WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, May 15, 2014

WHO yajitosa dhidi homa ya dengue

Dar es Salaam. Shirika la Afya Duniani (WHO), limejiunga katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa homa ya dengue kwa kuagiza vipimo 1,000 kwa ajili ya upimaji nchi nzima.
WHO imechukua hatua hiyo kusaidia juhudi zinazoendelea za kupambana na homa hiyo na imeagiza utafiti zaidi ufanyike ili kutambua aina halisi ya virusi vya dengue vilivyopo nchini kwa kulinganisha na vile vinavyopatikana katika maeneo mengine duniani.
Akizungumza na gazeti hili jana, Ofisa wa Taaluma na Udhibiti wa Magonjwa wa WHO, Dk Grace Saguti alisema tayari chombo hicho kimeagiza vipimo hivyo vitakavyogharimu Sh17.7 milioni na kila kimoja kinaweza kupima sampuli 25, hivyo kunufaisha watu 25,000.
Hatua hiyo imechukuliwa huku kukiwa na taarifa kwamba baadhi ya hospitali za Serikali za wilaya na rufaa zinakabiliwa na uhaba wa vipimo, hali iliyosababisha kutoza kati ya Sh25,000 hadi Sh30,000 kwa ajili ya kupima mgonjwa mmoja.
Katika vituo binafsi, wagonjwa wamekuwa wakipimwa kwa gharama inayofikia Sh50,000 hadi 60,000 kwa kila mtu.
Juhudi hizo za WHO zimetangazwa siku moja baada ya Serikali kupitia Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Steven Kebwe kulieleza Bunge kuwa kwa sasa vipo vipimo 350 na Serikali inatarajia kuagiza vingine 750.
Dk Saguti alisema WHO imeshatengeneza miongozo, mikakati na mafunzo pamoja na kutoa vitendea kazi ili kujua namna ya upimaji na udhibiti.
“Sheria za afya za kimataifa za mwaka 2005 hadi 2007, zinaelekeza nchi kuhusu tatizo lolote lisilo la kawaida liripotiwe WHO. Serikali ya Tanzania ilifanya hivyo na miongozo ya homa ya dengue ikatolewa,” alisema.
Alisema miongozo iliyotolewa na WHO ni pamoja na tatizo la dengue lisiachwe mikononi mwa Wizara ya Afya pekee, bali sekta zote zihusishwe katika kuudhibiti.

Miongozo mingine ni uhamasishaji wa upatikanaji wa vipimo ili kuhakikisha watu wenye dalili hizo na ambao wamepimwa hawana malaria, wanapimwa na kutibiwa kama inavyotakiwa.
Alisema miongozo mingine ya WHO ni kuwapo rasilimali fedha ili vituo vya afya viwe na dawa pamoja na vipimo.
Tayari Rais Jakaya Kikwete ameagiza Wizara ya Fedha na ile ya Afya kushirikiana na Bohari Kuu ya Dawa (MSD) kupambana na ugonjwa huo kwa dharura.
Takwimu
Jambo lingine ambalo WHO imeishauri Serikali ni kutafuta takwimu sahihi ili kujua ukubwa wa tatizo na kulifanyia kazi kulingana na uzito wake.
“Uhakiki wa takwimu, ushahidi na taarifa sahihi za magonjwa ni suala muhimu katika kudhibiti. Ndiyo maana tunaitaka wizara kuhakikisha inapata takwimu sahihi,” alisema.
Alisema wizara hiyo inatakiwa iwe na mfumo mzuri wa takwimu kuanzia ngazi ya chini na ihusishe sekta za Serikali na zile binafsi.
Wakati hadi jana takwimu za Serikali zilionyesha kuwa idadi ya watu waliougua wamefikia 460, takwimu zilizopatikana katika baadhi ya hospitali jijini Dar es Salaam zilionyesha kuwa walikuwa wamefikia 677, achilia mbali waliokuwa wameugua kati ya Oktoba mwaka jana hadi Machi.
Katika uchunguzi huo wa gazeti hili, ilibainika kuwa Mwananyamala wamefikia wagonjwa 142, Amana (54), Maabara ya Lancet (53), Hindul Mandal (26), Aga Khan (11), Kliniki ya IST (245), Regency (63), Temeke (15), Dk Mvungi (3) Muhimbili (65).
MSD: Tuna vipimo vya kutosha
Wakati baadhi ya hospitali zikiripoti uhaba wa vipimo, Kaimu Mkurugenzi wa MSD, Cosmas Mwaifani amesema inavyo vya kutosheleza mahitaji.
“Sisi wakati wote tupo tayari kupambana na dharura, si tu kwa sababu ya mlipuko, pia hatuhusiki kabisa na masuala ya kuongezeka kwa bei za vifaatiba au dawa hospitalini kwa sababu ni taasisi ya Serikali,” alisema.
Mmoja wa wasambazaji wa vipimo vya upimaji wa dengue, Ally Hamimu alipiga simu chumba cha habari jana na kueleza wasiwasi wake kuhusu gharama za vipimo kuwa akisema ni kubwa kuliko uhalisia.
??Tunaamini kuna vipimo mbalimbali vya kupima homa ya dengue lakini hata kama hospitali zinatafuta faida, zinatakiwa kutoza kati ya Sh13,000 na Sh15, 000 kwa kipimo,” alisema Hamimu na kutolea mfano vitendanishi vya Dial Lab Dengue lgG/lgM ambavyo boksi la vipimo 30 huuzwa kati ya Sh175,000 na Sh190,000.
“Hii inamaanisha kuwa kipimo kimoja kwa rejareja kinaweza kuuzwa kati ya Sh6,500 hadi Sh7,500 na huduma za kupima zisizozidi Sh15,000.
“Sasa kutokana na mahitaji kuwa makubwa ya vipimo hivi baada ya mlipuko wa dengue, baadhi ya wamiliki wa hospitali wanapandisha bei, wananchi wasikubali,” aliongeza Hamim.
Dk Buberwa azikwa
Wakati huohuo, mamia ya wakazi wa Dar es Salaam wakiwamo madaktari na watumishi wa hospitali mbalimbali, jana walijitokeza katika Makaburi ya Tabata Kinyerezi, Dar es Salaam kumzika Dk Gilbert Buberwa aliyefariki dunia Jumapili kutokana na homa ya dengue.
Dk Buberwa aliyekuwa daktari bingwa na mkuu wa kitengo cha magonjwa ya akili katika Hospitali ya Temeke, ameacha mke na watoto wawili.
Andrew Msechu, Florence Majani, Nuzulack Dausen na Julius Mathias (FS)

source: mjengwa blog

No comments:

Post a Comment