WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, December 5, 2013

Magufuli aungwe mkono kulinda barabara zetu

Katuni
Serikali hutumia mabilioni ya fedha kila mwaka kwa ajili ya kutengeneza barabara na miundombinu yake.
Kwa kutambua hilo, Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli alisema juzi kuwa ataendelea kusimamia sheria inayotoa mwongozo sahihi wa matumizi ya barabara ya mwaka 1973, lengo likiwa ni kuhakikisha kuwa barabara zetu zinadumu kwa muda mrefu.

Magufuli alisisitiza kuwa daima ataendelea kusimamia sheria namba 30 ya mwaka 1973 kuhusiana na usalama barabarani, iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2001, na ambayo inaelekeza kiwango cha mwisho cha uzito wa mizigo ya magari.

Sisi tunaunga mkono msimamo wa Magufuli kwa asilimia moja. Ni kwa sababu tunajua kuwa barabara hujengwa kwa kutumia fedha nyingi za walipa kodi na hivyo ni lazima zilindwe.

Tunaamini vilevile kuwa Watanzania wengi wanaunga mkono msimamo wa Magufuli, hasa baada ya kueleza namna nchi zilizoendelea zinavyotunza barabara zao.

Kwa mujibu wa waziri huyo, uzito wa juu unaoruhusiwa katika barabara za Marekani ni takriban tani 36, Urusi tani 38 huku Ujerumani, Uingereza na Ufaransa zikiruhusu tani 40 tu. Hapa kwetu, ambako kimsingi hakuna barabara nzuri na zenye ubora wa juu kama za mataifa hayo ya dunia ya kwanza, uzito wa juu unaoruhusiwa ni tani 56.

Kwa kuzingatia taarifa hiyo, tunaona kuwa Waziri Magufuli ana kila sababu ya kuzuia mpango wowote wa kinyemela kutaka kuruhusu uzito mkubwa zaidi kupitishwa kwenye barabara zetu kwani hata uzito unaoruhusiwa sasa ni mkubwa sana kulinganisha na viwango vya juu vinavyoruhusiwa katika nchi zilizoendelea; na ambazo kwa kiasi kikubwa hushiriki kusaidia miradi yetu mbalimbali ya maendeleo, ikiwamo ya barabara.

Ikumbukwe kuwa nchi zilizoendelea kama Marekani na Urusi ndizo zinazotarajiwa kuwa na barabara nzuri na imara zaidi kulinganisha na zetu kutokana na sababu ya tofauti kubwa za kiuchumi na kiteknolojia.

Hivyo, katika hali ya kawaida, ilitarajiwa kuwa barabara za nchi kama Ujerumani ndizo ziruhusiwe kupitisha magari ya uzito mkubwa kuliko Tanzania.
Hata hivyo, kinachofanyika ni kinyume chake. Barabara zetu ambazo baadhi hulalamikiwa kwa kujengwa chini ya kiwango ndizo zinazobeba mizigo mizito sasa kuliko Ujerumani.
Katika hali kama hiyo, tunadhani kwamba kila anayezitakia mema barabara zetu anapaswa kumuunga mkono Magufuli na wizara yake katika kulinda barabara zetu.

Magufuli anapaswa pia kuambukiza msimamo wake kwa maafisa wote wa wizara yake ya Ujenzi, hasa watumishi wa mizani ambao baadhi wanatajwa kuwa ni vinara wa kupokea rushwa na kuruhusu magari yenye mizigo mizito kuendelea na safari.

Hata hivyo, pamoja na kuiunga mkono serikali kupitia kwa Magufuli kutokana na uamuzi wa kulinda barabara, tunashauri vilevile kuwa kamwe isiishie hapo. Bali, ichukulie kuwa barabara ni suluhisho la muda mfupi katika kusafirisha mizigo mizito.

Tunataka ije na mpango kabambe wa kuimarisha njia zote za reli zilizopo nchini na pia kuangalia uwezekano wa kujenga nyingine ili kusafirishia mizigo mizito.
Reli ambayo ni njia ya pili kwa unafuu katika sekta ya usafirishaji duniani kote, ndiyo hutumika zaidi kusafirisha mizigo mizito nchini Ujerumani, Marekani, Uingereza, China na hata Japan; na hiyo ndiyo sababu ya wao kuruhusu tani 40 tu kupitishwa kwenye barabara.
Hapa kwetu ni tofauti. Reli ya Kati na ile ya Tazara haziko katika hali nzuri.

Matokeo yake, mizigo inayofikia kontena 800 inayopakuliwa katika Bandari ya Dar es Salaam kila uchao husafirishwa kwa njia ya barabara.
Na ikiwa kontena moja litakuwa na wastani wa tani 20, na kisha kila lori moja likakadiriwa kuwa na uwezo wa kusafirisha tani 50, maana yake ni kuwa kila uchao huwa kuna malori 320 yanayotoka katika Bandari ya Dar es Salaam kwenda sehemu mbalimbali nchini kupitia katika barabara zetu, achilia mbali mamia ya malori mengine yanayosafirisha mizigo isiyotoka bandari ya Dar es Salaam, mfano ikiwa ni mbao kutoka Nyanda za Juu Kusini na mahindi kutoka Rukwa.
Mizigo yote hiyo ni hatari kwa uhai wa barabara zetu. Njia pekee ni kuwa na mpango wa muda mrefu wa kuwa na usafiri wa uhakika wa reli.
Vinginevyo, tunahofia kuwa hata jitihada hizi nzuri za Magufuli zitaishia kugonga mwamba.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment