WHATEVER YOUR ARE BE A GOOD ONE;

A nation that is afraid to let its people judge the truth and falsehood in an open market is a nation that is afraid of its people. John F. Kennedy

“Taifa letu – taifa lolote – ni zuri na mahali pazuri pa kuishi kama raia wake watalifanya liwe hivyo. Uongozi wake unaweza kuwa mzuri, mbaya au usiojali lakini kama watu wake wameamka (ki-elimu?) na wanajitambua, haitachukua muda mrefu kuwakilisha mtazamo wa jamii na kubadili mawazo na matumaini ya taifa.” Julius Kambarage Nyerere


Friday, June 20, 2014

MTEI ALEZEA KIZUNGUMKUTI CHA HISA ZA WANZANZIBARI KATIKA EAC-BANK ILIYOVUNJIKA.


Edwin Mtei Kuzaliwa:  Mwaka 1932, Marangu Mkoani Kilimanjaro Kazi: Gavana wa Kwanza wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) •Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki •Waziri wa Fedha chini ya uongozi wa Mwalimu Nyerere  Elimu: Shahada ya Sanaa (Sayansi ya Siasa na Historia na Jiografia) Siasa: Mwanzilishi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) 

Arusha. Kero za Muungano zimetokea kuwa msamiati maarufu katika siku za karibuni nchini, hasa pale ulipoanza mchakato wa kupatikana kwa Katiba mpya.
Wengi wamekuwa wakieleza kuwa kero zipo lukuki katika Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao umetimiza miaka 50 sasa.
Kero hizo zimetumika kama kete ya kutetea muundo unaofaa wa Muungano ingawa mjadala sasa umehamia kwenye  serikali mbili au tatu.
Hata hivyo, katika kero hizo, zipo ambazo zimeanza kupatiwa ufumbuzi na zipo ambazo zimeibuka upya tena kwa kasi.
Miongoni mwa kero ambazo ni ngeni kwa wengi, ni kutokujulikana zilipopelekwa fedha za Zanzibar zilizokuwa katika Bodi ya Sarafu ya Afrika  Mashariki  (EACB) iliyonjika mwaka 1965.
Kero hiyo, ilikuwa ikizungumzwa chini chini na baadhi ya viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) na hata wanasiasa wa pande zote mbili za Muungano.
Kutokana na watu wengi kuhoji, fedha hizo, wakati wa uzinduzi wa Bunge Maalumu la Katiba  mjini Dodoma, Rais Jakaya Kikwete naye alizungumzia kero hiyo na kuahidi kuwa itafanyiwa kazi.
Hata hivyo, ili kupata maelezo ya kina juu ya kero hii, gazeti hili linazungumza na Gavana wa kwanza wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Edwin Mtei, ambaye pia aliyekuwa Waziri wa Fedha kati ya mwaka 1978 hadi 1981.
Mtei, ambaye pia aliwahi kuwa katibu mkuu wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC) na ameshika nafasi mbalimbali katika jumuiya hiyo kabla ya kuvunjika, anaeleza historia ya akiba hiyo ya Zanzibar na wapi ilipo.
Anasema ni kweli kuwa baada ya kuvunjika kwa EACB mwaka 1965, Zanzibar ilikuwa na akiba ya fedha zake katika bodi hiyo.
Anasema Zanzibar ilikuwa na kiasi cha fedha kama asilimia 4, huku Kenya, Uganda na Tanzania (Bara) zikiwa na kiasi kikubwa cha fedha.
Je, zipo wapi fedha za Zanzibar?
Mwanasiasa huyo anasema fedha hizo  baada ya kuvunjika kwa bodi hiyo, fedha hazipo tena na anashangazwa na watu wanaoibuka leo na kudai sasa kana kwamba bado zipo BoT.
Anasema anakumbuka wakati huo, mara baada ya kuvunjika kwa bodi hiyo, ulifanyika mgawanyo wa fedha katika hazina za nchi hizo kuanzisha benki kuu.
Anasema fedha za Tanzania Bara zilifanya kazi mbalimbali  na zile za   Zanzibar  ziliingizwa katika kazi ya kuanzishwa kwa tawi la BoT Zanzibar kwani wakati huo kulikuwa na tawi moja  lililokuwa Dar es Salaam.
“Nakumbuka fedha za Zanzibar tulitumia katika ujenzi wa BoT, tawi la Zanzibar, ujenzi ambao ulikuwa na gharama kubwa ukihusisha kujengwa kwa eneo maalumu la  kuhifadhi fedha hizo,” anasema Mtei.
Anaongeza kuwa kabla ya hapo, Zanzibar ilikuwa haina tawi la Benki Kuu hivyo, fedha hizo ndizo zilitumika kuanzishwa tawi la kwanza.
“Ni kweli kulikuwa na malalamiko ya Zanzibar baada ya bodi  kuvunjika, lakini hatukuzitumia fedha hizi kwa mambo mengine, ila tulifungua tawi la Benki Kuu Zanzibar,” anasema.
Anaeleza kuwa anachokumbuka ni kuwa fedha za Zanzibar zilikuwa asilimia nne katika jumuiya hiyo na kwa jumla Tanzania ilikuwa na asilimia 35 katika bodi hiyo.
“Kuanzisha  BoT Zanzibar  haikuwa kazi ndogo kwani ilibidi tutafute majumba strong (imara). Tujenge mahali pa kuhifadhi fedha na ujenzi ni gharama hasa  strong room (chumba maalumu cha kuhifadhi fedha), ” anasema Mtei.
Anaongeza kuwa kwa kumbukumbu zangu, wakati huo, kwenye vikao vya uamuzi huo, Zanzibar ilikuwa inaongozwa na Katibu wa Wizara ya  Fedha aliyemtaja kwa jina moja la Sheha.
“Sheha ndiye aliyekuwa anahudhuria vikao, alikuwa akija na kukutana nami tunajadili,” anasema.
 Serikali moja  EAC
Akizungumzia mvutano wa kisiasa kwa sasa, kutokana na mapendekezo ya rasimu ya Katiba mpya, anasema ni vyema maoni ya wengi yafuatwe na kuheshimiwa.
Hata hivyo, anasema  baada ya  Muungano kudumu kwa miaka 50, angetaka ndoto iwe ni kuwa na nchi moja katika ukanda wa Afrika ya Mashariki.
“Mimi  kama mchumi nataka nchi kubwa moja. Tuache kuzungumzia mambo ya kutugawanya, inawezekana kuna nchi ndogondogo lakini lazima ziunganishwe na kuwa moja kubwa kupitia Shirikisho la Afrika ya Mashariki,” anasema.
“Nchi hii ni moja ambayo nadhani tuanze kuifikiria sasa iwe na Tanganyika, Zanzibar, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na hata  Zambia na  Malawi
“Mimi nimejifunza katika political science (sayansi ya siasa) kuwa nchi inapokuwa moja kubwa, basi uchumi wake unastawi na watu wanapata maendeleo ya kiuchumi kuliko kuwa nchi ndogo,” anasema.
Anaongeza, hata hivyo, kuwa ni vyema kujiuliza ni kwa nini miaka 50 ya Muungano sasa, bado Watanzania wengi ni maskini?
“Lazima, tufikirie mbele zaidi, kwenye vikao vya umoja wa mataifa, zinapozungumza nchi kubwa, utaona kabisa kila mjumbe anakuwa makini na hata kama yupo nje anarudi kusikiliza, lakini kama ni nchi ndogo wajumbe wanatoka kuvuta sigara nje ya ukumbi.”
 Anaongeza kuwa Watanzania na wakazi wa ukanda wa Afrika ya Mashariki wanapaswa kufikiria kuwa na nchi moja kubwa kama Marekani, Ujerumani  au Brazil kama kweli wanataka kukuza uchumi wao.
Muungano ni maridhiano.
Akizungumza muundo wa Muungano, Mtei  anasema ni muhimu kuwapo kwa Muungano ambao unaridhiwa na nchi zote wanachama.
Anasema Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni lazima uendelezwe na kulindwa, lakini, kwa kuzingatia masilahi na maridhiano ya kila upande.
“Tuwapinge wote ambao wanataka kuvunja Muungano, pia tuondoe kero zote zilizopo kwani Muungano ni makubaliano ya watu wote kwa masilahi yao,” anasema.
Mtei ambaye ni muumini wa Kilutheri ana historia ndefu ya maisha ambayo yanafurahisha. Ni mtu ambaye alilelewa na mama yake mzazi na kukulia katika maisha ya umaskini, akichunga mbuzi baada ya kutoka shule ya Ngaruma iliyokuwa ikimilikiwa na Kanisa la Kiinjili la  Kilutheri Tanzania. Baadaye alikwenda  Old Moshi, Tabora, kisha Chuo Kikuu Makerere, Uganda.
source: mwananchi

No comments:

Post a Comment