WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Monday, May 5, 2014

Ukawa gumzo mkutano wa CCM Zanzibar

Katibu Mkuu wa CCM,Abdulrahman Kinana
Mkutano wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) uliofanyika jana katika Uwanja wa Kibandamaiti mjini Unguja, ulitawaliwa na kauli za wazungumzaji kuwashambulia Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Katika mkutano huo ambao ulihudhuriwa na viongozi waandamizi wa CCM, kila aliyesimama kuzungumza hakuacha kuwataja wajumbe wa Ukawa na kuwashutumu wajumbe wake wa Bunge Maalum la Katiba kwa hatua yao ya kuondoka katika Bunge hilo Aprili 16, mwaka huu.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, alimtaka Msajili wa Vyama vya Siasa kuiangalia Ukawa kama ina usajili wa kisiasa au ni shirika lisilo la kiserikali.
Balozi Iddi alisema kama haijasajiliwa kisiasa, ipigwe marufuku kwa kuwa haina maana yoyote wala manufaa.

Alidai kuwa Mwakilishi wa Mji Mkongwe, Ismail Jussa Ladhu, hana imani na Wazanzibari na amejivisha koti la Zanzibar wakati siyo Mzanzibari.

Alisema anayo mengi ya kueleza kuhusu Jussa, lakini kutokana na muda kutotosha atamzungumzia katika mkutano mwingine.

Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, alisema sera ya Ukawa ni kutembea Tanzania nzima kutafuta uongozi kutokana na kutokuwa na wanachama.

Alisema kuwa lengo la Ukawa kutembea nchi nzima ni kwamba CUF watapata serikali Zanzibar na Chadema Bara, na kusema kwamba hilo ni jambo lisilowezekana kwa kuwa kama walishindwa mwaka 1995, 2000, 2005 na 2010 itakuwaje washinde mwakani.

Asha Bakari, Mwakilishi wa Viti Maalum na Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, alisema Ukawa hawaitakii mema Zanzibar na kwamba lengo lao ni kuvunja Muungano.

Alisema anawashangaa CUF kwamba wameingia katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa, lakini ni wasaliti, na kuongeza kuwa wanachama wa CCM watamuomba Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, kutoendelea na Serikali ya Umoja wa Kitaifa miaka mitano itakapoisha mwakani.

Aliwahakikishia wananchi kuwa Katiba itapita na itakuwa ya muundo wa serikali mbili na kwamba kilichobaki ni wananchi kupiga kura ya maoni na kuiunga mkono.

Alisema CCM itaendelea kusimamia mfumo wa Serikali mbili na kuwa katika Muungano zipo kero kadhaa, lakini watahakikisha wanazishughulikia.

Miongoni mwa mambo aliyozungumza ni umiliki wa mafuta na gesi, Zanzibar na kupata fursa za kiuchumi. Aliwataka wajumbe 201 wa Bunge Maalum la Katiba wakae pamoja na wajumbe wa CCM ili kujadili Rasimu ya Katiba na kutatua kero za Muungano.

Salmin Awadh Salmin, Mwakilishi wa Magomeni na Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, alisema wajumbe wa Bunge Maalum kutoka CCM wataendelea kuijadili Rasimu ya Katiba na kupitisha muundo wa Serikali mbili bila kuogopa vitisho vya Ukawa.

Alisema kwa kuwa Ukawa wamesema watazunguka nchi nzima, na wao (CCM) watahakikisha kwamba watakapokanyaga Ukawa nao watakanyaga.

Awadh alisema Ukawa wamekimbia bungeni kutokana na kutokuwa na hoja za msingi za kutetea Serikali tatu.

Alisema jukumu la Tume ya Jaji Warioba limekwisha na sasa liko mikononi mwao na kwamba wana uwezo wa kufanya lolote bila kuwapo mtu wa kuwaingilia.
Awadh alisema CCM watarejea Zanzibar na Serikali mbili na hakuna Serikali tatu.

“Ukawa hawana sababu za kukimbia, kama ni wajasiri tupambane bungeni,” alisema.

Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM na Mbunge wa Songea Mjini, Dk. Emmanuel Nchimbi, alisema Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, aliandika kitabu mwaka jana kupinga muundo wa serikali tatu, hivyo mapendekezo ya Tume ya Warioba yanamsuta.

Mwakilishi wa Kwa Mtipura, Hamza Hassan Juma, alisema hoja za Wazanzibari zilikuwa Serikali mbili wakati wa kukusanya maoni ya wananchi kwamba CUF walitaka Serikali ya Mkataba na CCM Serikali mbili na kuhoji Tume ilipata wapi maoni kuwa Wazanzibari wanataka Serikali tatu.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment