WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, December 19, 2013

Maskini Zitto Kabwe Chadema

Zitto Kabwe
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimesema hakitashughulikia rufaa iliyokatwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, kwa Baraza Kuu kupinga uamuzi wa Kamati Kuu (CC) wa kumvua nyadhifa zake katika chama, hadi hapo itakapopitia utetezi wake na kuamua hatima ya uanachama wake katika chama hicho.
Pia kimethibitisha kupokea utetezi dhidi ya mashitaka 11 yanayohusisha usaliti dhidi ya chama na kuwachafua viongozi wakuu kupitia waraka wa mabadiliko.

Mashtaka hayo yanamkabili Zitto, pamoja na aliyekuwa Mjumbe wa CC, Dk. Kitila Mkumbo na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba.
Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema, Victor Kimesera, alisema hayo alipozungumza na NIPASHE, ofisini kwake, jijini Dar es Salaam jana.

Kimesera, ambaye ni Katibu Mtendaji Ofisi ya Katibu Mkuu wa Chadema, alisema rufaa hiyo ni kitu kidogo, hivyo haiwezi kuanza kushughulikiwa na chama katika sakata la Zitto na watuhumiwa wenzake.

“Kuna (kitu) kikubwa cha mbele yake (rufaa),” alisema Kimesera akijibu swali la NIPASHE lililotaka kujua nini kinaendelea kwenye chama baada ya Zitto kukata rufaa.
 Kimesera alisema kitu kikubwa kuliko rufaa, ambacho kitaanza kushughulikiwa na chama ni maelezo ya utetezi wa Zitto na watuhumiwa wenzake.

Alisema hiyo ni kwa sababu tayari kuna hoja ya CC, ambayo inataka ijiridhishe kama Zitto na wenzake waendelee kuwa uanachama au la.

 Kwa mujibu wa Kimesera, baada ya Zitto na wenzake kuwasilisha utetezi wao, CC itaitishwa na kuyapitia na kisha itatoa maamuzi juu ya uanachama wao.
“Sasa huwezi kuongea juu ya rufaa wakati hujajua uanachama wao kwanza,” alisema Kimesera.

 Hivyo, alisema rufaa ya Zitto itaendelea kuhifadhiwa kwenye jalada hadi hapo hatua ya kwanza ya kupitia maelezo yao ya utetezi na kuyatolea maamuzi itakapochukuliwa. “Lazima twende kwa hatua. Kwa hiyo, hiyo (rufaa) imekaa,” alisema Kimesera.

 Mwanasheria wa Zitto, Albert Msando, alitaja sababu mbili za mteja wake kukata rufaa kuwa ni kukiukwa kwa taratibu za kuchukua hatua za nidhamu na sababu zilizotolewa kutokuwa sahihi.

Msando alitaja kifungu cha 6.5.6 cha Kanuni ya Uendeshaji ya chama hicho, akisema utaratibu uliotakiwa kufuatwa kabla ya kumchukulia hatua za kinidhamu kiongozi kwa mujibu wa Katiba na Kanuni ni kupewa kwanza mashtaka kwa maandishi ili apate nafasi ya kujibu.

 Alisema kiongozi yeyote hatachukuliwa hatua za kinidhamu bila kwanza kupewa mashtaka yake kwa maandishi na mamlaka husika na kupewa nafasi ya kujibu mashtaka kwa maandishi.

Alitaja  ibara ya 5.4.3 na 5.4.4 ya Katiba kwamba mwanachama yeyote hatachukuliwa hatua za kinidhamu ama kuonywa ama kuachishwa ama kufukuzwa uanachama bila kujulishwa makosa yake kwa maandishi na kutakiwa kutoa majibu katika muda usiopungua wiki mbili.”

 Alitaja vipengele vingine ni kupewa nafasi ya kujitetea mbele ya kikao kinachohusika na atajulishwa kwa maandishi uamuzi wa kikao ndani ya wiki mbili baada ya kusikilizwa.

 Katika hatua nyingine, Kimesera alisema Chadema imepeleka majibu baada ya Mwigamba kupeleka barua yenye malalamiko kwa Msajili wa Vyama vya Siasa dhidi ya uongozi wa chama hicho.

Katika malalamiko yake, Mwigamba anadai kuwa katiba ya Chadema ilivurugwa na viongozi wa chama kwa kuondoa kinyume cha taratibu maelezo ya kifungu cha katiba ya chama yaliyokuwa yakiainisha ukomo wa vipindi viwili vya uongozi.

 Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi, alithibitisha kupokea barua hiyo ya Mwigamba na kusema ofisi yake inaifanyia kazi.

 Kimesera jana aliliambia NIPASHE kuwa walipeleka majibu dhidi ya malalamiko ya Mwigamba baada ya kuagizwa na msajili kufanya hivyo kabla ya Desemba 19, mwaka huu.

 Katika barua yake, Mwigamba amemuomba msajili kutoa mwongozo kuhusu anachodai kuwa ni mgogoro wa kikatiba uliopo ndani ya Chadema kufuatia kipengele cha katiba kinachogusia ukomo wa uongozi kubadilishwa kinyume cha utaratibu.

 Novemba 22, mwaka huu, CC iliwavua madaraka viongozi hao na kuwataka wajieleze kwa maandishi ndani ya siku 14 baada ya kudaiwa kuhujumu chama kwa kuandika waraka wa siri unaodaiwa pamoja na mambo mengine, kuwadhalilisha viongozi wakuu wa Chadema.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment