WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Tuesday, October 1, 2013

Tunajibaraguza huku tukijenga dola-mihadarati




NAREJEA somo la lugha ya Kiswahili na narejea neno langu ninalolirejea mara kwa mara nikitumai kwamba siku moja, au katika maeneo fulani, litaeleweka. Neno lenyewe ni ‘hamnazo.’
Neno hili ni mojawapo ya maneno yanayotumika holela, kila mmoja anayelitumia akilipa maana na tafisri inayompendeza yeye. Hii ni dalili mojawapo ya upuuzi tunaoufanya katika maeneo mengi hapa nchini.

Nimewahi kutumia hadithi mojawapo kati ya hadithi za kusisimua katika maandishi matakatifu kueleza umuhimu wa maelewano ya kilugha. Simulizi hiyo inatuhadithia kwamba huko zamani, zama za mitume na manabii, watu walijaa kiburi na jeuri iliyotokana na uwezo mkubwa wa kiuchumi na ujuzi mkubwa wa kutenda mambo waliokuwa wamejijengea.

Kutokana na ujuzi huo na uwezo mkubwa waliokuwa nao wakaamua kufanya jambo moja kubwa kuliko yote waliyokuwa wameyafanya hadi wakati huo: wakaamua kujenga mnara mrefu ambao ungepanda hadi juu mbinguni ili wafike huko na wajionee wenyewe maajabu ya mbingu na uwezo wa Mungu.

Wakaanza kujenga kile kilichokuja kujulikana kama Mnara wa Babel (Biblia, Kitabu cha Mwanzo, 11) . Wasanifu majengo walikuwa nao wa kutosha, wahandisi na waashi mahiri walikuwa tele. Na watu wote waliongea lugha moja iliyowafanya waelewane.

Inaelekea Bwana Mkubwa hakupenda jeuri ya watu hawa, na akaamua kuwasambaratisha. Ili kuwasambaratisha Bwana Mkubwa hakuwashushia radi wala tetemeko la ardhi kubomoa mnara ule, jambo ambalo bila shaka angeweza kufanya. La hasha, aliwashushia kutoelewana katika lugha, wakaisahau lugha yao, wakawa wanasemasema sana lakini hakuna anayemwelea mwenzake. Mradi mzima ukasambaratika na mnara ule ukaporomoka.

Hadithi hii inatufundisha kwamba iwapo tutaendelea kupoteza lugha na kujisemeasemea hovyo tutakuja kufika mahali tushindwe kuelewana kabisa, na huo uwe ndio ukomo wa juhudi zetu za kujenga taifa au jamii.

Sasa nirudi katika neno langu ‘hamnazo’.  Kujifanya hamnazo ni kujibaraguza, kujifanya huoni, hujui, huelewi au hutambui jambo ambalo kila mmoja analitambua ila wewe.

Ukweli ni kwamba wewe mwenyewe unalitambua vilivyo jambo hilo, lakini unaangalia kando kwa sababu ukionyesha kwamba unalitambua utahitajika kufanya jambo ambalo kwa sababu uzijuazo mwenyewe hutaki kulifanya.

Kwa mfano sote tunajua kwamba dawa za kulevya zimechangia mno kuwaharibu vijana wetu. Tunajua kwamba katika mitaa yetu dawa hizi zinauzwa kama njugu na vijana wetu wamekuwa “mateja,” hali ambayo imesababisha madhara makubwa katika jamii. Haya yote tunayajua.

Hivi sasa nchi yetu imepata sifa ya hovyo, ya kuwa njia kuu ya kusafirishia dawa hizi, na vijana wetu wamekuwa kila kinachoitwa ‘punda’ na hili limetangaa duniani kote. Wakuu wa usalama katika vituo vya mipakani wanamuona kila mwenye pasi ya kusafiria ya Tanzania kama mshukiwa.

Wakuu wa serikali yetu wanalijua hili, lakini wanajifanya hamnazo, wanajibaraguza. Tuliwahi kuambiwa kwamba vinara wa dawa za kulevya wanajulikana, kwa majina na kwa anwani. Pamoja na kujulikana huko hawakamatwi, hawachukuliwi hatua, wanaachiwa waendelee kukua na kujitanua.

Tunaangalia duniani na tunaziona nchi zilizovurugwa kutokana na biashara hii. Miaka ishirini iliyopita tulikuwa tukizungumzia Colombia na akina Pablo Escobar. Huyu ndiye aliyejijengea nguvu za kiuchumi kiasi kwamba hata alipokamatwa na kufungwa jela aliachiwa asanifu jengo la jela atakamofungwa. Ilibidi serikali ijadiliane naye hadi wakubaliane namna atakavyofungwa.

Hivi sasa tunazungumzia nchi nyingine ambayo imekwisha nayo kugeuka kuwa ‘narco-state’ au dola-mihadarati, Mexico, ambayo miaka michache iliyopita haikujulikana hivyo. Katika Bara la Afrika tunayo Guinea-Bissau, ambayo imekuwa na zahama zisizoisha kwa sababu serikali inaendeshwa na dawa za kulevya, na sehemu kubwa ya wanasiasa, wanajeshi, polisi na wanausalama na mawakala wa biashara hiyo.

Waswahili wanasema, asiyejua kifo aangalie kaburi, nami naongeza: Kaburi lako hutaliona wewe, hivyo angalia makaburi ya wenzio. Ni busara kujifunza kutoka kwa makosa yako mwenyewe, lakini ni bora kujifunza kutokana na makosa ya wenzako.

Ni kweli kwamba wanaosukuma biashara ya dawa za kulevya wamejenga nguvu kubwa, na dalili mojawapo ni haya matukio ya punda wanaotokana na nchi yetu wakibeba mizigo ya kifo. Ni kweli pia kwamba sehemu kubwa ya siasa na utawala wa nchi yetu vinaendeshwa kwa fedha kwa maana ya ununuzi wa kura na rushwa katika mifumo yetu yote ya utawala.

Sasa, kama fedha nyingi kiasi cha kutisha ndio mtaji mkuu wa kutafuta ‘uongozi’ wa kisiasa na ukuu serikalini, na kama biashra ya mihadarati ndiyo inayoingiza fedha nyingi kuliko biashara nyingine yoyote, kwa nini anayesaka kiti cha ubunge au urais asifanye biashara hiyo, hasa kama anajua kwamba hata akijulikana hakuna hatua zo zote zitakazochukuliwa dhidi yake?

Aidha, iwapo imetokea kwamba wajasiriamali wa mihadarati wanafanikiwa kuingiza fedha zao chafu ndani ya siasa na utawala na wakaweza kupata nafasi za kuitawala nchi, ni kwa nini wasihakikishe kwamba biashara hiyo inalindwa, inakuzwa, inaendelezwa na kudumishwa? Nashuku kwamba hali hii tunayo tayari.

Ukweli ni kwamba tumekwisha kupelekea ‘siasa’ yetu sokoni, na ukishapeleka ‘siasa’ yako sokoni, huna budi kujua kwamba itapata mnunuzi, na mwenye mtaji mkubwa zaidi ya wengine ndiye atakayemudu kuinunua. Tayari hili linafanyika nchini, na hakuna anayebisha.

Ikifikia hapo, kilichobaki ni kukubali kwamba, kwa njia moja au nyingine, serikali inayotokana na uuzaji na ununuzi wa kura katika mazingira ambamo fedha iliyotumika katika biashara hiyo ni matunda ya mihadarati, itakuwa ni serikali ya mihadarati na itajenga dola-mihadarati. Serikali inayojifanya hamnazo mbele ya biashra hii ni wazi inafaidkia nayo.

Anayebisha tukutane miaka michache ijayo.

No comments:

Post a Comment