzi wa madarasa mapya katika sehemu mbalimbali. Lengo pia ni kuwashirikisha wananchi katika masuala ya elimu.

Hata hivyo, kuna ugumu mkubwa katika hili, kwani wengi wa wananchi ambao Serikali inataka kuwashirikisha, nao pia wana kiwango kidogo kabisa cha elimu ikiwamo ujinga wa kutokujua kusoma, kuandika na kuhesabu.

Ili mipango ya Serikali iwe na mafakinio ya muda mrefu, kunahitajika pia kuwepo na mpango wa kuimarisha Elimu ya Watu Wazima. Wazo hapa ni kuwepo kwa Mpango wa Kuendeleza Elimu ya Watu wa Wazima (Mkewawa).

Visheni ya Serikali ya kuondoa umaskini ifikapo mwaka 2025 haiwezi kufanikiwa endapo hakutakuwepo na visheni ya kuondoa ujinga wa kutokujua kusoma na kuandika sambamba na kampeni ya kuondoa umaskini.

Kwa vile zaidi ya asilimia 80 ya watu wa nchi hii wanaishi vijijini na kwamba kilimo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wetu, kamwe hatuwezi kupiga hatua za haraka za maendeleo, endapo idadi kubwa ya watu wetu na hususan waishio vijijini watazidi kuzama kwenye bahari ya ujinga wa kutokujua kusoma na kuandika.
 
Kuufuta ujinga wa kutokujua kusoma na kuandika miongoni mwa watu wetu iwe ndiyo hatua ya kwanza katika kampeni za kuondoa umaskini. Hapa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima(TEWW) kupitia Vyuo Vya Maendeleo ya Wananchi ingeweza kushiriki kikamilifu katika Mpango wa Kuendeleza Elimu ya Watu Wazima kwa kutoa mchango mkubwa katika kuendesha kampeni za kufuta ujinga na kuwandeleza wananchi kielimu katika hatua ya utu uzima
 
source: Mjengwa Blog

No comments:

Post a Comment