WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Thursday, September 19, 2013

JK: Tutakabiliana na wauza ‘unga’ kwa nguvu zote;

jk_dawa_3bea9.jpg

Wakati Rais Jakaya Kikwete akisema Serikali yake haitawatetea Watanzania wanaokamatwa wakijishughulisha na biashara ya dawa za kulevya, Watanzania wawili Agnes Masongange na mwenzake, Melisa Edward jana walinyimwa dhamana na Mahakama Kuu ya North Gauteng katika kesi ya dawa ya kukamatwa na dawa hizo

Rais Kikwete alisema Serikali yake itakabiliana na biashara hiyo kwa nguvu zote kwa kuwa ni haramu na ni kinyume na sheria za nchi.

Alisema hayo juzi usiku alipokutana na Watanzania wanaoishi katika Jimbo la California, Marekani..."Serikali yangu haitawatetea watu wanaojishughulisha na ubebaji wa dawa za kulevya na kusafirisha nje ya nchi. Hii ni biashara haramu na inavunja sheria za nchi yetu."

Masogange na Melisa walikamatwa Julai 2, mwaka huu kwenye Uwanja wa Oliver Tambo, Afrika Kusini wakituhumiwa kusafirisha kilo 150 za dawa za kulevya zenye thamani ya Sh6 bilioni.

Aidha, amesema hayo siku chache baada ya meli ya mizigo ya Gold Star iliyosajiliwa nchini kukamatwa na maofisa forodha na askari wa doria wa Italia katika Pwani ya Sicily, Bahari ya Mediterranean ikiwa na tani 30 ya dawa ya kulevya aina ya bangi zenye thamani ya Paundi za Uingereza 50 milioni (Sh125 bilioni).

Pia, Agosti 31, mwaka huu, mshambuliaji nyota wa zamani wa timu ya soka ya Simba na Taifa, Joseph Kaniki 'Golota' na bondia Mkwanda Matumla walikamatwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Bole, Addis Ababa walipokuwa wakijiandaa kwenda Paris, Ufaransa wakituhumiwa kubeba dawa za kulevya.

Juzi, Rais Kikwete alisema ni wajibu wa Watanzania wanaoishi ughaibuni kuwa raia wema, kufuata na kuheshimu sheria katika nchi wanazoishi kwa sababu wakizivunja, Serikali yake haitawatetea.

"Ukikamatwa na dawa za kulevya hatukutetei kwa sababu hata sheria za nchi yetu zinazuia biashara hiyo. Sisi hatuwezi kuendelea kuwa na sifa ya kufanya biashara za ovyoovyo kiasi hicho. Serikali itawatetea Watanzania wanaoishi nchi za nje ikiwa wataonewa. Lakini ukifanya biashara ya dawa ya kulevya au kubaka watu hatukutetei kamwe," alisema.
Masogange, Melisa wakwama dhamana

Masogange na mwenzake Melisa jana walikosa dhamana baada ya kupandishwa kizimbani katika Mahakama Kuu ya North Gauteng, Afrika Kusini kujibu mashtaka ya kusafirisha dawa zinazodaiwa kutumika kutengenezea dawa aina ya amphetamine (maarufu kama tik).

Taarifa kutoka Mahakama hiyo zinaeleza kuwa, Masogange na Melissa walirudishwa rumande na kesi yao itasikilizwa tena Novemba mwaka huu.

Mkuu wa Kitengo cha Kudhibiti Dawa za Kulevya cha Polisi nchini, Kamanda Godfrey Nzowa alithibitisha kuwa watuhumiwa hao walipanda kizimbani jana kujibu mashtaka yanayowakabili ya kusafirisha dawa za kulevya na kwamba wamerudishwa rumande hadi Novemba.

Awahoji akina Masogange Nzowa alisema alikwenda Afrika Kusini kuwahoji Melisa na Masogange kabla ya kupandishwa kizimbani lakini alisema hawakumpa ushirikiano.

Kamanda huyo alisema imebainika kuwa mzigo walioubeba wasichana hao haukuwa dawa halisi za kulevya, bali kemikali zinazotumika kutengeneza dawa zinazoitwa amphetamine. Kutokana na madai hayo, Nzowa alisema wanaweza kupewa dhamana na kesi yao kuendelea kusikilizwa nchini baada ya yeye (Nzowa) kushauriana na Kitengo cha Dawa za Kulevya cha Afrika Kusini.

Alisema, inawezekana watuhumiwa wakapewa hukumu nyepesi kidogo kutokana na kosa hilo.

Chanzo:Mwananchi

No comments:

Post a Comment