WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Monday, April 8, 2013

Mkapa atema cheche; ataka viongozi wafuate misingi ya Nyerere

 
Na Phinias Bashaya,

 Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa amesifia utawala wake kwa kuongoza taifa bila ya kubaguana na amesikitishwa na matukio ya udini, ambayo yanaashiria kuvuruga amani na utulivu wa Tanzania katika siku za karibuni.

Akitoa salamu zake baada ya kusimikwa kwa Askofu Mpya wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Desdelius Rwoma, Mkapa alisema anachojivunia ni kuheshimiwa na waumini wa madhehebu yote.

“Katika kipindi cha uongozi wangu, viongozi wa madhehebu yote walikuwa wakinisisitizia kuwa sisi sote ni ndugu pamoja na tofauti zetu za kiimani. Wakati wa utawala wangu nilijitahidi kwa uwezo wangu wote kuwahudumia wananchi bila kuwepo kwa malalamiko ya kubaguana katika jamii,” alisema Mkapa, ambaye aliiongoza Tanzania kuanzia mwaka 1995-2005.

Mkapa alionya kuwa taifa limeacha misingi aliyoiacha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ambaye mara zote alisimamia umoja wa taifa.

“Wakati wa utawala wangu nilijitahidi kwa uwezo wangu wote kuwahudumia wananchi bila kuwepo kwa malalamiko ya kubaguana katika jamii,” alisema.
Mkapa ambaye hakupanga kuongea lolote katika tukio hilo, alitaka taifa lijenge utamaduni wa kupendana, huku akilaumu kuwa kizazi kipya cha uongozi kimeanzisha mambo ya ajabu ya kukosa upendo na kudhalilishana.

Pia alitahadharisha kuwa zama hizi kumeibuka mitafaruku mbalimbali na kuwakumbusha Watanzania kuwa ni wakati wa kumwabudu Mwenyezi Mungu.
Mkapa alisema mara nyingi alishauriana na viongozi wa dini katika masuala ya kijamii na kiroho na kumtaja askofu mpya wa Bukoba, Rwoma na Mtangulizi wake aliyestaafu Nestory Timanywa kuwa alishirikiana nao katika masuala ya wananchi. Onyo la Mkapa limekuja siku chache baada ya Rais Jakaya Kikwete kukemea mambo ya kidini na kutetea Serikali yake haiongozi kwa misingi ya ubaguzi.

Katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi, Rais Kikwete alikwenda mbali zaidi na kudai amekuwa akilalamikiwa na viongozi wa madhehebu ya Kikristo na yale ya Kiislamu.

Maneno ya Mkapa na Kikwete yamekuwa katika kipindi hiki taifa likiwa limetikiswa na matukio yenye mwelekeo wa chuki za kidini. Matukio makubwa yakiwa yale ya kuuawa wa Padri Evarist Mushi huko Zanzibar na Mchungaji Mathayo Kachila wa Geita.
Pia kupigwa risasi kwa Padre Ambrose Mkenda na kumwagiwa tindikali kwa Sheikh Fadhil Soraga na vurugu za mambo ya kuchinja huko Geita na Tunduma.

Askofu Mpya wa Bukoba Rwoma alimshukuru Mkapa kwa kuzungumzia umuhimu wa amani ya nchi, huku akisisitiza suala la upendo miongoni mwa wananchi.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu Mstaafu Fredrick Sumaye jana alitaja vyanzo vya vurugu zinazoendelea nchini kuwa unatokana na tofauti kubwa kati ya walionacho na wasionacho.

Alitoa kauli hiyo jana wakati akizindua santuri ya nyimbo za dini kwa Kwaya ya Mt Joseph, Mfanyakazi ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).

Sumaye alionya kuwa kama hali ya utajiri kwa baadhi ya watu itaachwa na kuendelea hivyo, ni wazi kuwa nchi haitatawalika kwa amani.
 
“Binadamu mwenye njaa na aliyekata tamaa kamwe hawezi kutawalika kwani kila wakati anahisi kutengwa na kundi jingine,” alisisitiza Sumaye.
 
source: Mwananchi

No comments:

Post a Comment