WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, May 15, 2014

ELIMU BAHARI: Mbu wa homa ya dengue anataga mayai 1,000 maishani

HAAAAAAAAAAAAAAA_2731e.jpg
MBU Aedes au Aedes aegypti ni wadudu wenye mabawa mawili na miguu sita kutoka familia ya Culicidae.
Mbu huyo asili yake ni Afrika lakini hivi sasa amesambaa sehemu mbalimbali duniani hasa sehemu za tropiko na anapatikana majira yote ya mwaka hasa sehemu zenye maji maji. Machapisho mbalimbali ya kimataifa ya utafiti wa kisayansi kuhusu mbu huyo yanaeleza kuwa amekuwepo kwa zaidi ya miaka milioni 150 iliyopita na kusabisha maradhi kwa binadamu wa kale.
Utafiti wa awali uliofanywa na mwanasayansi Fredric Hasselquist mwaka 1757 ulitaja mbu huyo kwa jina la Culex aegypti. Jina la Aedes aegypti lilianza kutumika mwaka 1920 na lilianzishwa na mwanasayansi Harrison Gray Dyar, Jr. Aedes ni mbu anayeeneza virusi vinavyosababisha ugonjwa maarufu kwa jina na chikungunya, homa ya manjano na homa ya dengue ambayo hivi sasa inaenea kwa kasi katika jiji la Dar es Salaam.
Mbu Aedes ni miongoni mwa wadudu walioko katika hali ya metamofisisi ambao maisha yao hupitia hatua nne zinazowafanya kuwa na tabia na maumbo tofauti ambazo ni yai, lava, pupa na mbu kamili. Unaweza kumtambua mbu huyo kwa kuwa ana mistari meupe miguuni.
Tofauti na mbu wanaoeneza ugonjwa wa malaria ambao huuma usiku, mbu wa homa ya dengue huuma mchana na usiku.Taarifa za kisayansi zinaeleza kuwa mbu jike ndiye hasa anayeuma na kueneza kirusi cha homa ya dengue wakati akifyonza damu katika mwili wa binadamu.
Mbu jike hutumia damu kama lishe kuu ili aweze kurutubisha mayai yake ili kuendeleza kizazi cha mbu hao. Baada ya kunyonya damu ya kutosha mbu jike huweza kutaga mayai 100 hadi 200 kwa uzao mmoja. Jike anaweza kutaga mara tano katika kipindi cha uhai wake.
Mbu aliyepevuka huishi kwa wastani wa wiki mbili hadi mwenzi moja hivyo mbu mmoja aweza kutaga mayai kati ya 500 hadi 1,000 kwa kipindi cha wiki mbili hadi mwenzi mmoja. Wingi wa mayai unategemea kiasi cha damu aliyopata kwa kuwa kadiri anavyopata damu nyingi ndivyo anavyotaga mayai mengi zaidi.
Ingawa mbu huyo anataga mayai 200 katika uzao mmoja, hutaga mayai sehemu tofauti ili kuzuia kizazi chache kisiangamie kwa urahisi endapo adui atavamia mayai hayo. Mayai ya mbu aina ya Aedes yana umbo la mviringo uliochongoka, yana gamba laini na urefu wa milimita moja. Mbu anapotaga hutoa mayai meupe ila baada ya dakika chache hubadilika na kuwa na rangi nyeusi.
Mbu hawa hupendelea kuzaliana kwenye maji yaliyotuama karibu na makazi ya watu au hata ndani ya nyumba. Mbu huyo anataga kwenye madimbwi ya maji hasa sehemu yenye mafuriko, kwenye mapango ya miti, sehemu zenye mashimo au mapango yaliyotengenezwa na binadamu.
Pia wanataga mayai hao kwenye mapipa, vyungu na makopo ya maua, kweye chupa na makopo yaliyotupwa ovyo, matairi ya gari, vifuu vya nazi, matambara katika viambaza vya nyumba na sehemu zozote zile zenye upenyo hasa katika lundo la uchafu katika viambaza vya nyumba.
Mayai hayo huanguliwa kwa siku tofauti kulingana na hali ya hewa na mazingira ya eneo husika. Sehemu yenye joto kama Dar es Salaam mayai huanguliwa katika siku mbili tu lakini sehemu zenye baridi mayao huchukua hadi siku saba kabla ya kuanguliwa. Mayai ya mbu wa homa ya dengue hayaanguliwi yote kwa wakati mmoja, wakati wa kuanguliwa yanaweza kupishana saa chache au siku nzima kulingana na mazingira ya eneo husika.
Kupishana huko huwezesha kizazi cha mbu kuwepo wakati wote katika majira ya mwaka ikiwa eneo husika litakuwa na hali ya maji maji. Mayai ya mbu anayeeneza ugonjwa wa dengue yanauwezo wa kuhimili hali ya hewa na kukaa muda mrefu bila kuharibika. Ikiwa mayai hayo yametagwa wakati wa kiangazi yanaweza kukaa zaidi ya mwaka mzima bila kuanguliwa kisha huanguliwa kipindi cha mvua ili kiluilui waweza kuishi na kukua vyema.
Kitendo cha yai kukaa muda mrefu kinasababisha changamoto katika harakati za kumuangamiza mbu huyo mwenye uwezo wa kudhuru na hata kuua binadamu ili waweze kuendeleza kizazi chake. Baada ya mayai kuanguliwa viluwiluwi vya mbu huishi kwa kula chembechembe zinazopatikana kwenye maji.
Baadhi ya chembechembe ni ndogo sana haziwezi kuonekana kwa macho bila msaada wa darubini. Viluwiluwi hao huogelea kwenye maji na wakati mwingine huja juu ya maji. Wanaweza kuishi kwenye kina kifupi cha maji ndio maana wanaweza kuzaliana kwenye makopo ya maua yanayoruhusu maji kutwama, kwenye vifuu vya nazi na maeneo mengine yanayohifadhi maji kwa muda mrefu.
Viluwiluwi wanakua kulingana na hali ya hewa, endapo kuna hali joto anaweza kukua kwa muda mfupi katika siku moja ila kama kuna hali ya ubaridi na maji ya kutisha anaweza kubaki kwenye maji hata kwa zaidi ya mwenzi mzima. Lava aliyekomaa huwa na urefu wa milimita nane. Mbu dume hukua haraka zaidi hivyo hubadilika na kuwa mbu kabla ya mbu jike.
Hatua ya kukua yaani yai, lava na pupa huchukua muda mrefu ikilinganishwa na muda ambao pupa anapobadilika na kuwa mbu kamili. Mbu aliyepevuka anaweza kuishi kwa wastani wa wiki mbili hadi mwezi mzima na kusababisha maradhi mbalimbali yanayotokana na homa ya dengue.
Inaelezwa kuwa neno dengue linatokana na neno la lugha ya Kihispania linalomaanisha homa kali pia baadhi ya watafiti wanasema limetoholewa kutoka na lugha ya Kiswahili “Dinga” ambalo hutumika kuelezea ugonjwa wa Ka-dinga pepo, unaofanana na dengue ambapo Waafrika waliamini kuwa husababishwa na pepo mbaya.
Homa ya dengue Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara wa Afya na Ustawi wa Jamii, homa hiyo imethibitishwa kuwepo nchini tangu Juni 2013 baada ya sampuli zilizochukuliwa kutoka kwa watu waliohisiwa kuwa na ugonjwa huo jijini Dar es Salaam kuchunguzwa katika maabara ya Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu.
Dalili za ugonjwa ni homa, kuumwa kichwa, maumivu ya viungo na uchovu. Dalili hizo huanza kujitokeza kuanzia kati siku ya 3 na 14 tangu mtu alipoambukizwa kirusi cha homa ya dengue. Kwa wakati mwingine dalili za ugonjwa huo zinaweza kufanana sana na dalili za malaria hivyo wananchi wanahimizwa kuchukua tahadhari na kupima afya zao mara wanapohisi dalili za malaria ili kugundua kama wana vimelea vya malaria ua virusi vya homa ya dengue.
Tabia ya kunywa dawa bila kupima inaweza kusababisha mtu kupoteza maisha kwa sababu homa ya dengue haitibiwi kwa dawa za malaria, haina chanjo wala tiba maalumu. Kwa maneno mengine homa ya dengue sio kama malaria ambayo kina mtu anaweza kutibiwa na dawa za mseto.
Homa ya dengue hutibiwa kwa dawa tofauti kulingana na dalili zinakazoambatana na ugonjwa. Endapo ugonjwa unaambatana na homa kali mgonjwa atatibiwa homa, kama anapungukiwa na damu au maji mwilini tiba ni kuwekewa damu au maji.
Pia mgonjwa wa homa ya dengue anaweza kutokwa na damu kwenye fizi, mdomoni, puani, kwenye macho na pia njia ya haja kubwa na ndogo na tiba yake haiwezi kufanana na tiba ya mgonjwa mwenye homa bali atapata tiba sahihi kulingana na tatizo lake.
Ugonjwa huu hauenezwi kutoka binadamu mmoja kwenda kwa mwingine. Homa ya dengue inaweza kutibika kama mgonjwa atapelekwa hospitali mapema na kupatiwa matibabu ya haraka. Endapo mgonjwa atachelewa kupatiwa matibabu, mgonjwa anaweza kupoteza maisha.
Wananchi hawapaswi kuwa na hofu kuhusu tiba kwa sababu serikali imeazimia kuanzisha vituo maalum vya ufuatiliaji wa ugonjwa huu katika hospitali 15 za Mkoa wa Dar es Salaam ikiwa ni pamoja Hospitali ya Taifa Muhimbili, Hospitali zote tatu za Manispaa katika Jiji la Dar es Salaam yaani Amana, Mwananyamala na Temeke.
Pia vituo maalum vitaanzishwa katika Kituo cha Afya Kigamboni, Kituo cha Afya cha Mbagala Rangi Tatu, Dispensari ya Yombo Vituka, Kituo cha Afya cha Mnazi Mmoja, Dispensari ya Tabata A, Kituo cha Afya cha Bochi, Kituo cha Afya cha Mbweni, Hospitali ya Mission Mikocheni, Hospitali ya TMJ, Hospital ya Regency na Hospital ya Hindu Mandal.
Mbinu za kupambana dhidi ya mbu wa homa ya dengue Ingawa mbu huyo anaweza kuangamiza kizazi cha binadamu ni rahisi kupambana naye kama jamii itaweka dhamira ya dhati ya kuchukua hatua madhubuti ikiwa ni pamoja na kuangamiza mazalio ya mbu hao kwa kufukia madimbwi ya maji yaliyotuama au nyunyuzia dawa ya kuua viluwiluwi vya mbu kwenye madimbwi hayo.
Kufanya usafi kwa kuondoa vitu vyote vinavyoweza kuweka mazalio ya mbu kama vile, vifuu vya nazi, makopo, magurudumu ya magari yaliyotupwa hovyo, kufyeka vichaka vilivyo karibu na makazi ya watu na kuhakikisha maua yanayopandwa kwenye makopo au ndoo hayaruhusu maji kutuama.
Pia kuna ulazima wa kufunika mashimo ya maji taka kwa mfuniko imara na kusafisha gata za paa la nyumba ili kutoruhusu maji kutuama. Pia ni vyema kunyunyuzia dawa kwenye makaro ya maji machafu na vyoo vya shimo.
Ili kuepuka ugonjwa wa dengue kila familia inahimizwa kuzingatia usafi, kuweka wavu kwenye milango na madirisha, kuvaa nguo ndefu na yenye mikono mirefu ili kuzuia kung’atwa na mtu, kujipaka dawa ya kufukuza mbu na kutumia neti yenye dawa wakati wote, mchana na usiku.
Makala haya yameandaliwa kwa kutumia vyanzo mbalimbali vya habari kwa njia ya mtandao wa kompyuta pamoja na taarifa kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii nchini. 

(CHANZO: Mjengwa Blog :HABARILEO)

No comments:

Post a Comment