WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Saturday, August 24, 2013

Je, tunaweza kuzitambua sifa za uongozi?




NIMESEMA huko nyuma kwamba tumejenga nakisi kubwa ya uongozi, na matokeo yake ni jamii yetu, kwa kiasi kikubwa, inaendeshwa na maofisa, watu waliokabidhiwa ofisi. Hawa ni tofauti kabisa na viongozi, kwa sababu, kama ambavyo nimeeleza mara nyingi, inawezekana kiongozi akawa pia ni mtawala, lakini si kila mtawala ni kiongozi.

Kiongozi ni yule anayeonyesha njia, kwa maneno yake, tabia yake na matendo yake, hata kama hana ofisi na hajakabidhiwa kazi inayoitwa ya “uongozi” kama ambavyo tumezoea nchini mwetu. Haiwezekani kwamba kila anayeteuliwa kuwa mtendaji wa kata, au mkuu wa wilaya, au mkuu wa mkoa, waziri, akawa ni kiongozi kwa sababu tu kateuliwa kushika ofisi hiyo. Uongozi ni zaidi ya ofisi.

Kila medani ya maisha ya kijamii inao viongozi wake, na wingi wao wala hawajachaguliwa kwa kura na wala hawajateuliwa na yeyote. Wengi pia hawalipwi mshahara na hawapokei posho, lakini ni viongozi kwa sababu wanaonyesha njia na wenzao wanawafuata.

Kiongozi hujitokeza, hateuliwi. Katika jamii za jadi wazazi na wakuu wa jamii waliweza kumtambua mtoto ambaye angekuja kuwa kiongozi. Kwa mfano kuna mashindano ya mchezo kama soka. Timu mbili zinashindana na zinahitaji mwamuzi lakini hakuna mtoto anayekubali kuacha kucheza ili awe mwamuzi.

Watoto wenyewe wanaamua kumpata mwamuzi ambaye ni mchezaji wa mojawapo ya timu mbili zinazoshindana.  Wanamkubali kuwa mwamuzi ingawa anaichezea timu yake kwa sababu wanamjua ni mtenda haki. Anachezesha mechi na inapobidi anachukua uamuzi dhidi ya timu yake mwenyewe. Huyo ni kiongozi; atafaa kuwa hakimu.

Mtoto mwingine atajipambanua na wenzake kwa ujasiri wa kukabiliana na tishio linalomkabili yeye na wenzake, na atawaongoza wenzake katika kukabiliana na hatari yoyote ile, akiwaelekeza kuhusu mbinu za kutumia kupambana na adui. Huyo naye ni kiongozi; atafaa kuwa kamanda wa kijeshi au mtaalamu wa usalama.

Mwingine ataonyesha umahiri mkubwa katika kufanya biashara na kutengeneza faida kwa kujinyima na kuwekeza vyema. Huyo naye atakuwa kiongozi, na ataweza kuilekeza jamii katika masuala ya kiuchumi.

Watoto huonyesha dalili hizi wazi wazi, na wakuu wa jamii wenye maono ya kiuongozi huwatambua watoto wa aina hiyo wakiwa bado wadogo, na kisha huwaelekeza kwa kuwasaidia kukuza vipawa vyao.

Katika marika ya jando na unyago watoto wenye mwelekeo wa uongozi walitambuliwa kirahisi zaidi na walijitokeza kuwaongoza wenzao katika mitihani mingi waliyokabiliwa nayo. Katika unyago kwa kisasa, ambayo ni elimu ya shule, kiongozi wa aina hiyo hujitokeza na kuwa ama kiranja au kiongozi wa migomo pale wanafunzi wanapohisi kwamba hawatendewi haki.

Ni hususan shuleni (pamoja na vyuoni) wanapochomoka viongozi wa baadaye. Katika shule za kimapokeo (za kizamani) walimu waliwateua watoto wakubwa wa mwili na wakali wa tabia kuwa viranja na monita. Katika shule za kisasa wanafunzi wenyewe huchagua viranja wao na kuwaheshimu badala ya kuwaogopa kama ilivyo kwa shule za kizamani.

Inapotokea kwamba wanafunzi wanahisi kwamba wanaonewa kwa njia yoyote ile, viongozi wa wanafunzi hujitokeza na kuongoza ama majadiliano baina ya wanafunzi na utawala wa shule, ama mgomo wa wanafunzi pale majadiliano yanapokuwa hayana tija. Viongozi wa migomo shuleni mara nyingi hukua na kuingia katika harakati za kisiasa ama za vyama vya wafanyakazi; aghalabu huwa ni watu wa kudai na kutetea maslahi ya wenzao.

Kama vile ambavyo viongozi wa wanafunzi wakati wa migomo na misuguano baina ya wanafunzi na walimu hujikuta mara kwa mara wanapewa adhabu, pia viongozi wa kisiasa nao hujikuta wakikamatwa, wakipigwa au hata kuuawa.

Kama ilivyo mtaani na shuleni wakati wa utoto, pia katika umri mkubwa (ofisini, kiwandani, majeshini, katika biashara) kiongozi ni mtu anayesema wazi kile anachokiamini na kukitetea bila kutafuna maneno. Kiongozi ni mtu wa kujitolea nafsi yake, wala si mtu wa kutumia nafasi ya uongozi kupata faida binafsi juu ya wengine.

Anaposafiri nchini na kuona hali duni ya maisha ya watu wake, kiongozi anasononeka na anazidi kukuna kichwa akitafuta namna ya kuwaokoa watu wake watokane na umasikini huo. Akikuta eneo ambako wananchi wake wana neema anafurahi kuwaona walivyonawiri, mashamba yao yalivyostawi, mifugo yao ilivyonona; hatafuti njia za kuwanyang’anya kwa ujanja mashamba yao au mifugo yao. Ukwasi wa raia ndiyo furaha ya kiongozi, si ukwasi wake binafsi.

Tukizirejea sifa hizi za uongozi, tutang’amua kwamba kama tunao viongozi basi wataenea katika kiganja cha mkono. Katika maeneo mengi, katika nafasi nyingi, katika ngazi zote za maisha tumeelemewa na watu wanaopenda kujiita viongozi lakini hawana hata chembe ya uongozi.

Walio wengi ni watu wema, waungwana, wapole, watu ambao ungependa kuwa nao mtaani kama majirani. Lakini hawana sifa za uongozi; ni wema na waungwana tu, basi, lakini si viongozi kwa sababu hawajui ni wapi wanataka kuipeleka jamii.

Mbali ni hawa, wako wachache ambao si tu kwamba hawana sifa za uongozi lakini kibaya zaidi ni kwamba ni majambazi, wazandiki, wanafiki na madhalimu waliojiingiza katika nafasi za “uongozi” kwa kila aina ya hila, na ambao wanatumia nafasi zao usiku na mchana kuiba, kudhulumu, kupora, kunyang’anya na kukwapua.

Tukichanganya wale wema wasio na sifa za uongozi na hawa majangili tunachopata ni jumla ya uongozi dhaifu usioweza kuonyesha mafanikio ya kweli katika kuboresha maisha ya wananchi, hata pale ambapo ni dhahiri kwamba uwezo wa rasilimali ni mkubwa. Sifa moja ya uongozi mbovu ni pale watu wanapokufa kwa kiu huku wamezungukwa na maji.  

Source:www.raiamwema.co.tz: Jenerali Ulimwengu

No comments:

Post a Comment