WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, May 15, 2014

Katiba ilivyowaunganisha wapinzani bungeni

Kwa mara ya kwanza kambi rasmi ya upinzani bungeni iliyokuwa ikiundwa na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imekubali kushirikisha vyama vingine wiwili vya upinzani.
Vyama vilivyoshirikishwa katika kambi hiyo rasmi ya upinzani ni Chama Cha Wananchi (CUF) na NCCR-Mageuzi na Kiongozi wa kambi hiyo, Freeman Mbowe ameunganisha ushirikiano na vyama hivyo baada ya kuvunja na kuteua Mawaziri vivuli wanaotoka nje ya Chadema.

Tangu mwaka 2010, baada ya Chadema kupata idadi kubwa ya wabunge, ilikataa kuunda kambi rasmi ya upinzani kwa kushirikisha vyama vingine vya upinzani vyenye wabunge vikiwamo vya CUF, TLP,UDP na NCCR-Mageuzi.

Wiki iliyopita Mbowe alitangaza Baraza hili kuvuli huku akiwapa nafasi wabunge wa CUF na NCCR-Mageuzi ambavyo vimeonyesha ushirikiano tangu Bunge la Katiba ambalo lililoanza mwezi Februari mwaka na kuahirishwa mwezi uliopita.

Hata hivyo, Mbowe amewaacha nje wabunge kutoka vyama vya TLP, Augustino Mrema na John Cheyo anayetoka Chama cha UDP, kwa madai kwamba hawaeleweki wapo upande gani wa shilingi na hivyo hana sababu ya kushirikiana na watu wa namna hiyo.

Wiki iliyopita Mbowe ambaye ni Mbunge wa Hai Chadema na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, alitangaza Baraza hilo.

Mbowe anasema lengo la ushirikiano huo wa vyama vitatu lilikuwa limelenga kwenye Bunge la Katiba tu lakini sasa nguvu yao itaimarishwa hadi kwenye Bunge la Bajeti linaloendelea hivi sasa mjini Dodoma.

Anasema lengo la umoja huo ni kuweka nguvu ya pamoja na hata nje ya Bunge ili kuhakikisha unaiondoa  CCM madarakani katika Uchaguzi Mkuu ujao mwakani.

Kuhusu uwezekano wa wa umoja huo kuendelea na kufikia hatua ya kuachiana majimbo ya kugombea mwaka 2015, Mbowe anasema kwa sasa hajui baadaye ishirikiano huo utakuwa katika hali gani.

“Unajua siasa inabadilika kulingana na mazingira, kwa sasa siwezi kuwa mtabiri kuwa huko mbeleni hali itakuwaje, ngojeni wakati ukifika,”anasema Mbowe.

Mbowe anasema Mawaziri (makamanda)  hao vivuli watakuwa na jukumu la kupambana kuihoji Serikali ya CCM ili itoe majibu ya matatizo yanayowakabili wananchi.

Kuhusu ushirikiano wa vyama hivyo, Mbowe ambaye ndiye Mwenyekiti wake, anasema hawatashiriki katika Bunge la Katiba ambalo litaendelea mwezi Agosti mwaka huu mjini Dodoma

Vyama hivyo vitatu viliamua kususia Bunge la Katiba na kutoka nje kwa madai kwamba Wajumbe wake wanaotoka CCM na baadhi wale walioteuliwa na Rais kuendekeza matusi, kejeli, vijembe huku wakikataa sura ya kwanza na sita ya Rasmu iliyowasilishwa bungeni na Jaji mstaafu Joseph Warioba.

Sura hizo mbili zinazozungumzia muundo wa muungano zilizua mjadala mkali licha ya kuwa mpaka Bunge hilo la Katiba linaahirishwa hakuna maamuzi yoyote yaliyokuwa yamefikiwa kwa maana ya kuzijadili na kuzipitisha.

Mbowe anasema umoja unaoundwa na vyama hivyo hautarejea katika Bunge la Katiba na wanachokifanya sasa ni kuhakikisha wanaendeleza mapambano kuhusu kuundwa Katiba mpya kwa kuyaelekeza nje ya Bunge hilo ambalo litaendelea mwezi Agosti mwaka huu.

Baadhi ya wabunge ambao walipata uteuzi huo wa Mbowe kuwa Mawaziri Vivuli wanasema nia ya umoja huo ni kukua na kudumu hadi kufikia kuachiana nafasi za kugombea Ubunge na mgombea mmoja wa Urais mwaka 2015.

Waziri kivuli wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Magdalena Sakaya (Viti Maalum-CUF), ambaye awali hakuwemo katika Baraza la Mbowe anasema, watashirikiana na kwamba wanataka siku moja kuwe na chama kimoja cha upinzani chenye nguvu ili kufikia malengo wanayokusudia.

Ingawa kila chama kina chama kina sera zake lakini, lengo kubwa ni kuwahudumia Watanzania ili kufikia ndoto zao za maendeleo ya kweli.

 Waziri wa Maendeleo, Jinsia na Watoto,  Barwan Salum Khalfani anasema pamoja na kwamba awali upinzani haukuwa pamoja lakini sasa mambo hayapo hivyo na kwamba mazingira ya kisiasa yamewafanya wajikute wanalazimika kuungana.

Kwa upande wake, Waziri wa Uchukuzi, Moses Machali (NCCR-Mageuzi) anasema upinzani kwa muda mrefu ulifikiria kuungana, lakini wapo wenzao waliokuwa wanafifisha ndoto hizo huku akimtaja Augustine Mrema kuwa si mpinzani wa kweli kwani bado yuko CCM.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment