WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Tuesday, October 8, 2013

MCHAKATO KATIBA MPYA:JK: Hoja ya Z`bar irudishwe bungeni

  *Apinga maandamano ya wapinzani
  *Awakaribisha Ikulu kwa majadiliano
  *Amshushua Tundu Lissu, asema mzushi
  *Kuvunjwa Tume ya Warioba afafanua
 
Rais Jakaya Kikwete
Rais Jakaya Kikwete, amekata mzizi wa fitina katika suala la mchakato wa katiba kwa kushauri ile hoja ya Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria  na Utawala kutokufanya vikao Zanzibar kusikiliza maoni ya wadau wa Zanzibar, ilirudishwe Bungeni ili wabunge walizungumze na kulifanyia uamuzi muafaka.
Aidha, amevitaka vyama vya Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi kuachana na mipango ya maandamano na kufanya ghasia kama dhamira yetu ni kutaka kupata Katiba mpya kwa mujibu wa Katiba na Sheria.
Kauli hiyo ya Rais imekuja kukiwa kumebakia siku tano zilizotangazwa na viongozi wakuu wa vyama hivyo kwa ajili ya kufanya maandamano nchi nzima kupinga Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba uliopitishwa wakati wa mkutano wa 12 wa Bunge mwezi uliopita.
Rais Kikwete alisema aliambiwa kuwa kuliwepo madai ya Zanzibar kutokushirikishwa ipasavyo katika kutoa maoni kwenye muswada huo.
“Nimeeleza kwa kiasi gani Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeshirikishwa na kutoa maoni yake yaliyojumuishwa katika Muswada.  Hivyo basi napata tabu kuyaelewa madai kwamba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar haikushirikishwa msingi wake nini!  Labda kuna kitu sikuambiwa,”alisema
Hoja kwamba Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala kutokufanya vikao Zanzibar kusikiliza maoni ya wadau wa Zanzibar, aliambiwa kuwa kanuni za Bunge hazina sharti hilo, hivyo kamati haistahili kulaumiwa. 
Rais Kikwete alishauri kama ni hivyo, suala hilo lirudishwe Bungeni ili wabunge walizungumze na kulifanyia uamuzi muafaka, vinginevyo watu wataendelea kulaumiana isivyostahili. 
Alisema, “kuligeuza jambo hili kuwa ni suala la kukataa Muswada au kususia vikao vya Bunge au kufanya maandamano sidhani kama ni sawa”. 

MAANDAMANO YA WAPINZANI
Rais Kikwete alisema kuandamana nchi nzima au kuchukua hatua za kutotii sheria kama Mwenyekiti wa Chadema, freeman Mbowe anavyotaka hakutaleta mabadiliko wanayoyataka katika sheria hii.
“Kuna msemo wa wahenga kuwa “historia hujirudia”.  Naomba hekima ziwaongoze viongozi wa Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi na zituongoze sote kutumia utaratibu tulioutumia mwaka 2012,”alisema.
Alisema kuwa mwaka jana, kulipotokea mazingira ya kutoelewana katika suala la katiba, pande zote zilikaa pamoja na kuzungumzia hoja moja baada ya nyingine na kukubaliana nini kifanyike na  baada ya kuridhiana hatua zipasavyo za kisheria na kanuni zilichukuliwa na kumaliza mzozo.
Alisema kufanya kinyume cha hayo hakutaleta ufumbuzi wa mzozo huu na badala yake tutaliingiza taifa kwenye matatizo yasiyokuwa ya lazima na kwamba tukikataa kufanya hayo Watanzania wanayo kila sababu ya kuhoji dhamira zetu na kutilia shaka nia zetu.
 “Watanzania watakuwa na haki ya kuuliza nia ni hii yetu sote ya kupata Katiba Mpya kwa kutumia njia za kikatiba na kisheria au tuna dhamira nyingine iliyojifisha?, alihoji Rais Kikwete.
Alisema viongozi wa vyama hivyo watumie njia halali zinazotambulika kikatiba na kisheria kujenga hoja za kufanya marekebisho wanayoyaona wao yanafaa kuboresha  Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na kufanya hivyo kutasaidia  kujenga Taifa badala ya kubomoa. 
Aliongeza kuwa baadhi ya hoja zilizotolewa na Kambi ya Upinzani zimemsikitisha sana na madai na tuhuma za uongo kwamba katika uteuzi wa Tume ya Katiba hakuheshimu mapendekezo ya Baraza la Maaskofu Katoliki (TEC), Baraza la Kikristo (CCT) na walemavu.
AMSHUSHUA LISSU
“Siyo tu kauli hiyo ya Tundu Lissu (Mbunge wa Singida Mashariki) ni uzushi na uongo mtupu bali pia ni ya unafiki, fitina na uzandiki wa hali ya juu.  Nasema hivyo kwa sababu, sipendi kuamini kuwa mbunge amesema yale kwa kutokufahamu ukweli au kwa bahati mbaya.”
Rais alisema mbunge huyo aliamua kupotosha ukweli ili pengine isaidie kujenga hoja yake ya kutaka Rais asiteue wajumbe 166 wa Bunge Maalum la Katiba. 
Alisema hashabikii jukumu hilo, lakini kwa kutimiza wajibu na maslahi ya taifa akiagizwa na sheria za nchi atalifanya.
Akilinganisha na uteuzi wa wajumbe 30 wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Rais Kikwete alisema haikuwa rahisi hata kidogo na hii ya uteuzi wa watu 166 watakaoingia katika Bunge Maalum la Katiba itakuwa ngumu zaidi.
Alieleza kuwa licha ya kutakiwa kuteua watu 30 wajumbe walioteuliwa na wadau walikuwa zaidi ya 500  akieleza kuwa kwa Zanzibar zilikuwa asasi zaidi ya  60  wakati Bara  zilikuwa asasi zaidi ya 170 zikiwa na waombaji zaidi ya 500.
Alisema uteuzi ulihakikisha kuwa wawakilishi wa  vyama vya siasa vyenye wabunge na wajumbe Baraza la Wawakilishi wanapatikana,  mashirika ya dini kubwa ya  TEC, CCT na Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata)  pia wanakuwepo.
Alisema kwa upande mwingine Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) ilipendekeza uteuzi wa wajumbe wa Bunge Maalum ufanywe na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushauriana na kuafikiana na Rais wa Zanzibar.  Pia SMZ ilishauri kwamba kama Bunge Maalum litashindwa kufikia maamuzi ndani ya siku 70 zilizopendekezwa, liongezewa muda hadi kufikia siku 90. 
“Ndiyo maana naiona mantiki ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akishirikiana na Rais wa Zanzibar wa kuwateua wajumbe wa Bunge Maalum.”
Alisema dhana kuwa kila kikundi kiteue chenyewe watu ingefaa kama kungekuwepo na nafasi za kutosha kwa  kila kundi nchini.  Rais alisema pendekezo hilo haliwezekani, labda kuwe na Bunge Maalum lisilokuwa na ukomo wa wajumbe. MUSWADA BUNGENI
Rais Kikwete aliwaambia wapinzani kuwa  mapendekezo yao kuhusu marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya katiba hayawezi kuzungumzwa nje ya Bunge.
Alisema maoni yao yangezungumzika na hata baadhi yangekubalika kama wasingetoka nje wakati wa mjadala huo uliozua tafrani bungeni mwezi uliopita.
Aliongeza kuwa baada ya wapinzani kupoteza fursa halali kutoa mapendekezo yao na sasa kutaka kupata ufumbuzi nje ya Bunge ni jambo lisilowezekana.
“ Haya ni masuala yanayohusu Bunge ambayo hujadiliwa na kuamuliwa Bungeni na si vinginevyo,”alisema.
Aliwaambia kuwa kwa vile hawakuwepo ndani ya mjadala na  hakuna aliyewawakilisha hivyo hakuna kinachoweza kufanyika.

WAJUMBE BUNGE LA KATIBA
Rais Kikwete alisema kulikuwa na hoja ya kutaka idadi ya wajumbe wa Bunge la Katiba kutoka Tanzania Bara na Zanzibar iwe sawa kama ilivyo kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Alisema sababu ya idadi ya wajumbe wa tume kuwa sawa inatokana na utaratibu wao wa kufikia uamuzi, kwani ni kwa maelewano ya wote (consensus) na siyo kwa kupiga kura.
Alifafanua kuwa, Bunge maalum la Katiba lina sharti la kufanya uamuzi kwa theluthi mbili ya kura za kila upande kukubali, bila ya hivyo hakuna uamuzi, hivyo katika bunge hilo nguvu si uwingi wa kura ambazo upande fulani unaweza kupata bali ni ulinganifu sawa wa kura za kila upande peke yake.
“Zanzibar ina majimbo 50 ya uchaguzi na Tanzania Bara ina majimbo 189, hivyo ukiamua kwa wingi kila wakati Wazanzibari watashindwa.  Lakini, hapajakuwepo madai ya Zanzibar nao kutaka kuwa na idadi sawa ya majimbo kama Bara au kupunguza majimbo ya Bara yawe sawa na ya Zanzibar kwa sababu wingi si hoja,”alisema.

Alisema msingi unaotumika ni kutoa nguvu sawa za uamuzi kwa kila upande wa Muungano wakati wa kuamua masuala ya Katiba, hakuna mdogo wa kumezwa na mkubwa, wote wako sawa.

 KUVUNJWA TUME YA WARIOBA

Alisema kumekuwepo na madai ya wapinzani kuhusu suala la uhai wa Tume ya Katiba ambao wanataka usiishe wanapokabidhi rasimu ya pili kwa Bunge Maalum bali waendelee kuwepo mpaka mwisho wa mchakato.

Aliongeza kuwa  suala la ukomo wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba siyo mapendekezo ya Serikali wala ya Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala bali lilitokana na pendekezo la Mbunge katika Bunge wakati wa kupitia vifungu na kuungwa mkono na wabunge wengi.
 “Nami naiona hoja ya wajumbe wa tume kuwa na wajibu wakati wa Bunge Maalum hasa wa kusaidia kufafanua mapendekezo ya Tume.  Je ushiriki huo uwe vipi? Je ni Wajumbe wote au baadhi yao ni jambo linaloweza kujadiliwa,”alisema.
Jumanne wiki hii, Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, akizungumzia suala la ukomo wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, alisema suala hilo lilipendekezwa na Mbunge wa Kisarawe, Suleman Jaffer.
Chikawe alisema mbunge huyo alipendekeza kuwa tume hiyo itakapowasilisha ripoti yake ivunjwe sababu haitakuwa na kazi na kama Bunge la Katiba litahitaji ufafanuzi wowote ataitwa Mwenyekiti wa Tume hiyo kutoa ufafanuzi.

MUSWADA KUHODHIWA NA CCM

Chikawe alisema kama unachukua Bunge kwa misingi ya chama siyo sawa lakini bunge halikukutana na kupitisha muswada huo kwa misingi hiyo.

“Kitu cha msingi ni kwamba kolamu ya wabunge ilitimia wakati wa kupitisha muswada huo, hivyo sheria haikuvunjwa,sikuona sababu ya wabunge wa upinzani kutoka Bungeni,”alisema.

Alisema tabia ya wabunge wa vyama vya upinzani kutoka bungeni na kukimbilia mitaani na kwenda kuwapotosha wananchi siyo sahihi.

KUMTISHA RAIS ASIPOSAINI MUSWADA

Alisema yeye (Chikawe) hana ubavu wa kumtisha Rais kwani Rais ana hiari ya kuusaini muswada huo au kutousaini.
“Ni imani yangu kwamba Rais atasaini muswadam atatumia ustaarabu wake,”alisema Chikawe.

Juzi viongoz wa Kamati ya Ufundi ya Ushirikiano wa Vyama vya CUF,Chadema na NCCR-Mageuzi walisema maandalizi kwa ajili ya maandamano hayo yatakayofanyika Oktoba 10 mwaka huu, yameanza kufanyika baada ya kuwasiliana na viongozi wa mikoa yote.

SHAMBULIZI LA KIGAIDI NAIROBI

Rais Kikwete alisema tangu shambulio lililotokea mwaka 1998, Serikali imekuwa inajenga uwezo wa vyombo vya ulinzi na usalama kupambana na ugaidi katika nyanja mbalimbali.

”Tunaendelea kujiimarisha bila kusita siku hadi siku.  JWTZ, Polisi na Idara ya Usalama wa Taifa wamekuwa na ushirikiano wa karibu kwa ajili hiyo.  Juhudi zetu hizo ndizo zinazotufanya tuwe salama hadi sasa,”alisema.

Rais Kikwete alisema baada ya tukio la Kenya, vyombo vya ulinzi na usalama vimeimarisha mikakati yao maradufu na kwamba pamoja na kujizatiti kwetu huko hatuwezi kusema kuwa tukio la kigaidi halitaweza kutokea nchini.

Alisema uhakika huo haupo kwani hata mataifa makubwa na tajiri yameshambuliwa, hivyo jambo la muhimu ni kuendelea kuchukua tahadhari na wananchi kusaidia ili  vyombo vya ulinzi na usalama  vifanikiwe zaidi. 
 
Aliongeza kuwa watu wote wenye shughuli zinazokusanya watu wengi kama vile maduka, maofisi, mahoteli, migahawa waweke kamera za ulinzi nje na ndani ya maeneo yao na kuweka vifaa vya upekuzi (metal detectors and x-rays). 

Rais Kikwete alisema wananchi waendelee kufanya shughuli zao bila ya hofu ingawaje wasiache kuwa makini na kuchukua tahadhari, na kwamba maafisa husika wa vyombo vya ulinzi na usalama wataendelea kuelimisha umma kuhusu hatua mbalimbali za tahadhari za kuchukua. 
*Gaudensia Mngumi na Thobias Mwanakatwe
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment