WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, August 2, 2013

Ni hatari vyama vya siasa kuunda vikosi vya ulinzi




KUMEKUWA na mjadala juu ya dhana ya vyama vya siasa kuunda vikosi vyake vya ulinzi. Hivyo basi, kuunda vikosi vyake vya wanamgambo.

Inavyoonekana, kama nchi, kuwa tungali kwenye ile hali ya delirium ambayo nilipata kuielezea ni hali ya mwanadamu kuwa katika mkanganyiko (kuchanganyikiwa). Ni maradhi. Tunayoyashuhudia sasa ni dalili za kuwa tumo kwenye hali ya Mkanganyiko- Delirium.

Naam, kama nchi inatupasa tukae chini na kuitafakari nchi yetu na mustakabali wake. Maana tumeanza kushindwa kutofautisha kati ya chama cha siasa na chama cha ukombozi. Mathalan, TANU ilikuwa Chama cha Ukombozi. TANU ilipigania uhuru wetu.

TANU chini ya utawala wa ukoloni ilihitaji kuunda kikosi cha vijana wake kwa madhumuni ya kuwalinda viongozi wake na hata kuwaandaa kuwa makamanda kwenye mapambano. Ndipo kukawa kilichoitwa  “TANU Youth League” na humo ndani kukawa na vijana wenye majukumu ya ulinzi kwa chama na viongozi wake.

Sasa basi, nchi inapokuwa huru hakuna haja ya vyama vya siasa kuwa na vikosi vyake vya ulinzi. Kazi hiyo inaachwa kwa vyombo vilivyoundwa kwa kazi hiyo. Kinachotaka kutokea kwa nchi yetu kwa sasa ni jambo la hatari sana. Kwamba tunafikiri kuruhusu vyama vya siasa kuwa na vikosi vyake vya kujilinda.

Na huu ni wakati, kwa Watanzania, bila kujali tofauti zetu za  kiitikadi, kidini au rangi, tukemee kwa sauti moja jambo hili. Kamwe tusikubali ikawa ni vitu vya kawaida kwa vyama kuwa na vikosi vya vya wanamgambo.

Maana, uzoefu unatuambia, kuwa harakati za vikosi vya wanamgambo wa vyama huambatana na vitendo vya kulipiza kisasi. Na hilo ni jambo baya sana.

Maana, hapo ndipo chuki inapozaa chuki na hatimaye Watanzania kuanza kuchinjana wenyewe kwa wenyewe. Yale tuliyokuwa tukiyasikia yakitokea kwenye nchi za wenzetu tutaanza kuyaona nchini mwetu.

Tunaamini, Watanzania kwa ujumla wetu ni watu tunaopenda amani na utulivu. Hata hivyo, kundi linaloweza kwa haraka kuvuruga amani na utulivu wetu ni kundi la wanasiasa.

Tunaona sasa, dalili ya baadhi ya wanasiasa, hata kwa kuvihusisha vyama vyao, kuwa tayari kutumia risasi na mapanga ili mradi wafanikishe malengo yao ya kisiasa.

Watanzania tunapaswa kuwa makini. Tunachopitia sasa ni kipindi kigumu sana. Kuna walio tayari  kupandikiza chuki miongoni mwetu ili tuanze kuchinjana wenyewe kwa wenyewe kwa kisingizio cha tofauti zetu za kiitikadi, kidini, kikabila na hata rangi zetu.

Tufanye nini? Hakika, tutafanya makosa makubwa kama kuna watakaodhani, kuwa madhara ya harakati za wanamgambo wa vyama vya siasa hayatawahusu wao.  

Vyama vya siasa vilivyo makini na vinavyoitakia mema nchi yetu, vianze sasa kuachana na utamaduni wa kuwa na wanamgambo- ama vikundi vya vijana wanaopewa mafunzo ya kijeshi kwa masuala ya ulinzi.

Historia inatufundisha kuwa Afrika  ‘Parties militia guards’ ama vikundi vya wanamgambo vya vyama vya siasa huwa chanzo cha kuharakisha vurugu za kisiasa za wenyewe kwa wenyewe katika nchi na hata kuwa chanzo cha mauaji. Tumeona Rwanda, Burundi, Jamhuri ya Kongo na kwingine Afrika.

Ni vikundi hivi vya wanamgambo wa vyama ambavyo hutumika na vyama, wanasiasa, au hujituma vyenyewe kufanya kazi ya kulipiza visasi vya kisiasa kwa kutumia silaha.  

Hapa kwetu tayari, vyama vikubwa vya siasa vina vikundi vya aina hiyo; CCM wana ‘Green Guards’, CHADEMA wana ‘Red Brigade’ na CUF wana ‘Blue Guards’.

Katika nchi ya kisasa si busara kuwa na utaratibu unaoruhusu vyama vya siasa kuwa na vikundi kama hivyo vya vijana vyenye kupata mafunzo ya kijeshi.

Na hakika, Katiba yetu ijayo itusaidie kuondoa utaratibu kama huo wa ‘kijima’ kwa kuweka marufuku ya vyama vya siasa kuunda vikosi vya vijana vyenye kukaa kambini na kupata mafunzo ya kijeshi, vikosi ambayo, vinaweza kuja kutumika vibaya na kutusababishia madhara makubwa kama taifa.

Kama vyama vitahitaji ulinzi kwenye shughuli zake, basi, viombe ulinzi kwenye kampuni za ulinzi zinazotambulika kisheria na zisizofungamana na siasa za vyama.

Vinginevyo, tuhakikishe jeshi letu la polisi linaimarishwa na linakuwa chombo cha usalama kinachoaminika na umma, kisichoegemea kwenye itikadi za vyama katika kufanya kazi yake. Vivyo hivyo, kwa vyombo vingine vya usalama katika nchi ikiwamo Idara ya Usalama wa Taifa. Vifanye kazi zao kwa kutanguliza maslahi ya taifa na si ya wanasiasa au vyama vyao. Ni rai yangu.

No comments:

Post a Comment