WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Sunday, November 10, 2013

Wanyarwanda wanamkumbuka Nyerere



 MWALIMU Nyerere
MWALIMU Nyerere alikuwa Baba wa Taifa la Tanzania, Baba wa Afrika na Baba wa watetea haki za binadamu duniani kote. Jambo hili linajidhihirisha kila mwaka watu wanapokusanyika kumkumbuka na kumwombea.

Sala kubwa ni ile ya kumtaka Mwenyezi Mungu, kumweka kwenye kundi la watakatifu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Hapa Tanzania, kila mwaka Oktoba 14 ni Siku ya Nyerere (Nyerere Day) na ni siku ya mapumziko. Afrika Kusini nao siku hii ni ya   kumkumbuka Mwalimu kwa majadiliano na tafakuri, juu ya mawazo yake na mawazo mengine yanayofanana na ya Mwalimu ya haki za binadamu na masuala ya uchumi wa dunia hii ya Utandawazi.

Kule Amerika, wapenda amani na watetezi wa haki za binadamu wanakusanyika kusali na kuomba siku ya kukumbuka kifo cha Mwalimu Nyerere. Serikali ya Rwanda, imetangaza rasmi Oktoba 14 ni Nyerere Day, ni siku ya kitaifa na watu wanapumzika siku hiyo. Wanyarwanda wanasema kumbukumbu ya Mwalimu ni sherehe, maana Mwalimu aliacha mambo mengi mazuri nyuma yake.

Sherehe hizi za kumkumbuka Mwalimu nchini Rwanda zinaratibiwa na Jumuiya ya Urafiki baina ya Wanyarwanda na Watanzania – RWATAFA (Rwanda Tanzania Friendship Association).

Kwa faida ya msomaji wa makala hii ni bora kutambua kwamba RWATAFA ina ndugu yake Tanzania,  Jumuiya ya Urafiki baina ya Watanzania na Wanyarwanda –TARAFA (Tanzania Rwanda Friendship Association). Kwa pande zote mbili Jumuiya hizi za urafiki zimesajiliwa na kutambuliwa kisheria.

Mwaka huu sherehe za kumkumbuka Mwalimu Nyerere zimefanyika Novemba 3, 2013 kwenye Ukumbi wa  Hoteli ya Nobleza mjini Kigali kwa ibada nzuri ya misa iliyoongozwa na mapadri wawili na baadaye nyimbo, mashairi na hotuba za kumkumbuka Mwalimu Nyerere.

RWATAFA, chini ya Mwenyekiti wake Mzee Isidore Gahamanyi katika jitihada zake za kutaka kudumisha undugu na urafiki na TARAFA, iliamua mwaka huu kuwaalika familia ya Mwalimu Nyerere, iliyowakilishwa na Madaraka Nyerere pamoja na Makongoro Nyerere, pia waliwaalika Makamu Mwenyekiti wa TARAFA, Mzee Patrick Qoor na mwandishi wa makala hii.

Sherehe za kumkumbuka Mwalimu, zinatanguliwa na matembezi ya maeneo ya kihistoria na hasa sehemu za Kumbukumbu ya mauaji ya kimbali. Mwaka huu RWATAFA iliwatembeza wageni wake kwenye kumbukumbu ya Murambi ambako hadi sasa miili elfu moja inatunzwa.

Miili hii imetunzwa kwa utaalamu wa hali ya juu, kiasi cha miili hiyo kutoa picha ya aina ya kifo; kukatwa kwa panga, kupigwa nyundo kichwani, kufungwa mikono na miguu, kubakwa na kuingiziwa mti kwenye sehemu za siri hadi mti huo ukatokea mdomoni hasa kwa wanawake, watoto wadogo kupasuliwa vichwa na mateso mengine mengi ya kinyama.

Hapa ndipo mtu anaposhuhudia unyama uliofanywa wakati wa mauaji ya Kimbali. Wanyarwanda wameendelea kuitunza miili hii na kuionesha kwa watu ili watambue ubaya wa ubaguzi na ubaya wa siasa zenye propaganda chafu.

Kila mtu akifika hapa na kujionea mwenyewe, anakuwa na maswali mengi rohoni mwake. Binafsi, kila nikitembelea makumbusho haya ambayo ni mengi nchini Rwanda, swali langu ambalo hadi leo hii halina majibu ni kwa nini mauaji haya yalitokea?

Chuki hii kubwa hivyo kiasi cha kuwaua watu kinyama na mbaya zaidi hata kuwaua watoto wadogo ambao umri wao haukufika mwaka mmoja, ilitoka wapi? Nini chanzo cha chuki hii? Ni propaganda za Wafaransa? Ni siasa mbaya? Ni nini? Ni imani yangu kwamba jibu litapatikana siku moja.

Wanyarwanda wanamkumbuka na kumuenzi Mwalimu kwa heshima kubwa. Binafsi nimeshuhudia jambo hili. Wanyarwanda wanasema wana sababu nyingi za kumkumbuka Mwalimu.

Wanasema,  baada ya vita ya 1959, Umoja wa Mataifa uliamua wakimbizi wa Rwanda wapelekwe Canada, lakini mwalimu alikataa na kuwapatia hifadhi Tanzania na kwamba wakimbizi wa Rwanda waliokwenda Burundi, DRC na Uganda, hawakupata uraia wa nchi hizo, lakini wale waliokimbilia Tanzania walipatiwa uraia, walisoma kwenye shule za serikali, walitibiwa kwenye hospitali za serikali na walipata huduma zote kama Watanzania wengine, na kwamba mauaji ya kimbali yalipotokea, Mwalimu Nyerere, alikuwa kiongozi wa kwanza duniani kukemea na kuyalaani mauaji hayo.

Seneta Kamanzi, akitoa wasifu wa Mwalimu Nyerere, bila kutafuna maneno alisema; “Mwalimu, alihoji watu kuitwa wakimbizi. Hakulipenda neno hili, alipendekeza wakimbizi waitwe ‘wageni wakazi’. Nina imani kama Mwalimu angekuwa bado hai angepinga kwa nguvu zake zote msamiati huu wa kibaguzi wa wahamiaji haramu.”

Uwepo wa watoto wa Mwalimu kwenye sherehe hizi ulileta mvuto wa aina yake. Madaraka na Makongoro, walielezea wanavyomfahamu baba yao; mtu ambaye hakuwa na ubaguzi; aliipenda nchi yake na kulipenda Bara zima la Afrika.

Wote wawili kila mmoja kwa namna yake; Makongoro mwanasiasa na Madaraka mtafiti na mtunzaji wa kumbukumbu za Mwalimu kule Butiama, waliziimba na kuzielezea kwa ufasaha sifa za Mwalimu na kuelezea wazi kwamba hata Mwalimu alitambua upungufu wake.

 “Mwalimu, alikuwa akitwambia kuwa yeye si malaika, naye ana makosa yake, lakini alisisitiza tuige mazuri yake na kuachana na makosa yake,” alieleza Madaraka Nyerere.

Rwanda kuna utulivu na amani. Pamoja na misuguano ya kisiasa iliyojitokeza hivi karibu kati ya Tanzania na Rwanda, bado Wanyarwanda wana imani kubwa na Watanzania.

Wanaamini siasa ni siasa, zitakuja na kupita lakini udugu wa Watanzania na Wanyarwanda utadumu milele. Nchi hii ya jirani ni fursa nzuri kwa Watanzania kwenda na kuwekeza. Kuna Watanzania ambao wameanza kuwekeza Rwanda na wataalamu wengi wanaofundisha kwenye vyuo vya Rwanda wanatoka Tanzania.

Hata hivyo bado kuna nafasi kubwa ya kuwekeza nchini Rwanda. Nchi hii sasa hivi inapiga hatua kubwa ya maendeleo. Mji wa Kigali ni msafi kuzidi miji mingi, ikiwamo baadhi katika nchi za Ulaya. Hata kama si kuwekeza, kuna mambo mengi ya kujifunza kutoka Rwanda.

Hakika, kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Kigali, ni tukio la kujenga undugu kati ya Tanzania na Rwanda. Na jambo la kufurahisha ni kwamba undugu huu unajengwa katika ngazi ya wananchi kwa wananchi. Ni imani ya RWATAFA na TARAFA kwamba undugu ukijengeka baina ya wananchi wa nchi hizi mbili, serikali zitatekeleza zinataka zisitake.

No comments:

Post a Comment