WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Saturday, November 9, 2013

Wasomi waifagilia hotuba ya Rais Kiwete

Dk. Benson Bana
Baadhi ya wasomi na wanasiasa wameunga mkono hotuba ya Rais Jakaya Kikwete kuhusu msimamo wa Tanzania kubaki kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki na kuufananisha msimamo huo na ule alioutoa Hayati Julius Nyerere mwaka 1965 alipozikemea Kenya na Uganda kuhusu Jumuiya hiyo kabla haijavunjika.
Akizungumza na NIPASHE Jumamosi, Profesa Kalamagamba Kabudi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema hotuba ya Kikwete ilijaa msimamo wa nchi kuhusiana na chokochoko za kuvunja Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), zinazofanywa na Kenya, Uganda na Rwanda.

“Hili si tamko la kwanza kwa viongozi wa nchi hii, 1965 Nyerere alitoa hotuba kali kwa Marais Jomo Kenyatta wa Kenya na Milton Obote (Uganda), wakati zilipoleta chokocho kama hizo,” alisema Profesa Kabudi.

Kabudi alisema nchi hizo mara nyingi huisingizia Tanzania kwamba ndio wavunjaji wa Jumuiya hiyo, lakini sasa itaonyesha ni dhahiri nchi zote zinatakiwa kurejea katika meza ya majadiliano.

Alisema katika Jujmuiya iliyovunjika 1977, Kenya ndiyo iliyonufaika zaidi kwa kuwepo na viwanda vingi toka kwa nchi mabeberu, Marekani na Uingereza, hivyo kuamua kuibagua Tanzania kwa sasa kutokana na nchi hiyo kuogopewa na mabeberu.

“Nchi yetu inaonekana ndogo, lakini mabeberu wanaihofia sana hivyo kuamua kuzitumia nchi hizo ziitenge Tanzania kutokana na kusimamia kidete ardhi yake inayotamaniwa na nchi hizo,” alisema.

Hata hivyo, alisema Tanzania haiwezi kuhofia kwa nchi hizo kujiona ni majirani wakati imezungukwa na majirani wa ‘damu’ kama nchi ya Msumbuji, Zambia na Malawi ambao makabila ya huko yanapatikana nchini.

Naye mhadhiri mwingine wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Benson Bana, alisema hotuba ya Kikwete inatakiwa iwekwe kwa lugha ya Kiingereza na kupelekwa katika nchi za jumuiya hiyo ichapishwe na kusomwa na wananchi wao.

“Ni hotuba nzuri na yenye msimamo wa nchi, inatakiwa itafsiriwe kwa lugha ya kiingereza ili nchi hizo ziweze kuisoma kwenye mitandao ya kijamii,” alisema Dk. Bana.
Alisema pamoja na hotuba hiyo, lakini Rais alitakiwa kuzungumzia yale ambayo aliyazungumza na Rais Uhuru Kenyatta na Yoweri Museveni walipokutana Afrika Kusini hivi karibuni.

Hata hivyo, Bana alisema pamoja na msimamo huo wa serikali, lakini Kikwete anatakiwa kuwapoza makali mawaziri wake, Bernard Membe wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa pamoja na Waziri wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta kuhusu misimamo yao mikali ya nchi hizo kutaka kuitenga Tanzania.

“Kweli mawaziri hao wanachukia kuona nchi hizo zinavyofanya kwa kuitenga Tanzania, lakini yale wanayoyazungumza yanawapa sintofahamu watanzania…ni vizuri Rais alivyotolea ufafanuzi wa kutojitoa EAC ili kukwepa lawama,” alisema.

Profesa mchumi, Ibrahim Lipumba ambaye ni mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), alisema baada ya kuona nchi hizo tatu zinataka kuitenga Tanzania, inachotakiwa ni kujipanga na kuiimarisha bandari ya Dar es Salaam na njia za reli.

“Kwanza inatakiwa kuimarisha miundombinu yetu ya bandari na reli…bandari ya Dar meli inachukua mwezi mmoja kupakua mizigo wakati Mombasa ni siku tatu hadi nne, njia za reli zimekuwa mbaya, tuimarishe kwanza hizo,” alisema Profesa Lipumba.
Aidha, alisema pamoja na hotuba hiyo ‘kuwakuna’ walio wengi, lakini alimtaka katibu wa EAC kutoegemea nchi aliyotoka bali azungumze yale yaliyopo ndani ya jumuiya katika vikao husika kama mtendaji mkuu.

UVCCM YAMPONGEZA
Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) umempongeza Rais Kikwete kwa uamuzi wa kihistoria uliolenga maslahi ya nchi.

Katika taarifa iliyotolewa na Naibu Katibu wa UVCCM Taifa Zanzibar, Shaka Hamdu Shaka, alisema Rais ameonyesha ukomavu wa hali ya juu, upeo na mazingatio ya kidiplomasia.

Alisema Rais Kikwete, ameonyesha mustakabali wa uhai na ustawi wa Tanzania na ameweza kuwafungua macho wananchi kuhusu jumuiya hiyo.

Alisema kitendo cha viongozi wa nchi tatu wanachama wa EAC yaani Kenya, Uganda na Rwanda kukutana faragha na kuiacha kando Tanzania, hakijengi na badala yake kuwepo na uungwana na kuheshimu juhudi za pamoja zinazoweza kuleta maendelo ya Jumuiya hiyo.

“Hatua hiyo ni dhaifu mno, inayoweza kumlazimisha yeyote alazimike kutafsiri usiri kati ya viongozi hao, kuwa inabeba ajenda tete isiofikirika miongoni mwa nchi wanachma,” alisema Shaka.

Shaka alisema UVCCM inapongeza umakini wa Serikali ya Tanzania katika kujenga misingi ya uvumilivu kutoharakisha kujiingiza na kukubali kuharakishwa kwa shirikisho la kisiasa, Uhamiaji, Ajira na Ardhi.
Aliunga mkono hatua ya serikali kutaka mambo yote yalioanishwa katika mkataba wa Afrika Mashariki yaheshimiwe na wananchi katika nchi wanachama kushirikishwa katika maamuzi.

Alisema Rais ametumia muda muafaka kuelezea kwa upana mchakato wa kupatikana Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Shaka alisema mazingira hayo kiuhalisia na uhakika wake yanaonyesha kupatikana kwa Katiba mpya shirikishi iliowajumuisha kwa pamoja wananchi wa Tanzania na kwamba mchakato wake ni wenye mapana ya demokrasia na utengamano wa pamoja.

*Habari hii imeandaliwa na Daniel Mkate na Beatrice Shayo
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment