WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, February 21, 2014

Posho zapingwa kila kona


Slaa_1_2b62b.png

Dar es Salaam. Wakati maombi ya baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba ya kuongezewa posho yakipingwa kila kona, uongozi wa muda wa Bunge hilo umeunda kamati kuchunguza uhalali wa maombi hayo.
Juzi, ndani ya kikao cha Bunge hilo, baadhi ya wajumbe walieleza mahitaji yao ya posho kuongezwa wakisema kiwango cha Sh300,000 (Sh80,000 za kujikimu na Sh220,000 kwa kikao), hakitoshi
.
Baada ya maombi hayo, Mwenyekiti wa Muda wa Bunge, Pandu Ameir Kificho aliahidi kuliwasilisha suala hilo serikalini ili lifanyiwe kazi, lakini jana aliamua kuunda timu ya wajumbe sita kuchunguza uhalali wa posho hizo.
Posho kupingwa
Baadhi ya vyama vya siasa, wanaharakati na wananchi wa kawaida wameshangazwa na maombi hayo ya posho, wakisema wajumbe wamesahau kilichowapeleka bungeni na kukimbilia kutetea masilahi yao.
Vyama vya Chadema na CUF kwa nyakati tofauti, vilisema kuwa vitaanzisha juhudi za kuwataka wabunge wao ambao ni wajumbe wasusie agenda yoyote inayotaka kuongezwa kwa posho hizo.
Tamko la vyama hivyo limetolewa huku Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambacho wajumbe wake ndio wanaodaiwa kupigia debe mpango huo, kikisema kitatoa ufafanuzi juu ya hoja hizo baada ya kupata 'taarifa rasmi'.
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema jana kuwa wajumbe hao hawakupaswa kudai nyongeza ya posho kwa vile hawakutumwa kwenda Dodoma kudai marupurupu ya fedha.
Alisema kuanza kujadili suala la nyongeza ya posho badala ya kuzungumzia hoja za msingi zilizopo kwenye Rasimu ya Katiba, ni sawa na kuwapuuza wananchi ambao wanasubiri kupata Katiba Mpya.
"Wametoka kwenye hoja na kutupeleka kwenye mambo mengine ambayo hayana msingi wowote. Sisi kama Chadema tunapinga na tunataka wabunge wetu watambue hilo," alisema.
Alisema wale wanaolalamika kwamba Sh300, 000 hazitoshi wanajaribu kupindisha ukweli, kwani kuna baadhi ya watumishi wa Serikali wanalipwa kiasi hicho ikiwa ni mshahara wao wa kila mwezi.
Alisema Chadema kimewataka wabunge wake kutojiingiza kwenye malalamiko hayo badala yake wazingatie kile walichotumwa na wananchi kwenda Dodoma

Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro alisema amesikitishwa na maombi hayo ya posho na kuahidi kuanzisha kampeni ya kuyakwamisha kwa sababu hayana tija kwa wananchi.

"Tunafahamu kuwa kuna njama zinapangwa ili wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba waongezewe fedha zaidi, binafsi na wenzangu wengi tumepanga kutumia kila uwezo kuzuia nia hiyo ovu. Ifikie wakati tuambiane ukweli, vinginevyo nchi hii watu watakufa maskini," alisema Mtatiro ambaye pia ni mjumbe wa Bunge hilo.

"Sh300,000 tunazopewa kwa siku zinatosha kabisa, ambaye hazimtoshi aongeze za kwake na ambaye anaona hawezi kuongeza fedha zake aondoke Dodoma ili kupisha wanaoweza kutunga Katiba waendelee." Alipotakiwa kutoa msimamo wa CCM kuhusiana na hatua hiyo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye alisema: "Sina chochote cha kuzungumza sasa hadi pale nitakapoletewa taarifa rasmi kwani siwezi kufanya kazi kupitia magazeti."

Akizungumzia posho hizo, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba alipinga madai kwamba viwango vilivyotangazwa vya wajumbe wa Bunge la Katiba (Sh300, 000) kwa siku ni pungufu kwa vilivyotolewa kwa wajumbe wa Tume.

Bila ya kutaja kiwango alisema: "Ninachofahamu, posho ya wajumbe wetu ilikuwa chini ya hiyo."
Hata hivyo, taarifa kutoka ndani ya tume hiyo, zinaeleza kuwa wajumbe hao walikuwa wakipokea Sh200,000 kwa siku.

Kuhusu madai kwamba kazi inayofanywa na Bunge Maalumu la Katiba ni nzito kuliko iliyofanywa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Warioba alisema hawezi kupima uzito wa kazi ya Tume kwa kuilinganisha na inayofanywa na Bunge la Katiba na hafahamu waliotoa madai hayo wametumia utaalamu gani
Kamati yaundwa

Kutokana na kupanda kwa joto la posho hiyo, jana asubuhi, Kificho alitoa maelezo kwa wajumbe kuwa uongozi unatafakari namna bora ya kuwafanya wajumbe waishi kwa amani mjini Dodoma.
"Kwanza tulikubaliana kuwa kikao kianze leo (jana) saa nne asubuhi, lakini tumechelewa kwa sababu muhimu, kwani lazima mtambue kuwa kila jambo mnalozungumza hapa halitupwi kama jiwe," alisema Kificho na kuongeza:

"Mlinituma tuzingatie namna gani tutakaa Dodoma kwa amani, ili tuweze kumudu na kuishi vizuri katika kazi hii nzito iliyoko mbele yetu."
Alisema kuwa walikuwa wameshauriana na wataalamu wake ambao ni makatibu na kukubaliana kuunda timu ya kufuatilia na kuishauri Serikali jinsi ya kuongeza posho hizo

Aliwataja walioteuliwa kuunda timu hiyo kuwa ni, William Lukuvi, Mohamed Aboud Mohamed, Freeman Mbowe, Paul Kimiti, Asha Bakari na Jenister Mhagama.
Wakati akiitangaza timu hiyo iliyopaswa kuanza kazi yake jana, jina la Lukuvi ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge) lilizua kelele kutoka miongoni mwa wajumbe wakipinga uteuzi wake.

"Hatufai huyo, hatufai huyo, hilo jina liondoeni na kulitupa kapuni kwani mbona wapo wengine, kwa nini mkaingiza jina la Lukuvi?" zilisikika sauti za juu kutoka ndani ya ukumbi, lakini lilipotajwa jina la Mhagama wajumbe wengi walishangilia.

Imeandikwa na George Njogopa, Editha Majura na Habel Chidawali

source:  Mwananchi

No comments:

Post a Comment