WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Sunday, February 23, 2014

Vita ya uenyekiti Bunge la Katiba

Andrew Chenge na aliyekuwa Spika wa Bunge, Samuel Sitta, ambao wametajwa kutaka kuwania nafasi ya uenyekiti wa Bunge la Katiba wakipeana mikono siku za hivi karibuni. 


Dodoma. Kadiri siku zinavyosogelea uchaguzi wa Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, ndivyo mpasuko ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) unavyozidi, kutokana na kuwapo kwa makundi mawili yanayojipanga kusimamisha wagombea na ambayo yameanza kuendesha kampeni kuchafuana.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa makundi hayo ni yale yanayomsaidia aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Andrew Chenge na aliyekuwa Spika wa Bunge, Samuel Sitta, ambao wametajwa kutaka kuwania nafasi hiyo.
Hata hivyo, wakati Chenge akiwa hayuko tayari kuthibitisha nia yake hiyo, Sitta hakupatikana jana kuzungumzia suala hilo. Lakini habari zinasema vigogo hao wameshajipanga kwa ajili ya mbio hizo za uchaguzi na sasa wanatafuta watu wa kuwasaidia.
Makundi hayo yalianza wakati wa kikao cha ndani cha CCM kilichofanyika mjini Dodoma chini ya Mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete, ambako habari zilisema, baada ya chama kumteua Pandu Ameir Kificho kuwania nafasi ya mwenyekiti wa muda wa Bunge la Katiba, mmoja wa wajumbe wa kikao hicho walimpendekeza Chenge kuwa mwenyekiti wa kudumu wa bunge hilo.
“Hapo ndipo mgogoro ulipoanza. Kwanza tulimkubali Kificho ili kupunguza wingu la ushindani kwenye uchaguzi wa mwenyekiti wa kudumu. Lakini wajumbe tulimkataa Chenge kwa hoja nzito na mwenyekiti alikubali na kuamua kuwa watu wakagombee bungeni.”
Tuhuma dhidi ya Chenge
Baadhi ya wabunge wa CCM wamesema ni ukweli ulio wazi kwamba Sitta na Chenge ndio wanaofaa kuwania nafasi hiyo, lakini mchuano utakuwa mkali kutokana na kila mmoja kuwa na ushawishi wa aina yake kwa wajumbe ambao ndio watakaopiga kura kumchagua mwenyekiti.
 “Wakati wa kuapa, wajumbe watatakiwa kushika Biblia au Qur’an. Ila tusema ukweli, unawezaje kufanya kiapo cha utii mbele ya mwenyekiti ambaye uadilifu wake unatia shaka? Alihoji mmoja wa wajumbe wanaomuungano mkono Sitta.
Mjumbe mwingine alisema Chenge hazuiwi kugombea, lakini ajiandae kujibu maswali makuu matatu, moja likihoji uadilifu wake wakati kuna mikataba mingi ya wawekezaji kwenye kampuni za madini iliyoshuhudiwa na yeye akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ni mibovu.
“Pia tutamtaka aeleze kwa nini alikubali Uenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Bunge la Jamhuri kwa uteuzi wa Spika, wakati kanuni zinasema wenyeviti wachaguliwe na wabunge wenyewe,” alisema mjumbe huyo ambaye hakupenda kutajwa jina lake.
Kauli ya Chenge
Chenge mwenyewe amepuuza tuhuma hizo akisema kuwa ni za watu wasiopenda kuelewa.
“Hayo yote na mengi zaidi nimeyasikia ndiyo maana nimeamua kuondoka Dodoma. Siko Dodoma nitarudi Jumatatu,” alisema Chenge na kuendelea;
“Lakini ndugu yangu, mi naona hakuna haja ya kulumbana na watu ambao hawataki kuelewa. Kama watu wanatuhumu, lakini hawana kielelezo cha kwenda nacho mahakamani, wanaambiwa kwa ushahidi kuwa tuhuma zao hazina msingi na hawataki kusikia, unadhani tutawafanyaje zaidi ya kuwaacha tu?”
Alipotakiwa kuthibitisha kuwa kweli ana mpango wa kugombea nafasi hiyo ya Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba alijibu;
“Chama kina utaratibu wake na mipango yake. Ni taasisi inayopaswa kuheshimiwa, kwa nini tulumbane leo wakati chenyewe kina msimamo wake juu ya hilo?”
Alipoulizwa tena kueleza namna anavyojiandaa kujibu maswali matatu magumu yanayoandaliwa na wapinzani wake, endapo atasimama kunadi sera zake akitakiwa kugombea nafasi hiyo alijibu;
“…Bwana! Chenge ni huyo huyo, chaguzi ni hizo hizo ambazo ameshinda mara kadhaa na nchi hii ni yetu sote.”
Sitta
Sitta hakupatikana jana kuzungumzia suala hilo, lakini mmoja wa wanaomuunga mkono ambaye hakutaka jina lake litajwe, amesema hawana shaka kwamba akisimama na Chenge kwa kura za haki, atapita.
Tayari kumeripotiwa taarifa za rushwa kwenye mbio hizo za kuwania nafasi ya Mwenyekiti wa Bunge la Katiba. Hata hivyo, Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameonya vitendo hivyo na kuzitaka jumuiya za CCM kuwa macho dhidi ya suala hilo.
Pinda alitoa karipio hilo jana alipokuwa akizungumza na Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi mjini Dodoma.
Alisema viongozi wanaopatikana kwa njia ya rushwa siyo viongozi bora na kuhoji, “Hivi mtu anayetumia fedha kuingia madarakani akipata madaraka fedha hizo atazirudishaje?”
Pinda ametaka jumuiya hiyo kuwa mstari wa mbele kusimamia uendeshaji wa chaguzi ndani ya chama kwa misingi ya maadili, kwani wanaomwaga fedha ili kupata uongozi ndani ya chama wanawavuruga na hiyo siyo njia ya kukijenga chama.
Pinda aliwaasa wanachama wa CCM waache kupanga nani agombee na nani asigombee na kufafanua kuwa hali hiyo hujenga makundi ndani ya chama hicho.
“Tunahitaji kupata viongozi kwa kuzingatia umoja wetu na mshikamano miongoni mwa wanachama. CCM ikiwa imara itaunda Serikali imara. Chama kikiwa dhaifu ni wazi kuwa hata Serikali yake nayo itakuwa dhaifu,” alisema.

source: mwananchi

No comments:

Post a Comment