WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Saturday, September 14, 2013

Wabunge wamesahau vyama vitapita, Tanzania itadumu



ZIMEKUWEPO na zitaendelea kuwapo tafsiri nyingi juu ya vurugu zilizotokea bungeni Alhamisi ya juma lililopita. Tafsiri hizi zinahusu mitazamo ya kisheria, kijamii, kisiasa, kiuchumi, kihistoria na mingine. Ilimradi kila aliyesikia ama kushuhudia atakuwa na tafsiri ya aina yake.

Pamoja na ukweli kuwa Bunge la Tanzania sio la kwanza duniani ‘kuruhusu’ vurugu au ngumi ndani ya ukumbi wa mikutano ya Bunge, ni dhahiri hili lililotokea hapa kwetu wengi wamelichukulia kwa mzito mkubwa. Hivyo mitazamo inayoendelea kujadiliwa juu ya hili yamkini ni mahsusi kwa ustawi wa taifa; na inalenga kutusaidia kutafakari wapi tulipopotoka ili tuweze kujinasua.

Kwa kuwa tafsiri na mitazamo ipo ya aina nyingi, nachagua kutafakari na kujadili mustakabali wa utaifa na uzalendo wetu, mintarafu ukada au upenzi wetu kwa vyama vyetu vya siasa.

Kwa kipindi kirefu sasa tumeshuhudia jinsi mchakato wa uandaaji wa Katiba mpya ulivyogeuzwa kuwa mtaji au chambo cha baadhi ya vyama vya siasa kukubalika zaidi kwa umma. Hii imeanzia kwenye wazo lenyewe la umuhimu wa kuwepo kwa mchakato huu wa kuandika Katiba mpya.

Inajulikana wazi kuwa nyakati, mabadiliko na mahitaji ya Watanzania yalikuwa yanalazimu tu kuwepo kwa mchakato wa Katiba mpya. Hata hivyo, wakati mchakato ukiwa umeshaanza, ilikuwa nusura hoja ya nani ndio aliyesukuma uanzishwaji wa mchakato huu (badala ya mchakato wenyewe)kuwa ndio hoja kuu.
Kwa watu walio wastaarabu na wenye busara, hapakuwa na haja ya malumbano juu ya hili. Badala yake kama ukweli unajulikana kuwa mahitaji ya nyakati ndio yalikuwa mwasisi wa jambo hili, ikijumlishwa na wale waliokuwa mstari wa mbele kulisemea (waasisi namba mbili), ukweli huu ilipaswa watu kuukiri, na baada ya hapo kusonga mbele. Lakini sasa, mzimu huu wa ‘nani ndiye mwasisi’ wa Katiba (chini ya miamvuli ya vyama vya siasa) inaonekana unaendelea kututafuna kwa mtindo mwingine.

Mtindo huu ulioanzia katika ubishani wa nani ‘Mwasisi wa Katiba’, umegeukia kwenye nani anataka maslahi yake na chama chake yazingatiwe zaidi (yote) katika rasimu hii tuliyonayo hivi sasa. Mtindo huu ambao ndio unavuruga mchakato wa uandaaji wa Katiba mpya wanayoihitaji sana Watanzania, umewafanya baadhi ya watu kulewa kabisa na mapenzi ya U-chama. Wamesahahu kuwa Katiba hii ni ya nchi na wananchi wa Tanzania; vyama ni matokeo tu ya Katiba imara inayozaa taifa imara.

Ni ulevi huu wa mapenzi ya vyama vyao umepelekea baadhi ya vyama na watu wao kufanya vurugu katika mabaraza ya katiba. Ni ulevi huu huu umepelekea vurugu za bungeni juma lililopita. Kwa ulevi huu, baadhi yetu (ikiwemo wabunge) wameacha kuzingatia (kwa makusudi) kanuni za demokrasia kuwa pande mbili zenye mitazamo tofauti lazima zifikie mahali pa kukubaliana, penye kukidhi lengo lililo kuu zaidi.

Kidemokrasia, kukubaliana kati ya pande mbili kunategemea uzito au nguvu ya hoja, huku kanuni mbili yaani ya ‘wengi wape’, na ile ya ‘hekima au busara ya wachache pia itumike (isibezwe)’ zikitiliwa maanani sana.

Kwa mantiki hii, maslahi ya vyama hayapaswi kuwa juu ya lengo kuu ambalo Watanzania wote wenye mapenzi mema na nchi yao wanataka litimizwe. Nalo ni kupata Katiba iliyoandaliwa na wananchi wenyewe na inayokidhi mahitaji yao kwa kadri wanavyotaka.
Tukirejea kilichotokea bungeni juma lililopita, ni dhahiri kuwa ni wengi waliohusika kwa namna ya moja kwa moja au nyingine kusababisha kadhia ile. Kwa mfuatano wa jinsi matukio yalivyokuwa, masuala kadhaa yamewashawishi walio wengi kuamini kuwa ulevi wa mapenzi ya vyama vya siasa ilikuwa ni sababu mojawapo kubwa iliyolifikisha bunge katika hali ile.

Kwa kuanzia, kitendo cha Naibu Spika Job Ndugai kuwa mbogo na kumkatalia katakata fursa ya kuongea Kiongozi wa Upinzani bungeni, Freeman Mbowe, ambaye ni Waziri Mkuu kivuli hakikuwa cha busara wala mantiki. Kwa nafasi yake, Mbowe alipaswa kusikilizwa. Laiti kama Ndugai angetumia busara kidogo tu, kadhia yote ile isingetokea.

Lakini pia manung’uniko kwamba Wazanzibar hawajashirikishwa inavyopaswa katika kutoa maoni kwa kamati ya bunge juu ya muswada huo wa marekebisho ya  sheria ya mabadiliko ya katiba hayakuwa ya kubeza kiasi kile. Pamoja na taarifa kutoka kwa Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar kuonesha kuwa Wazanzibari walishirikishwa, kitendo cha wabunge wa CUF (ambao ni sehemu ya serikali ya Zanzibar) kuendelea kupinga taarifa hiyo ya Makamu wa pili wa Rais kilipaswa kuchukuliwa kwa uzito unaostahili.

Kitendo cha Bunge kuendelea na upitishaji wa muswaada huo bila wabunge karibia asilimia 90 wa kambi ya upinzani nacho kimetia doa mchakato mzima. Hii pia si ishara njema kwa hatua nyingine zitakazoendelea katika mchakato mzima wa upatikanaji wa Katiba mpya ya Watanzania. Ikumbukwe kuwa wabunge hao wa kambi ya upinzani wanawakilisha maelfu ya Watanzania. Na hivyo wananchi wanaowakilishwa wangependa pia maoni yao yasikike kupitia kwa wawakilishi wao hao.

Kingine ambacho kiliendelea kulipunguzia bunge heshima na staha yake ni kitendo cha baadhi ya wabunge wa CCM waliobaki ukumbini, badala ya kujadili muswada, walitumia muda mwingi kuwarushia vijembe na kejeli wenzao wa upinzani waliokuwa wametoka. Hili nalo halikuwa na tija yoyote kwa wananchi waliowatuma kuwawakilisha, na kusimamia kwa ubora kabisa maslahi ya wananchi hawa.

Kwa kuzingatia hayo yaliyotokea bungeni, na mengine mengi ambayo yameshuhudiwa katika mchakato huu wa kuandaa katiba mpya, inabidi hatua madhubuti zichukuliwe ili kuweka mambo sawa huko tunakoelekea kwa manufaa ya taifa na vizazi vijavyo. Kwa kuanzia kabisa, Rais Jakaya Kikwete, kwa mamlaka aliyo nayo hana budi kuokoa jahazi ama kwa kuurejesha muswada huo ujadiliwe tena bungeni au kwa njia nyingine yoyote itakayofaa.

Pamoja na hayo, wabunge, viongozi wengine na wananchi kwa ujumla sharti tutambue kwamba lengo mahsusi na lililo kuu ni kutengeneza Katiba iliyo bora ambayo itadumisha taifa lililo bora. Mapenzi kwa vyama yasiwe chanzo cha kuwa na Katiba ya hovyo. Tukumbuke kuwa vyama hivi vitapita lakini taifa litaendelea kuwepo.

No comments:

Post a Comment