WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Wednesday, April 10, 2013

Uchambuzi Wa Habari; Viboko Mashuleni Au La, Ni Mjadala Wa Aibu!

3 05e57


Ndugu zangu ,

Moja ya habari kubwa leo ni hii;

“Serikali imesema itarudisha adhabu ya viboko kwa wanafunzi shuleni ili kujenga nidhamu na kujituma.Akizungumza Dar es Salaam jana wakati akizindua tovuti ya www.shledirect.co.tz inayowezesha wanafunzi kujisomea kwa njia ya mtandao, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo ilisema kuondolewa kwa adhabu ya viboko shuleni kumewafanya wanafunzi wengi kukosa nidhamu na wakati mwingine kujifanyia mambo kienyeji.

“Wasipotandikwa mambo hayaendi, nilipokuwa mwalimu mkuu nilikuwa nawatandika kweli ndiyo maana shule yangu ilikuwa ikiongoza Mkoa wa Mbeya hivihivi hawaendi...” alisema huku akishangiliwa na wageni waalikwa.” ( Mwananchi, Aprili 9, 2013)

Nionavyo;

Tunarudi nyuma miaka 50 badala ya kwenda mbele. Kuna wengi kama mimi tusioamini, kuwa, kumchapa mwanafunzi bakora ni kumsaidia kujenga nidhamu na kujituma.

Kinyume chake, kama ni nidhamu, utamjengea nidhamu ya woga na kufanya yale ambayo anadhani unataka ayafanye na si kuwa ayafanye kwa faida yake na jamii hapo baadae.

Viboko vinamfanya mwanafunzi asijiamini na hata akose uwezo wa kudadisi. Bado nakumbuka, kuwa nikiwa Darasa la Tano ilinitokea nikachapwa bakora darasani kwa kosa la ‘ kumdadisi sana mwalimu’. Mimi nilitaka kupata ufahamu zaidi lakini mwalimu aliniona nimekosa nidhamu.

Habari hiyo ya kwenye Mwananchi inazungumzia mpango wa kurudisha sheria ya adhabu ya viboko wakati kimsingi watoto wetu wanachapwa viboko mashuleni kila kukicha.

Wanafunzi kukosa nidhamu na kutokufanya vizuri kwenye masomo inachangiwa na mambo mengi. Tuanze kuyaangalia hayo kwanza kabla hatujawahamasisha walimu wakate bakora za miti ya mipera kuwachapa watoto wetu.

Na kwa Waziri mwenye dhamana kuonyesha kushabikia watoto kuchapwa bakora si kitu kingine bali ni jambo la kusikitisha sana. Na mjadala wa kama watoto tuwachape bakora au la, katika wakati tulio nao, ni mjadala wa aibu- A shameful debate!

Maggid Mjengwa,

Iringa.

No comments:

Post a Comment