WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Monday, September 30, 2013

Kufungiwa magazeti: Wahafidhina sasa wanaongoza @ZittoKabwe

Imeandikwa na Zitto Kabwe, Mb — Kwa mshtuko na masikitiko makubwa kuanzia jana jioni tumepokea taarifa za kufungiwa kwa magazeti mawili ya kila siku hapa nchini ya Mwananchi na Mtanzania. Serikali imechukua uamuzi huo kwa kutumia sheria ya kidikteta ya magazeti ya mwaka 1976 ambayo Tume ya Jaji Francis Nyalali iliiorodhesha kama sheria kandamizi. Sababu zilizotolewa kuhalalisha uamuzi huu ni sababu zisizo na maana na ambazo Serikali ingeweza kufungua mashtaka ya kawaida kabisa mahakamani kushtaki magazeti hayo iwapo haikupendezwa na habari walizochapisha.

Moja ya sababu ya kufungiwa kwa gazeti la Mwananchi ni kuchapisha taarifa kuhusu mishahara ya Serikali. Serikali inasema habari hii ni siri. Serikali hii hii ambayo imesaini makubaliano ya kuendesha serikali kwa uwazi (Open Government Initiative) na kumwagiwa sifa na Rais Barack Obama wa Marekani inalifungia gazeti kwa kuandika habari za mishahara ya watumishi wa Serikali. Mishahara kuanzia mshahara wa Rais mpaka wa mtendaji wa Kijiji haipaswi kuwa jambo la siri. Kuonyesha kuwa
jambo hili linapaswa kuwa wazi mkutano ujao wa Bunge tutatafuta kila namna kutaja mshahara wa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na baadhi ya Watendaji wa Mashirika makubwa ya Umma kama njia ya kuwaunga mkono gazeti la Mwananchi kwa habari yao hiyo. Mapato ya Mbunge yanajulikana sasa kuwa ni shilingi milioni 11.2 kwa mwezi kabla ya kuongeza posho za vikao za shilingi laki 200,000 kwa siku na posho ya kujikimu ya shilingi 130,000 kwa siku. Watanzania wana haki ya kujua wanawalipa kiasi gani watumishi wao. Tutaanza na mshahara wa Rais!

Gazeti la Mtanzania limefungiwa pamoja na mambo mengine kwa kuandika 'mapinduzi ni lazima'. Inashangaza Serikali ya Chama cha Mapinduzi inaogopa neno mapinduzi. Marehemu Mzee Steven Salum Nandonde, aliyekuwa mbunge wa Jimbo la Tandahimba alipata kusema bungeni kuwa 'lazima nchi ipinduliwe'. Ni matumizi ya lugha tu. Mzee Nandonde yeye alikuwa analalamikia maendeleo duni ya mikoa ya kusini na kutaka Kaskazini iwe Kusini na Kusini iwe Kaskazini. Serikali inafungia gazeti kwa sababu ya kuandika Mapinduzi ni lazima ilhali kila siku Zanzibar wanasema Mapinduzi daima!

Gazeti la Mtanzania linahaririwa na Absalom Kibanda, mwandishi wa habari ambaye bado anaponya majeraha ya mwili na kisaikolojia ya kuteswa na watu ambao mpaka leo hawajakamatwa. Badala ya Serikali kuwakamata watesaji wa Kibanda, inamnyima kazi Kibanda ili ateseke kwa njaa kwa kukaa miezi mitatu bila kazi. Pia wanatutesa Watanzania kwa njaa ya kupata habari ambayo ni haki ya msingi ya kikatiba. Hii ndio zawadi Serikali inampa Kibanda baada ya kung'olewa kucha, kunyofolewa jicho, kukatwa vidole na kuteswa kwa namna isiyoelezeka.

Matukio ya hivi karibuni na namna Serikali inavyoyachukulia yanaonyesha dhahiri kwamba Rais Kikwete kazidiwa nguvu na kundi la wahafidhina ndani ya chama na Serikali yake. Rais ambaye alianza kwa kuhubiri uvumilivu wa hali ya juu na hata yeye mwenyewe kupata kusema uvumilivu huu wengine wanauona kama udhaifu lakini ameamua kujenga Taifa la kuvumiliana. Rais alipata kulalamika hadharani kwamba kuna wenzake wanataka aongeze ukali. Ni dhahiri kundi hili la wahafidhina sasa ndio linalomwongoza Rais Jakaya Kikwete. Kitu kimoja tu Rais azingatie, kundi hili linaongozwa na maslahi binafsi ya kubakia kwenye utawala wakati yeye anapaswa kuacha 'legacy'. Rais Kikwete asipokuwa makini atakuwa Rais karatasi (lame duck) tu tunapoelekea mwisho wa utawala wake. Maamuzi ya hovyo na ya kidikteta ya kufungia magazeti yanamchora vibaya mbele ya wananchi na jamii ya kimataifa. Wahafidhina kuwa nguvu zaidi ya kiutawala ni makosa ambayo watanzania hawapaswi kuyakubali kamwe.

Wananchi sasa waifanye Serikali kujutia uamuzi wake wa kufungia magazeti. Nimeamua mimi binafsi kama mbunge kesho Jumatatu tarehe 30 Septemba, 2013 kupeleka taarifa rasmi kwa Katibu wa Bunge ya kupeleka muswada Bungeni wa kuifuta kabisa Sheria kandamizi ya magazeti ya mwaka 1976. Sasa tupambane na kundi dogo la wahafidhina ndani ya Serikali na CCM wasiopenda mabadiliko na iwe fundisho kwa wahafidhina wengine wowote waliopo ndani ya Serikali au nje ya Serikali kwamba Uhuru wa habari sio jambo la kuchezea kama gololi.

No comments:

Post a Comment