WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, July 11, 2013

K aponda mpango wa Chadema



Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete 

Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete (pichani) amekiponda Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa kuanzisha kikundi cha mgambo akisema hatua hiyo imejidhihirisha kwamba chama hicho hakipendi amani.

Ingawa Kikwete hakuitaja Chadema kwa jina, lakini chama hicho ndicho pekee kilichosusia kongamano la kutafakari amani kikidai kwamba Serikali haitendi haki.
Kikwete alisema hayo jana wakati akifunga kongamano hilo lililoandaliwa na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD).

Chadema ilisusia kongamano hilo ikisema kuwa amani haitafutwi kwa kufanya makongamano kama ilivyofanya TCD.

“Chama cha siasa kuanzisha kikundi cha wanamgambo kwa ajili ya kupiga watu ni kiashiria kwamba chama hicho hakitaki amani bali kinaridhishwa na vurugu,” alisema Kikwete na kuongeza kuwa wanaopenda amani humaliza tofauti zao kwa kuzungumza.

“Tusiiache nchi yetu ije kulindwa na majeshi ya Umoja wa Mataifa, tusije kufikia huko, tujitahidi kuondoa tofauti zetu kwa njia ya mazungumzo,” alisema Kikwete.

Juzi Chadema walitangaza kwamba wataanzisha mafunzo kwa vijana wao kwa ajili ya kuwalinda ikidai kuwa dola imekuwa haisikilizi madai yao.

Alisema wanaosusa kongamano hilo wangeweza kufika wangeweza kutoa madukuduku yao kwa sababu viongozi wa Serikali na polisi walikuwapo lakini bado hawataki.

“Sasa hawa kweli wanapenda amani yetu wakati hawapendi kuja tuzungumze, wanataka watu wauane ama wapigane,” alisema kwa mshangao Kikwete.

Alisema Serikali na viongozi wake hawapendi vurugu na kwamba chama hicho kinafanya vurugu hizo ili kuwatoa katika ajenda za kuwaletea maendeleo Watanzania.

Hata hivyo aliwapongeza Chadema kwa kushiriki katika maandalizi ya kongamano hilo licha ya kususia kushiriki.

Wakati huohuo, Rais Kikwete amesema kuwa vita vya Kagera iliyotokea mwaka 1978 -1979 ilisababisha madhara makubwa ya mtikisiko wa kiuchumi na kusababisha kutetereka kwa utoaji wa mafunzo ya Jeshi la Wananchi katika kipindi cha miaka kumi.

Akizungumza katika kilele cha Maadhimisho ya Miaka 50 ya Jeshi la Kujenga Taifa, JKT, Rais Kikwete alisema kuwa katika kipindi hicho, JKT imepitia katika changamoto nyingi ambazo zilisababisha kutetereka kiuchumi na kiutendaji hasa baada ya kutokea kwa vita ya Kagera.

“Hali mbaya ya uchumi katika kipindi cha miaka ya sabini mpaka tisini iliathiri hali ya utoaji wa mafunzo na kusababisha kutetereka na hii ilisababishwa na vita ya Idd Amin ya miezi minane tu ambayo ilichukua miaka mingi Serikali kurudi katika hali yake,”alisema Kikwete.

Alisema kutokana na sababu mbalimbali za kiuchumi zikiwamo kupanda kwa bei ya mafuta duniani, Serikali ililazimika kufunga mafunzo ya JKT mwaka 1993.

Alisema 1994 shughuli za msingi katika jeshi hilo zilitetereka na kubaki shughuli za kulinda kambi tu ambapo hakukuwa na wanajeshi wapya waliokuwa wanajiunga na jeshi hilo.

“Nakumbuka Nyerere kipindi kile alisema tuna miezi 18 ya kufunga mikanda ili kuweka mambo sawa baada ya vita ya Idd Amin lakini mimi nakumbuka ilituchukua zaidi ya hiyo miezi hiyo kwa wale waliokuwapo kile ndo kilikuwa kipindi shida,”alisema Kikwete.

Alisema JKT iliundwa mwaka 1963 likiwa na vijana 11 kutoka mikoa 11 ya Tanzania Bara ambapo lengo lilikuwa ni kujenga uzalendo na utaifa kwa vijana ili kuwa na taifa la watu wenye uchungu na nchi yao.

Alisema suala la kufufua mafunzo ya JKT kwa vijana ni moja ya ahadi aliyoiweka mwaka 2005 alipoingia madarakani ambapo Machi 26 ilitimizwa ahadi hiyo na kuanza upya kwa mafunzo ya lazima kwa mujibu wa sheria.

Alisema katika mafunzo hayo ambayo yaliongozwa na viongozi wa kitaifa wakiwamo wabunge na vijana waliomaliza masomo kutokana na kuamini kuwa hakuna chombo chochote kinachofundisha misingi ya utaifa kama jeshi.

source: mwananchi

1 comment:

  1. Binafsi, nilisoma kwa makini tamko la CHADEMA, likielezea historia ya serikali ya CCM kushindwa kufanya haki. Tamko lilielezea jinsi CHADEMA wanavyoonewa, na mimi kama raia ambaye sina chama nimeshuhudia hayo.

    Polisi wanaikingia kifua CCM na kuihujumu CHADEMA. Rais Kikwete mwenyewe, miezi kadhaa iliyopita, alituambia kuwa wako wat wa CCM ambao hutumia polisi kuwahujumu wapinzani.

    Kauli ya Rais Kikwete kuhusu watu kuanzisha mgambo wa kupiga watu ni kauli ya ajabu, kwani hicho sio kilichosemwa na CHADEMA. CHADEMA wameongelea kujilinda. Binafsi nasema kuwa kwa vile vyombo vinavyopaswa kuwalinda, na kutulinda sote, haviwajibiki, CHADEMA inayo haki ya kujilinda.

    Sielewi kama Rais Kikwete alikuwa usingizini alipotoa kauli yake. Lakini hii si mara yake ya kwanza kutoa kauli inayopingana kabisa na ukweli. Alipoongelea suala la madai ya watu wa Mtwara, alipindisha kabisa madai ya watu wa Mtwara.

    Yawezekana ni washauri wake ndio wanaofanya ufedhuli huu wa kumpotosha Rais. Vinginevyo, siamini kama Rais Kikwete amekosa akili kiasi cha kusema mambo ya ajabu ajabu, yenye kuongeza utata wa matatizo.

    ReplyDelete